TANGAZO


Wednesday, October 30, 2013

Dk Shein aongoza kumuaga, mazishi ya Balozi Sepetu Kijiji kwao, Mbuzini, Wilaya Magharibi Unguja


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, akimpa pole mjane wa marehemu Balozi Isaac Sepetu, Mama Miriam Sepetu, alipofika katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani, Mnazi mmoja Mjini Unguja, kuuaga mwili wa marehemu leo asubuhi. (Picha na Ramadhan Othman Ikulu)
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, akitia saini kitabu cha maombolezo ya marehemu Balozi Isaac Sepetu, katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani, Mnazi Mmoja, Mjini Unguja leo asubuhi. Marehemu Balozi Sepetu alifariki juzi, jijini Dar es Salaam na kuzikwa Kijiji kwao, Mbuzini, Wilaya Magharibi.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, akiuaga mwili wa marehemu Balozi Isaac Sepentu, katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani, Mnazi Mmoja Mjini Unguja leo asubuhi. Marehemu alifariki juzi jijini Dar es Salaam na atazikwa Kijiji kwao, Mbuzini Wilaya Magharibi.
Baadhi ya wananchi mbalimbali wakiwa katika sehemu maalum nje ya ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani, Mnazi Mmoja Mjini Unguja leo, wakisubiri kuuaga mwili wa marehemu Balozi Isaac Sepetu, ambao utazikwa Kijiji kwao, Mbuzini Wilaya Magharibi.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, akisalimiana na Padri wa Kanisa Katoliki la Minara miwili, Mjini Zanzibar, Cosmas Amani Shayo,  alipowasili katika eneo la mazishi ya marehemu Balozi Issac Abraham  Sepetu, yaliyofanyika kijijini kwao, Mbuzini Wilaya ya  Magharibi Unguja leo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, akiwa na viongozi wengine akiwemo Makamo  wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohamed Gharib  Bilali katika mazishi ya marehemu Balozi Issac Abraham Sepetu, yaliyofanyika kijijini kwao, Mbuzini Wilaya ya Magharibi Unguja leo.
Jeneza lenye mwili wa marehemu Balozi Issac Abraham Sepetu, likiwa limebebwa na Askari Polisi na kulifikisha katika kaburi lake yalipofanyika mazishi kijijini kwao, Mbuzini Wilaya ya  Magharibi Unguja leo.
Padri wa Kanisa Katoliki la  Minara miwili Mjini Zanzibar, Cosmas Amani Shayo, akiuombea mwili wa marehemu Balozi  Issac Abraham Sepetu, wakati wa mazishi yake, yaliyofanyika kijijini kwao, Mbuzini Wilaya ya  Magharibi Unguja leo.
Jeneza lenye mwili wa marehemu Balozi Issac Abraham Sepetu, ukiteremshwa katika kaburi wakati wa mazishi yake yaliyofanyika kijijini kwao Mbuzini Wilaya ya  Magharibi Unguja leo.

Na mwandishi wetu
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein leo amewaongoza viongozi na mamia ya wananchi wa Zanzibar katika mazishi ya mwanasiasa na mwanadiplomasia mkongwe Balozi Issac Abraham Sepetu yaliyofanyika huko kijijini kwake Mbuzini, Wilaya ya Magharibi Mkoa wa Mjini Magharibi unguja.
Serikali katika salamu zake zilitolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Mohamed Aboud Mohamed imesema kuwa Marehemu Balozi Sepetu atabaki katika nyoyo za wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa jumla kutokana na mchango wake katika kulitumikia Taifa.

Waziri Aboud alimuelezea Balozi Sepetu ambaye katika uhai wake alishika nafasi mbali mbali katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuwa mtu aliyeitumika nchi yake kwa uadilifu na uaminifu mkubwa hivyo msiba huo si wa familia tu bali kwa wananchi wote wa Zanzibar na Tanzania.
Alisema Serikali na wananchi wa Zanzibar wamepokea kwa masikitiko makubwa msiba wa hayati Balozi Sepetu na kuwaomba wanafamilia kuwa na moyo wa subira katika kipindi hiki kigumu cha maombolezi.
Akitoa salamu za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mazishi hayo  Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Benard Membe alisema Rais Jakaya Mrisho wa Kikwete ameguswa sana na kifo cha Balozi Sepetu ambaye aliwahi kufanya nae kazi katika Wizara ya Mambo ya Nje kwa miaka kumi.
Alisema kifo chake ni pigo kwa taifa na daima watanzania watamkumbuka sana Balozi Sepetu na kubaki katika nyoyo zao kutokana na utumishi wake bora kwa taifa.

Akisoma wasifu wa Balozi Sepetu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitega Uchumi-ZIPA nchini Khamis Salum alieleza kuwa maraeehmu Balozi Sepetu alizaliwa tarehe 16 Oktoba, 1943 huko Tabora alipata elimu yake ya msingi na sekondari katika skuli ya Mtakatifu Joseph mjini Unguja ambayo sasa inaitwa Tumekuja.
Mwaka 1966 alikwenda iliyokuwa Ujerumani Mashariki kwa masomo hadi mwaka 1970 ambapo alihitimu shahada ya pili katika Uchumi na sayansi ya siasa. Aliporejea nyumbani aliteuliwa kushika nafasi ya Meneja Msaidizi Mkuu wa Shirika la Shirika la Biashara Zanzibar BIZANJE.
Kabla ya kwenda masomoni nchini Ujerumani marehemu alifanyakazi katika Idara ya Habari na Utangazaji Zanzibar na aliwahi kuwa Mhariri Msaidizi wa Gazeti la Kweupe ambalo llianzishwa na Rais wa kwanza wa Zanzibar Marehemu Abeid Amani Karume.  

Balozi wa Sepetu aliwahi kushika nyadhifa za Naibu wa Waziri wa Mambo ya Nje, Waziri wa Habari na Utalii katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi wa Tanzania katika Shirikisho la nchi za Kisoshalisti la Kisovieti wakati huo na Jamhuri ya Kidemkrasia ya Kongo wakati huo ikiitwa Zaire.
Katika Serikali ya Zanzibar aliwahi kuwa Kamishna wa Tume ya Mipango, Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Mipango.Mwaka 2000 alichaguliwa mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki hadi mwaka 2005. Hadi anaaga dunia Balozi Sepetu alikuwa Mwenyekiti wa Bodi ya ZIPA.
Marehemu Balozi Sepetu ameacha wajane wawili, watoto na wajukuu.  
Mazishi hayo yalihudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad na Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Iddi pamoja na wageni mbalibali kutoka Tanzania bara. 
wakati huo huo mamia ya wakaazi wa mji wa Zanzibar walitoa heshma zao za mwisho kwa mwili wa marehemu Balozi Issac Abraham Sepetu mapema asubuhi huko katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi uliopo mjini Unguja.
 Mwili wa marehemu uliwasili kwa boti mapema asubuhi ukitokea Dar es Salaam ambako Balozi Sepetu mauti yalimkuta.
Baadae mwili ulipelekwa katika Kanisa la Roma la Minara Miwili lililopo Shangani mjini hapa kwa misa.

No comments:

Post a Comment