TANGAZO


Monday, October 13, 2014

Wauguzi waombwa wasigome Liberia

Zaidi ya watu 4,000 wamefariki kutokana na Ebola katika kanda ya Afrika Magharibi
Maafisa wa afya nchini Liberia, wanawaomba wauguzi na wasaidizi wao kusitisha mpango wao wa mgomo wa kitaifa huku mlipuko wa Ebola ukiendelea kukithiri nchini humo.
Chama cha kitaifa cha wafanyakazi wa afya, kinataka serikali iwaongeze marupurupu kwa kuhatarisha maisha yao hasa kwa wale wanaowatibu wagonjwa wa Ebola.
Rais wa Marekani Barack Obama, ameamuru hatua zaidi kuchukuliwa za kuhakikisha wauguzi hawapatwi na ugonjwa huo.
Muuguzi mmoja ambaye alikuwa anamtibu mgonjwa wa Ebola yeye mwenyewe aliambukizwa ugonjwa huo.
Naibu waziri wa afya wa Liberia , Tolbert Nyenswah alisema ikiwa mgomo utafanyika sasa hivi utakuwa na athari kubwa kwa walioathirika na pia kuathiri hatua zilizofikiwa hadi sasa katika vita dhidi ya ugonjwa huo.
Serikali inasema kuwa janga la Ebola ni kubwa na ina maana kuwa serikali haiwezi kutimiza ahadi ya kuwalipa pesa zaidi wafanyakazi hao kwa kuhatarisha maisha yao.
Kiwango wanacho lipwa ni dola 500 kila mwezi , pamoja na mshahara wao wa kati ya dola 200 na 300.
Wauguzi hao sasa wanataka kulipwa dola 700 kama marupurupu ya kuhatarisha maisha yao wakiwatibu wagonjwa wa Ebola.
Wafanyakazi hao wa afya, pia wanataka vifaa vya kuwalinda kutokana na maambukizi pamoja na kupewa bima ya afya na serikali.
Wauguzi wengine 95 wamefariki kutokana na Ebola nchini humo.
Liberia ni moja ya nchi zilizoathirika vibaya sana na Ebola.
Zaidi ya watu 4,000 wamefariki kutokana na ugonjwa huo tangu ulipoanza kuwa kero hasa kwa mataifa ya Afrika Magharibi.

No comments:

Post a Comment