TANGAZO


Sunday, January 4, 2015

Rais Dk. Shein: Lengo la Mapinduzi ni kuleta maendeleo endelevu kwa wananchi wote

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa  Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein akisalimiana na Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano Juma Duni Haji Viongozi wakati alipowasili leo katikauzinduzi wa Barabara ya Njia nne-Umbuji Wilaya ya Kati Unguja ikiwa ni katika  shamra shamra za kutimiza miaka 51 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar. (Picha zote na Ikulu)
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa  Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (katikati) akikata utepe  kufungua Barabara ya Njia Nne-Umbuji Wilaya ya Kati Unguja leo iliyojengwa na Serikali kupitia kitengo cha Idara ya ujenzi Barabara UUB ikiwa ni katika  shamra shamra za kutimiza miaka 51 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar (kulia) Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano Juma Duni Haji na (kushoto) Mkuu wa Mkoa Kusini Unguja Dk. Idriss Muslim Hija.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa  Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  akifungua pazia kama ishara ya   kufungua Barabara ya Njia Nne-Umbuji Wilaya ya Kati Unguja leo iliyojengwa na Serikali Mapinduzi kupitia kitengo cha Idara ya ujenzi Barabara UUB ikiwa ni katika  shamra shamra za kutimiza miaka 51 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar  (kushoto) Mkuu wa Mkoa Kusini Unguja Dk. Idriss Muslim Hija.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa  Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (katikati) akifuatana na Viongozi mbali mbali wakitembea katika Barabara ya njia nne -Umbuji Wilaya ya Kati Unguja mara baada ya kuifungua rasmi leo ikiwa ni katika shamra shamra za kutimiza miaka 51 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.
Katibu Mkuu Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Dk.Juma Malik Akili,akitoa ripoti ya kitaalamu leo wakati wa sherehe za Ufunguzi wa Barabara ya Njia Nne -Umbuji Wilaya  ya Kati Unguja baada ya kufunguliwa na Mgeni rasmi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa  Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein  ikiwa ni katika shamra shamra za kutimiza miaka 51 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.
Wananchi na wafanyakazi wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano wakiwa katika sherehe za ufunguzi wa Barabara ya Njia Nne -Umbuji Wilaya  ya Kati Unguja baada ya kufunguliwa na Mgeni rasmi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa  Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  ikiwa ni katika shamra shamra za kutimiza miaka 51 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa  Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein akitoa hutuba yake wakati wa sherehe za Ufunguzi wa Barabara ya Njia Nne -Umbuji Wilaya  ya Kati   Mkoa wa Kusini Unguja  zilizofanyika leo kijiji cha Umbuji ikiwa ni katika shamra shamra za kutimiza miaka 51 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar.
Msoma Risala Farida Rajab  akisoma risala hiyo mbele ya mgeni rasmi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa  Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein wakati wa ufunguzi wa Barabara ya Njia Nne-Umbuji Wilaya ya Kati Unguja ikiwa ni   katika shamra shamra za kutimiza miaka 51 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar.


Na Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa lengo la Mapinduzi Matukufu ya Januari 12, 1964 ni kuleta maendeleo endelevu kwa wananchi wote popote pale walipo tena bila ya ubaguzi wa rangi, dini, kabila ama kwa itikadi ya kisiasa.



Dk. Shein aliyasema hayo leo huko Umbuji, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja katika  uzinduzi wa  barabara ya  Njia nne- Umbuji iliyojengwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia Mfuko wake wa Barabara, ikiwa ni miongoni mwa maadhimisho ya miaka 51 ya Mapinduzi ya Zanzibar ambapi pia, Dk. Shein aliridhia barabara hiyo kuitwa jina lake kama alivyoobwa na wananchi wa kijiji hicho.

Katika uzinduzi huo viongozi mbali mbali wa vyama na Serikali pamoja na wananchi walihudhuria akiwemo Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd.

Katika hotuba yake aliyoitoa mara baada ya kuizindua barabara hiyo yenye urefu wa  kilometa 5.1, Dk. Shein alisema kuwa suala la maendeleo halina mjadala na haliusiani kabisa na itikadi za vyama vya siasa kwani misingi ya kuwepo kwa vyama vya siasa ni maendeleo kwani hiyo ndio nia ya Serikali anayoiongoza.



Dk. Shein alisema kuwa  Serikali ina wajibu wa kuwapelekea maendeleo wananchi wake popote pale walipo na ndio maana imechukua juhudi za makusudi za kuwajengea barabara wananchi wa kijiji cha Umbuji ikiwa na azma ya kuwafikishia maendeleo wananchi wake.

“Leo suala la barabara kwa wananchi wa Umbuji tumelimaliza na kama alivyosema Katibu Mkuu wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano lengo ni kuhakikisha barabara hii inajengwa hadi Uroa hatua kwa hatua...jambo ambalo lilikuwa linaniumiza roho basi ni barabara hii ya Umbuji”,alisema Dk. Shein.



Aidha,  Dk. Shein alisema Zanzibar itajengwa na Wazanzibari wenyewe kwani hilo ndio lengo la Mapinduzi matukufu ya Januari 1964 huku akieleza kuwa wazee wameanza kutekeleza juhudi za maendeleo na hivi sasa vizazi viliopo ni lazima viendeleze kwani hilo ndio lengo la Mapinduzi.

Dk. Shein alisema kuwa wakati Zanzibar inaadhimisha miaka 51 ya Mapinduzi tayari kuna mtandao mzuri wa barabara nchi nzima hali iliyowezesha kuunganisha vyema miji na vijiji katika maeneo yote ya Unguja na Pemba na kutoa pongezi kwa uongozi wa Wizara hiyo kwa ujenzi wa barabara hiyo sambamba na nyenginezo zinazoendelea.

Alisisitiza kuwa hizo ni juhudi za makusudi zilizochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kutafsiri kwa vitendo shabaha ya Mapinduzi kwa kuwafikishia huduma wananchi wake wote popote walipo tena bila ya ubaguzi huku akiahidi utekelezwaji wa ombi lao la ujenzi wa barabara ya Pagali hatua kwa hatua.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kwa kuwanasihi madereva wakataotumia barabara hiyo kuzingatia sheria za usala wa barabarani kwa kuacha kwenda mwendo wa kasi, kutopakia abiria zaidi ya kiwango kilichokubaliwa sambamba na kuacha kufanya matengenezo ya magari barabarani.



Pia, Dk. Shein aliwataka wananchi kuwacha kutumia barabara kama vikao vya mazungumzo na kutoa agizo kwa wananchi kufuata taratibu zilizowekwa  za hifadhi ya barabara kwa kutojenga katika maeneo yaliowekwa viguzo wala kufanya shughuli nyengine zozote kwani maendeleo yanazidi kuimarika kwa hapo baadae njia inawezekana ikawa ndogo na ikahitaji kupanuliwa.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliwahakikishia wananchi wa Umbuji kuwa Serikali imo katika mchakato wa kujenga kituo kipya cha Afya katika kijiji chao na kuwataka waendelee kuwa na subira kwa hilo huku akitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa wananchi wa Umbuji kukataa kulipwa fidia wakati wa ujenzi wa barabara hiyo.

Katika maelezo yake Dk. Shein aliwaeleza wanakijiji wa Umbuji kuwa haikuwa jambo la makusudi Serikali kuchelewesha ujenzi wa barabara hiyo bali hali hiyo imetokana na kuwepo kwa uhaba wa vifaa vya ujenzi wa barabara hapa nchini jambo ambalo serikali imo katika juhudi ya kulipatia ufumbuzi. 
 

Nae Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano Mhe. Juma Duni Haji alisema kuwa ni mfano wa kuigwa kwa kitendo cha wanakijiji wa Umbuji kukataa kulipwa fidia wakati wa kupitisha ujenzi wa barabara hiyo kitendo ambacho ni cha kizalendo na kueleza matumaini yake ya kuimarika kwa maendeleo katyika kijiji hicho kutokana na barabara hiyo.

Mapema Katibu Mkuu wa Wiza hiyo Juma Malik Akil alisema kuwa ujenzi wa barabara hiyo ulianza mwaka mwishoni mwa mwaka 2009 na kuendelea hadi  Oktoba 2013 katika hatua ya kifusi na kukamilika rasmi Novemba 24 mwaka jana kwa kiwango cha lami.

Alisema kuwa kukamilika kwa ujenzi wa barabara hiyo kunatokana na jitihada na ahadi za Dk. Shein katika kuwapelekea wananchi maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi.


Alisema kuwa barabara hiyo ina uwezo wa kupita magari kwa kasi ya mwendo wa kilomita 60 kwa saa na yenye uzito unaofikia tani 15 ambapo pia, barabara hiyo ni ya mwanzo kabisa kuwekewa viguzo vya hifadhi ya barabara katika kila upande wa barabara na kuwaomba wananchi kuziheshimu na kuzitunza alama hizo.

Aidha, alisema kuwa jumla ya fedha zilzotumika katika ujenzi wa barabara hiyo ni milioni 840.5, gharama ambazo ni nafuu zaidi ikilinganishwa na gharama halisi kutokana na kutengenezwa na wataalamu wa hapa nchini sambamba na kutumia malighafi za hapo hapo kijijini.

Alisema kuwa kutokana na juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha mfumo wa usafiri hivi sasa Zanzibar imefikia kuwa na mtandao wa barabara wenye jumla ya kilometa 1,235.52 (Unguja  kilometa 704.03 na Pemba kiloeta 531.50).



Nao wananchi katika risala yao walitoa shukurani kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein kwa kujengewa barabara yao hiyo na kumpongeza Dk. Shein kwa kutekeleza ahadi yake ya kujengwa barabara hiyo wananchi wa kijiji hicho.

Aidha, kwa umoja wao wananchi hao walimuomba akubali barabara hiyo kuitwa kuitwa jina lake kutokana na  juhudi zake za kuhakikisha kijiji hicho kinafikiwa na barabara ya lami ambayo itawasaidia katika shughuli zao za maendeleo ikiwemo kusafirisha bidhaa zao za kilimo pamoja na shughuli zao za kijamii.



Walieleza kuwa tayari kwa kiasi kikubwa huduma za maendeleo zimeshawafikia kama vile maji safi na salama, umeme, skuli za msingi na Sekondari, kituo cha afya pamoja na huduma nyengine muhimu ikiwemo huduma ya afya ambayo waliomba kujengewa kituo kipya cha afya cha kisasa ambapo Dk. Shein alisema kuwa tayari mchakato wake unaendelea.

Uzinduzi huo ulipambwa kwa burudani mbali mbali ikiwemo ngoma ya Kibati yenye asili ya Kisiwani Pemba katika Mkoa wa Kusini pamoja na utenzi pamoja na burudani nyenginezo.

No comments:

Post a Comment