TANGAZO


Saturday, November 26, 2022

WAZIRI MHAGAMA AZINDUA BODI YA WAKURUGENZI YA KWANZA YA MAMLAKA YA SERIKALI MTANDAO (EGA)

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akimkabidhi vitendea kazi Bw. Eric Shitindi ambaye ni mmoja wa Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), mara baada ya Waziri huyo kuizindua bodi hiyo jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) jijini Dar es Salaam, mara baada ya ya Waziri huyo kuizindua bodi hiyo. 

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Xavier Daudi akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kuzindua Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA).

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Dkt. Mussa Kissaka akitoa neno la shukrani kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama, mara baada ya Waziri huyo kuzindua Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA).

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Mhandisi Benedict Ndomba akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya eGA kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka hiyo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiwa katika picha ya pamoja Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), mara baada ya Waziri huyo kuizindua bodi hiyo jijini Dar es Salaam. Wa pili kutoka kulia ni Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI Bw. Xavier Daudi.

 

 

Na James Mwanamyoto, Dar es Salaam


WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amewataka Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) kusimamia vema utendaji kazi wa Serikali Mtandao ili kupunguza uwezekano wa wananchi kuathiriwa na vitendo vya rushwa.

 

Mhe. Jenista ametoa wito huo jijini Dar es Salaam, wakati akizindua Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) ambayo imepewa jukumu la kuisimamia Mamlaka hiyo kuhakikisha inatekeleza wajibu wake.

 

Mhe. Jenista amesema matumizi ya serikali mtandao yanawaepusha wananchi kukutana na watendaji hivyo kuondoa mazingira yanayoshawishi vitendo vya rushwa.

 

Amewataka Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya eGA kuweka mikakati madhubuti na imara itakayoiwezesha Serikali Mtandao kutatua changamoto zinazowakabili wananchi pindi wanapofuata huduma mbalimbali katika Taasisi za Umma.

 

“Ninasisitiza wajumbe wa bodi mjikite zaidi katika kuhakikisha mnaweka mikakati ya matumizi ya TEHAMA ambayo itaondoa changamoto ya upatikanaji wa huduma hasa kwa wananchi wa kawaida ambao Mhe. Rais amedhamiria kuwapatia huduma stahiki,”

 

Naye, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Xavier Daudi amesema kuwa, Wajumbe wa Bodi hiyo ya Wakurugenzi ya eGA wakitekeleza wajibu wao ipasavyo kwa kusimamia kikamilifu sera za serikali mtandao, wataisaidia Mamlaka ya Serikali Mtandao kulifikisha taifa katika uchumi wa kidijitali na mapinduzi ya nne ya viwanda, ikiwa ni pamoja na kuwezesha utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2025.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Dkt. Musa Kissaka amesema wajumbe wa bodi anayoiongoza wamepokea majukumu na maelekezo ambayo Mhe. Jenista ameyatoa, na kuahidi kuwa watajitahidi kadiri ya uwezo wao kufanya kazi kwa bidii na weledi katika kuisimamia na kuiongoza Mamlaka ya Serikali Mtandao.

 

Akizungumzia utekelezaji wa majukumu ya Mamlaka ya Serikali Mtandao, Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo, Mhandisi Benedict Ndomba amesema, mamlaka anayoiongoza imeendelea kusimamia na kuhimiza uzingatiaji wa Sheria, Kanuni, Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao katika Taasisi za Umma.

 

Mhandisi Ndomba ameongeza kuwa, Mamlaka ya Serikali Mtandao imeendelea kufanya kaguzi za mifumo ya TEHAMA, kufuatilia usalama wa Serikali Mtandao ikiwa ni pamoja na kufanya tafiti na kutoa mafunzo ya Serikali Mtandao kwa watendaji wa Serikali.

Tuesday, February 15, 2022

MAMLAKA YA SERIKALI MTANDAO YATEKELEZA AGIZO LA RAIS

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama, akizungumza. 
 

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama ameipongeza Mamlaka ya Serikali Matandao (eGA) kwa kutengeneza mfumo utakaowezesha mifumo mbalimbali ya Serikali kubadilishana taarifa, jambo hili ni hatua kubwa katika utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan la kuhakikisha mifumo ya TEHAMA ndani ya Serikali inawasiliana na kubadilishana taarifa wakati wowote.

Akizungumza na watumishi wa Mamlaka hiyo  jijini Dodoma, Waziri Mhagama amefurahishwa na utekelezaji wa haraka wa agizo hilo na kuahidi kutoa ushirikiano wa kutosha ili kuhakikisha mifumo yote ya TEHAMA inayotumiwa ndani ya Serikali inawasiliana na kubadilishana taarifa ili kurahisisha utoaji huduma kwa umma.

“Ninatoa pongezi nyingi kwa Mamlaka kwa kutekeleza agizo la Mhe. Rais kwa wakati na ninafahamu kuna baadhi ya taasisi za umma zimeshaunganishwa katika mfumo huo, hivyo ninaagiza kazi ya kuunganisha taasisi zilizobaki ikamilike kwa wakati na kufanya kazi kama ilivyodhamiriwa” Alisema Mhe.Mhagama.

Aidha, Mhe. Mhagama ametoa wito kwa watanzania kuendelea kutumia mifumo ya TEHAMA iliyobuniwa, kusanifiwa na kutengenezwa na wataalamu wa ndani katika shughuli zao za kila siku kwani zinarahisisha sana utendaji kazi, kupunguza gharama na mianya ya rushwa.

Pia, Mhe. Mhagama amesisitiza na kuwataka watumishi wa umma nchini kufanya kazi kwa kufuata maadili ya Utumishi wa Umma hasa wanapotumia mifumo ya kidijitali kwa uzalendo na uwajibikaji ili kumsaidia Mhe. Rais katika kuleta maendeleo ya haraka kwa wananchi kama kaulimbiu ya awamu ya sita ya “Kazi Iendelee” inavyosadifu.

Akiwasilisha taarifa ya utendaji wa Mamlaka ya Serikali Mtandao kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama, Mkurugenzi Mkuu wa eGA  Mhandisi Benedict Benny Ndomba amesema katika utekelezaji wa agizo la Mhe. Rais, Mamlaka imetengeneza mifumo mbalimbali ya TEHAMA ikiwemo Mfumo wa Ubadilishanaji Taarifa Serikalini (MUTAS) ambao mpaka sasa umeunganisha na unatumiwa na taasisi kumi kwa hatua ya majaribio.

Katika taarifa yake, Mhandisi Ndomba ameainisha baadhi ya mifumo mingine iliyotengenezwa na eGA kwa kushirikiana na taasisi husika na kwa kutumia wataalamu wa ndani kuwa ni Mfumo wa Ukusanyaji Malipo ya Serikali Kielektroni (GePG) unaosimamiwa na Wizara ya Fedha na Mipango, Mfumo wa Pamoja wa Utoaji Ankara kwa Mamlaka za Maji nchini (MAJIIS) unaosimamiwa na Wizara ya Maji, Mfumo wa Kusimamia Rasilimaliwatu Serikalini (New HCMIS) unaosimamiwa na Ofisi ya Rais Utumishi, Mfumo wa kusimamia Shughuli na Rasilimali za Taasisi (ERMS), Mfumo wa Ofisi Mtandao (e-Office) na Mfumo wa Baruapepe Serikalini (GMS).

Ziara hiyo ya Waziri Mhagama kwenye Ofisi ya Mamalaka ya Serikali Mtandao jijini Dodoma iliyofanyika Februari 11, 2022 ni sehemu ya kuzitambua taasisi zote zilizopo chini ya Wizara yake ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Tuesday, June 12, 2018

UFAFANUZI WA KUSITISHA HUDUMA ZA HABARI KWENYE BLOGU YETU HII KWA WADAU

NDUGU WADAU WETU TUMELAZIMIKA KUSITISHA UWEKAJI WA HABARI ZA KILA SIKU KWENYE CHOMBO CHETU HIKI KUTOKANA NA AMRI YA SERIKALI KUTUTAKA WAMILIKI WA BLOGU ZOTE AMBAZO HAZIJAPATA USAJILI KUSIMAMISHA KUWEKA HABARI YOYOTE YENYE MAUDHUI MPAKA HAPO ITAKAPOSAJILIWA RASMI; KWAHIVYO WADAU WETU TUNAPENDA KUWAFAHAMISHA KWAMBA TUMO KATIKA JUHUDI ZA KUTAFUTA UWEZO WA KUSAJILIWA RASIMI TUKIFANIKWA TUNATEGEMEA KURUDI HEWANI HARAKA IWEZEKANAVYO.

AHSANTENI KWA MAWASILIANO: 0715830004, 0773830004, 0767830004 NA 0789533331

MKURUGENZI MWENDESHAJI KASSIM MBAROUK RAJAB

Sunday, June 10, 2018

WAZIRI DKT TIZEBA AMALIZA ZIARA YA KIKAZI MKOANI SINGIDA ATUA TABORA

Waziri wa Kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akizungumza kwenye kikao kazi katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida. (Picha Zote Na Mathias Canal, WK. Juzi 8 Juni 2018)
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu (Kushoto) na Mkuu wa Wilya ya Singida Mhe Elias Tarimo wakifatilia kikao cha kazi kilichoongozwa na waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba, Juzi 8 Juni 2018.
Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe Dkt. Rehema Nchimbi akizungumza jambo mbele ya waziri wa kilimo Mhe Dkt. Charles Tizeba alipotembelea ofisi ya Mkoa akiwa katika ziara ya kikazi ya siku mbili, Juzi 8 Juni 2018.
Waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akizungumza kwenye kikao kazi katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida. Juzi 9 Juni 2018.

Na Mathias Canal-WK, Tabora
WAZIRI wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba amemaliza ziara ya kikazi ya siku mbili Mkoani Singida na tayari amewasili mkoani Tabora kwa ziara ya kikazi ya siku moja hapo kesho 10 Juni 2018.

Akiwa Mkoani Singida Mhe Dkt. Tizeba ametembelea vituo mbalimbali vya ukusanyaji wa pamba na kujionea msimu wa ununuzi wa pamba katika Wilaya ya Ikungi na Iramba.

Miongoni mwa mambo ya msisitizo katika maeneo yote hayo ni pamoja na kuwashauri wakulima kutouza pamba chafu kwa kudhani kuwa watapata kilo nyingi kwani jambo hilo linafifihisha soko la zao hilo kwa wanunuzi.

Katika hatua nyingine ametoa onyo kwa viongozi wa vyama vya ushirika AMKOS kutojihusisha na ubadhilifu wa fedha za wakulima huku akielekeza kukamatwa na kufikishwa mahakamani kwa wale wote waliobainika kuiba fedha za wakulima katika maeneo mbalimbali nchini.

Aidha, ametangaza neema kwa wakulima wa pamba kote nchini kuwa msimu ujao wa kilimo wa mwaka 2018/2019 wakulima watapatiwa mbegu na dawa bure pasina malipo.

Akiwa katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Tizeba amewasisitiza watendaji wote mkoani humo kutoa ushirikiano mahususi kwa wakulima ili kuongeza tija katika uzalishaji wa zao la pamba na mazao mengine yakiwemo mahindi, mtama, alizeti N.k

Zao la pamba ni miongoni mwa mazao ya biashara yanayolimwa katika mkoa wa Singida, Katika msimu huu wa mwaka 2017/2018, mkoa ulipokea mbegu bora za pamba aina ya UKM 08 tani 381.48 na kusambazwa kwa wakulima ambapo jumla ya ekari 35,889 zilipandwa. 

Aidha, sumu chupa 137,970 zimesambazwa kwa wakulima na mabomba ya kunyunyizia sumu 365 yamesambazwa pia.

Pia amesisitiza kuwa uongozi wa mkoa huo unapaswa kujipanga kikamilifu kusimamia ununuzi wa pamba kupitia utaratibu uliowekwa wa kuvitumia Vyama vya Ushirika vya Kilimo na Masoko (AMCOS) pamoja Vyama vya Awali vya Ushirika  (Pre Cooperative Societies).

Katika mkoa huo jumla ya AMCOS 36 na “Pre Cooperatives” 20 zitahusika katika ununuzi wa zao la pamba katika msimu huu wa kilimo wa mwaka 2017/2018.

Akizungumza katika mkutano huo Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Dkt Rehema Nchimbi alisema kuwa mkoa huo ulikuwa na matarajio ya awali ya mavuno kwa tani 21,533.4 ambapo matarajio haya yameshuka mpaka kufikia tani 14,015.2 zinazotarajiwa kuvunwa kutokana na athari za wadudu waharibifu.

Alisema jumla ya vituo vitakavyotumika kukusanya na kununua pamba ni 117 ambavyo vimesambaa katika maeneo yote yanayolima pamba yaliyopo katika Halmashauri saba za Mkoa huo.

Aliongeza kuwa maghala yatakayotumika kununulia pamba katika vituo hivyo  yamesafishwa na kufukiziwa sumu ya kuuwa wadudu. Kampuni iliyoruhusiwa kununua pamba katika Mkoa huo ni BioSustain (T) LTD ambayo ni mdau mkubwa wa kilimo cha zao la pamba katika mkoa wa Singida kwani imewekeza kiwanda cha kuchambua pamba kilichopo Manispaa ya Singida.

SPIKA NDUGAI MGENI RASMI MASHINDANO YA KUHIFADHI QURAN YALIYOFANYIKA PAHI WILAYANI KONDOA MKOANI DODOMA

Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai akizungumza na waumini wa dini ya kiislamu baada ya kumalizika kwa mashindano ya kuhifadhi Quran yaliyofanyika jana katika kijiji cha Pahi kilichopo Wilayani Kondoa Mkoani Dodoma. Spika alikuwa Mgeni rasmi katika mashindasno hayo. wa pili kulia ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi, Mhe. Mwigulu Nchemba, Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Mhe. Simon Odunga (kulia) na Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mustafa Shaban (wa tatu kulia).(Picha zote na Ofisi ya BUNGE)Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai akizungumza na waumini wa dini ya kiislamu baada ya kumalizika kwa mashindano ya kuhifadhi Quran yaliyofanyika jana katika kijiji cha Pahi kilichopo Wilayani Kondoa Mkoani Dodoma. Spika alikuwa Mgeni rasmi katika mashindano ya usomaji Quran yaliyofanyika jana kijijini hapo, kutoka kulia ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi, Mhe. Mwigulu Nchemba anaefuata ni Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mustafa Shaban. Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai akizungumza na waumini wa dini ya Kiislamu baada ya kumalizika kwa mashindano ya kuhifadhi Quran yaliyofanyika jana katika kijiji cha Pahi kilichopo Wilayani Kondoa Mkoani Dodoma. Spika alikuwa Mgeni rasmi katika mashindano ya usomaji Quran yaliyofanyika jana kijijini hapo, kulia ni Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mustafa Shaban. Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai akimpatia zawadi kati ya washindi wa mashindano ya Quran yaliyofanyika jana katika Kijiji cha Pahi kilichopo Wilayani kondoa Jijini Dodoma. Kulia ni Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mustafa Shaban, Spika alikuwa Mgeni rasmi katika mashindano ya usomaji Quran yaliyoandaliwa na Mbunge wa Viti Maluum kutoka Kondoa na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji. Spika wa Bunge, Mhe, Job Ndugai (kushoto) akikabidhiwa mifuko mia tatu (300) ya simenti kutoka kwa Meneja wa Shirika la Bima la Taifa (NIC) Tawi la Dodoma, Ndg. Halima Makange katika tukio lililofanyika jana katika Kijiji cha Pahi kilichopo Wilayani Kondoa Jijini Dodoma. Mifuko hiyo imetolewa kwa ajili ya maendeleo ya elimu kijijini hapo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Shule na zahanati. Katikati ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi, Mhe. Mwigulu Nchemba, wa pili kushoto ni Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu kijaji, Mbunge wa Mtwara Vijijini, Mhe. Hawa Ghasia (kushoto), Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mustafa Shaban na Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Ndg. Simon Odunga aliemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dodoma. Spika wa Bunge, Mhe. Job ndugai akizungumza na waumini wa dini ya kiislam na wakazi wa kijiji cha Pahi (hawapo kwenye picha) kilichopo Wilayani Kondoa Mkoani Dodoma. Baada ya kufuturu futari iliyoandaliwa na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu kijaji. Wa pili kushoto ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi, Mhe. Mwigulu Nchemba na kulia ni Sheikh Mkuu wa Mkoa  wa Dodoma, Mustafa Shaban.
Na Benny Mwaipaja, Kondoa
SPIKA wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai, amewataka watanzania kuwa na uvumilivu wa masuala ya kidini ili nchi iendelee kuwa na amani, utulivu na maendeleo.
Ndugai ametoa wito huo katika Kata ya Pahi wilayani Kondoa mkoani Dodoma, alipokuwa akizungumza wakati wa mashindano ya kuhifadhi Qur'an yaliyowashirikisha zaidi ya watoto na vijana 40 kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.
Spika Ndugai ameeleza kuwa umoja na mshikamano uliopo hapa nchini ni matokeo ya viongozi wa dini mbalimbali hapa nchini kuendelea kuhubiri amani na utulivu na kuitaka jamii na viongozi hao kuiendeleza kazi hiyo.
Kwa upande wake Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameitaka jamii kuendelea kupiga vita uhalifu na kuwafichua wahalifu popote walipo ili nchi iendelee kuwa na amani.
Mratibu na Mwandaaji wa mashindano hayo, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kondoa, Dkt. Ashatu Kijaji, amesema kuwa lengo la mashindano hayo ya kuhifadhi Qur'an Tukufu ni kuwajengea vijana maadili mema ili waweze kushiriki kikamilifu kuleta maendeleo ya taifa.
Naye Mgeni Rasmi katika Mashindano hayo, Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mustapher Shabaan amewapongeza vijana walioshiriki mashindano hayo na kuonesha umahili mkubwa wa kuhifadhi qoran na kuwataka waumini wa kiislamu kusoma na kukielewa kitabu hicho kitukufu kwa kuwa kimejaa elimu na maarifa mengi yatakayo wasaidia kuenenda vyema katika jamii na kupata thawabu kutoka kwa Mungu.

BALOZI SEIF IDDI AKAGUA MAENDELEO YA UJENZI WA MTARO WA KIJIJI CHA BUBUJIKO WETE KISIWANI PEMBA KUZUIA MAFURIKO

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akisalimiana na wananchi wa Kijiji cha Bubujiko alipofika kukagua Maendeleo ya Mtaro waliojenga kwa nguvu zao ili kuepuka athari za mafuriko hasa wakati wa mvua za Masika.(Picha zote na Hassan Issa – OMPR – ZNZ)Mhandisi wa Ujenzi wa Mtaro wa Kijiji cha Bubujiko Bwana Bwana Mohamed Abdullah kutoka Wizara ya Kilimo, Mali Asili, Uvuvi na Mifugo Pemba akimuonyesha Ramani ya Mtaro huo Balozi Seif na Ujumbe wake wakiwa mbele ya Karo inayoingiza maji hayo.Balozi Seif akiwapongeza Wananchi wa Kijiji cha Bubujiko kwa hatua waliyochukuwa ya ujenzi wa Mtaro utakaonusuru na majanga ya mafuriko ya mavua.Baadhi ya Wananchi wa Kijiji cha Bubujiko wakisikiliza Balozi Seif hayupo pichani wakati alipokuwa akizungumza nao kwenye Mtaa wa Kijiji hicho kiliopo pembezoni mwa Mji wa Wete.Mkaazi Muathirika nambari moja wa majanga yaliyokuwa yakitokea kwenye Kijiji hicho wakati wa Mvua za Masika Maalim Omar Hamad kwa niaba ya Wananchi wenzake akiishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa jitihada inazochukuwa za kuwahudumia Wananchi wake.Wawakilishi wa Wananchi wa Mikoa Miwili ya Kusini na Kaskazini Pemba wakitekeleza Ibada ya Sala ya Magharibi  katika Kiwanda cha Makonyo Wawi kabla ya futari ya pamoja na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif.Mkuu wa Mkoa Kusini Pemba Mh. Hemed Suyleiman Abdullah akitoa neon la shukrani kwa niaba ya Balozi Seif  baada ya futari ya pamoja iliyowakutanisha Wawakilishi wa Wananchi wa Mikoa Miwili ya Kusini na Kaskazini Pemba pamoja na Balozi Seif.

Na Othman Khamis Ame, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
10/6/2018.
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imekusudia kuwapunguzia gharama za ujenzi wa Mtaro wa Maji ya Mvua Wananchi wa Kijiji cha Bubujiko waliojitolea kuanzisha Mradi huo kwa lengo la kujiepusha na Mafuriko yanayosababishwa na mkusanyiko wa maji mengi yanayoleta maafa wakati wa mvua za Masika.
Kauli hiyo imetolewa na Makamuwa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akizungumza na Wananchi wa Bubujiko mara baada ya ziara fupi ya kukagua hatua za ujenzi wa Mtaro huo uliosimamiwa na Wananchi wenyewe na kuungwa mkono na Uongozi wa Mkoa na Wilaya pamoja na washirika wa maendeleo.
Balozi Seif Ali Iddi alisema  kitendo cha Wananchi wa Bubujiko kujenga Mtaro huo kimekuja mara baada ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohamed Shein kutoa kauli ya Serikali ya ujenzi wa Mtaro huo ambacho kinapaswa kupongezwa.
Alisema Serikali Kuu itaangalia namna ya kusaidia hatua iliyobaki ya kukamilika kwa ujenzi wa Mtaro huo uliobakia Mita 65 zinazotarajiwa kugharimu jumla ya shilingi Milioni 30,000,000/- ambapo hadi kukamilika kwake unatarajiwa kufikia Milioni 50,000,000/-.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alieleza kwamba Umoja na Mshikamano waliyouonyesha Wananchi wa Kijiji cha Bubujiko ndio chanzo cha mafanikio hayo yanayopaswa kuigwa na Wananchi wa Vijiji vyengine hapa Nchini.
“ Nafarajika kuona Mtaa wa Bubujiko kwa sasa utabakia katika Historia ya kuepuka na Mafuriko yaliyokuwa yakileta simanzi na hasara kubwa kwa Wakaazi wake”. Alisema Balozi Seif.
Mapema Msimamizi ambae pia ni Mhandisi wa Ujenzi wa Mtaro huo Bwana Mohamed Abdullah kutoka Wizara ya Kilimo, Mali Asili, Uvuvi na Mifugo Pemba alisema Mtaro huo umekisiwa kuwa na urefu wa Mita  Mia 200 ambapo kwa hatua ya awamu ya kwanza umeshafikisha Mita 165.
Mhandisi Mohamed alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba Mtaro huo uliojengwa kwa kianzio cha Mita Moja na Nusu hadi Mita Nnne unayawezesha Maji ya Mvua kusafiri kwa haraka bila ya athari yoyote huku mchanga na taka taka zinazotembea katika Mtaro huo hutolewa katika mapokeo maalum yaliyotengwa katika Ujenzi huo.
Alisema juhudi za ziada zilizofanywa na Wananchi katika kuondokana na hatari ya mafuriko ya mara kwa mara ya maji ya Mvua zimewezesha Mtaro huo kujengwa ndani ya kipindi cha Mwezi Mmoja na Nusu.
Akitoa Taarifa ya Ujenzi wa Mtaro huo wa Kijiji cha Bubujiko Mkuu wa Wilaya ya Wete Nd. Abeid Juma Ali alisema Utekelezaji wa Mradi huo umefanywa na Wataalamu Wazalendo.
Nd. Abeid alisema uzoefu unaonyesha kwamba Mtaro kama huo ungeamuliwa kujengwa na Wataalamu wa Kigeni ungekadiriwa kugharimu zaidi ya shilingi za Kitanzania Milioni 200,000,000/-.
Mkuu huyo wa Wilaya ya Wete alifahamisha kwamba Mvua kubwa za Masika zilizomalizika hivi karibuni hazikuleta athari yoyote kwa Wakaazi wa Kijiji hicho kilichopo pembezoni mwa Mji wa Wete baada ya kuanza kazi kwa Mtaro huo.
Akitoa shukrani kwa niaba ya Wananchi wa Kijiji cha Bubujiko Mkaazi Muathirika nambari moja wa majanga yaliyokuwa yakitokea kwenye Kijiji hicho wakati wa Mvua za Masika Maalim Omar Hamad kwa niaba ya Wananchi wenzake wameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa jitihada inazochukuwa za kuwahudumia Wananchi wake.
Maalim Omar alisema jitihada za Rais wa Zanzibar Dr. Ali Mohamed Shein na Msaidizi wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar wamekuwa wakizishuhudia na kuzifuatilia kiasi cha kuleta faraja kwa Wananchi wote wa Visiwa vya Unguja na Pemba.
Alisema Wananchi wa Bubujiko wameahidi kuendelea kuunga mkono jitihada hizo za Serikali katika kuona ustawi wa Wananchi wa Zanzibar unazidi kuimarika na kukua kila siku.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amemaliza ziara yake ya siku Tatu Kisiwani Pemba ambapo pamoja na mambo mengine alipata wasaa wa kufutari pamoja na Wawakilishi wa Wananchi wa Mikoa Miwili ya Kusini na Kaskazini Pemba.
Futari hiyo iliyohudhuriwa pia na baadhi ya Viongozi wengine wa Serikali na Vyama vya Kisiasa ilifanyika katika Ukumbi wa Makonyo uliopo Wawi Chake Chake Kisiwani Pemba.
Akitoa shukrani kwa niaba ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif, Mkuu wa Mkoa Kusini Pemba Mh. Hemed Suleiman Abdullah aliwaomba Waumini wa Dini ya Kiislamu wazidishe  Ibada hasa katika Kumi hili la Mwisho la Mwezi Mtukufu wa Ramadhan ili kupata baraka za Mwenyezi Muungu.
Alisema hayo yatapatikana na kulifanya Taifa liwe na baraka zaidi iwapo Waumini wenyewe wataendeleza Utamaduni wao wa kudumisha Umoja na Mshikamano kama Maamrisho ya Dini yenyewe yanavyoagiza.
Alisema Taifa linahitaji zaidi Mshikamano na upendo miongoni mwa Wananchi wake bila ya kujali itikadi za Kisiasa na Kidini ili faida ya Wanaadamu kuishi ndani ya Ardhi hii iweze kupatikana.

WAZIRI DKT TIZEBA AAGIZA KUKAMATWA KIONGOZI WA AMKOS ALIYEFUJA MILIONI 23

Waziri wa Kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akisisitiza jambo wakati akizungumza na wakulima wa pamba katika kijiji cha Msai wilaya ya Iramba  akiwa katika ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani Singida kutembelea vituo na kujionea ununuzi wa pamba. (Picha Zote Na Mathias Canal, WK)
Waziri wa Kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akisisitiza jambo wakati akizungumza na wakulima wa pamba katika kijiji cha Msai wilaya ya Iramba  akiwa katika ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani Singida kutembelea vituo na kujionea ununuzi wa pamba, Kulia kwake ni Mkuu wa Wilaya ya Iramba Mhe Emmanuely Lwehahula.
Kituo cha ukusanyaji na ununuzi wa pamba katika kijiji na Kata ya Msai, Wilayani Iramba.

Mkuu wa Wilaya ya Iramba Mhe Emmanuely Lwehahula akitoa salamu za shukrani kwa Waziri wa Kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba kwa kufanya ziara ya kuwatembelea  wakulima wa pamba katika kijiji cha Msai wilaya ya Iramba akiwa katika ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani Singida kutembelea vituo na kujionea ununuzi wa pamba, 

Na Mathias Canal-WK, Singida
WAZIRI wa Kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba amemuagiza Mrakibu wa polisi Wilaya ya Iramba ASP Magoma Mtani kumkamata aliyekuwa mwenyekiti wa Bodi ya Chama cha ushirika (AMKOS) Msai.

Waziri Tizeba ametoa agizo hilo jana 9 June 2018 Mara baada ya kutembelea kitongoji cha Kati, Msai na Mtoa akiwa katika ziara ya kikazi ya Siku mbili kwa ajili ya kutembelea vituo vya ununuzi wa pamba na kujionea msimu wa ununuzi wa zao hilo katika vijiji hivyo.

Dkt Tizeba amelaani vikali ufujaji huo wa fedha za wakulima huku akimtaja Paul Ramadhan Kurwa kuhusika na ufujaji huo wa shilingi milioni 23 huku akiendelea kuonekana mtaani pasina kuchukuliwa hatua za kisheria.

"Wakati muelekeo wa serikali yetu inayoongozwa na Rais wetu Dkt John Pombe Magufuli ukijipambanua kutaka kuboresha maisha ya watanzania kupitia Kilimo lakini kuna watu wanataka kurudisha nyuma juhudi hizo, hakika tutawapa kibano kweli kweli hakuna utani kwenye fedha za wananchi" Alikaririwa Dkt Tizeba

Mhe Tizeba ametoa siku moja kukamatwa kwa mwizi huyo na kufikishwa mahakamani ili awe mfano kwa wezi wengine wasio kuwa na haya wala soni.

Aidha, amewataka wananchi katika msimu huu wa uuzaji na ununuzi wa Pamba kutouza Pamba zenye uchafu wakidhani wataongeza idadi ya kilo kwani kufanya hivyo ni kufifihisha juhudi zao wenyewe jambo ambalo halina tija.

Sambamba na hayo pia amewaondoa hofu wakulima kote nchini kuwa serikali ya awamu ya tano inatekeleza kwa vitendo ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi yenye mkataba na wananchi katika kipindi cha miaka mitano 2015-2020.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Iramba Mhe Emmanuely Lwehahula amempongeza Waziri Tizeba kwa kutembelea maeneo mbalimbali ili kujionea ununuzi wa Pamba huku akiwasihi wananchi wilayani humo kulima kiasi kikubwa cha Pamba msimu ujao kwani mbegu na madawa ya kuulia wadudu vitatolewa bure kuanzia msimu ujao wa mwaka 2018/2019.