TANGAZO


Wednesday, July 17, 2013

Wizara ya Maliasili na Utalii yazungumzia majukumu ya wizara hiyo pia umuhimu wa wananchi kushiriki katika kulinda na kuzuia ujangili wa rasilimali za Taifa

Ofisa Habari wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini  kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Yustina Mallya (kushoto), akizungumza na vyombo vya habari kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa wanyama pori na faida za ushirikishwaji wa wananchi katika kuzuia ujangili, kwenye mkutano uliofanyika ukumbi wa Idara ya Habari leo,  jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari, Zamaradi Kawawa.
Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori  kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Profesa Alexander Songorwa akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari juu ya umuhimu wa uhifadhi wa wanyama pori na faida za ushirikishwaji wa wananchi katika kuzuia ujangili. Kulia ni Ofisa Habari wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini  kutoka Wizara hiyo, Yustina Mallya. 

Kaimu Mkurugenzi Kitengo cha Kuzuia Ujangili kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, John Muya, akifafanua jambo kwa waandishi wa habari kuhusu faida za ushirikishwaji wa wananchi katika kuzuia ujangili, kwenye mkutano uliofanyika ukumbi wa Idara ya Habari leo,  jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari, Zamaradi Kawawa. (Picha zote na Hassan Silayo-MAELEZO)


MCHANGO WA UHIFADHI KATIKA KUKUZA UCHUMI WA NCHI NA UMUHIMU WA WANANCHI KUSHIRIKI KATIKA KUZUIA UJANGILI. 
Wizara ya Maliasili na Utalii inawajulisha wananchi kuwa ingawaje kumekuwa na taarifa za kuongezeka kwa ujangili nchini na hasa mauaji ya kinyama ya tembo na usafirishaji haramu wa wanyamaporihai na meno ya tembo, Wizara inajitahidi kupambana na uhalifu huu kulingana na rasilimali watu na fedha zilizopo. Kwa mfano, mwaka 2012/13 pekee (kufikia Machi 2013) watuhumiwa 1,215 walikamatwa kwa makosa mbalimbali wakiwa na jumla ya bunduki 85 na risasi 215 za aina mbalimbali.

Kesi 670 zilifunguliwa katika mahakama mbalimbali nchini. Kati ya hizo, kesi 272 zimemalizika kwa washitakiwa 247 kulipa faini ya jumla ya shilingi 175,002,420/= na washitakiwa 71 kupewa adhabu ya vifungo vya jumla ya miaka 99. Aidha, kesi 398 zenye jumla ya washitakiwa 897 bado zinaendelea katika mahakama mbalimbali nchini.

Vita dhidi ya ujangili ni ngumu hasa ukizingatia kuwa, baadhi ya Watanzania wanaamini kuwa jukumu hili ni la serikali pekee na hasa maafisa na askari wanyamapori. Dhana hii ni potofu kwani, uzuiaji ujangili kamwe hautafanikiwa kama wananchi na wadau wengine walioko ndani na nje ya nchi yetu wataendelea kubakia watazamaji tu.

Wizara inaomba sote tuitafakari na kuitekeleza dhana ya Jeshi la Polisi ya Ulinzi Shirikishi. Ni muhimu kila mwananchi mzalendo wa nchi hii ashiriki kikamilifu kudumisha amani na ulinzi wa nchi na rasilimali zake zote. Hivyo basi, wananchi wanaweza kutoa taarifa za kina na uhakika zitakazopelekea kukamatwa majangili na/au wafadhili wao.

Yeyote mwenye taarifa azitoe ama kwa Afisa Wanyamapori aliye karibu yake, Makao Makuu ya Idara ya Wanyamapori, TANAPA, Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro au Kituo cha Polisi kilichokaribu. Pia unaweza kupiga simu kwenye namba zilizoambatanishwa kwenye taarifa hii.

Aidha, ikumbukwe kuwa hapa nchini, zaidi ya asilimia 90 utalii unategemea wanyamapori. Watalii wengi huja kuwaona, kuwapiga picha na kuondoka. Wachache huja kuwawinda kisheria na kuchukua nyara. Wanyamapori ndio wamebeba utalii katika Tanzania na kwa maana hiyo ndio, kwa kiasi kikubwa, wamebeba uchumi wa nchi hii – ndio wanatununulia dawa, vitabu mashuleni na kutujengea barabara.

Wizara inatoa wito kwa Watanzania kuwa tuache kumtazama fisi kama mnyama mwenye sura mbaya na anayenuka; na tuache kumtazama tembo kama kero kwa wakulima na kwa hiyo kufurahia kuuawa kwao. Badala yake tuwatazame wanyamapori kama benki kubwa na kama mkombozi wa nchi yetu kiuchumi.

Wanyamapori kama ilivyo viumbe hai, huzaliana. Hivyo, kama tutashirikiana kuwalinda na kuwatumia kiendelevu si miaka mingi tangu sasa watakuwa namba moja katika kuchangia pato la Taifa letu.
 WIZARA YA MALIASILI NA UTALII
17 Julai 2013 
Namba za simu: 0754877019; 0787491600; 0713350405; 0784483599; 0754756585 Barua pepe: dw@mnrt.go.tz au ps@mnrt.go.tz


No comments:

Post a Comment