TANGAZO


Thursday, March 24, 2016

Mfuko wa wazee wanukia

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy mwalimu akizungumza na viongozi na baadhi ya wazee wa mkoa wa Dar es Salaam katikati ni Mwenyekiti wawazee hao Mzee hemed Mkali na kulia ni Katibu wa wazee hao Mzee Mohamed Mtulia.

Na Raymond Mushumbusi MAELEZO
Dar es Salaam
23/03/2016
SERIKALI imeazimia kuanzisha Mfuko wa Wazee utakaowasaidia kupambana na changamoto zinazowakabili kwa kuwawezesha kiuchumi.

Akitoa azimio hilo mbele ya viongozi na baadhi ya wazee wa mkoa wa Dar es Salaam,Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu alisema Wizara imeazimia kuanzisha mfuko huo utakaowasaidia wazee nchini ili waweze kujikwamua kiuchumi.

“Wazee bado wanaweza kuchangia katika maendeleo ya taifa kama watashirikishwa katika kuendesha sekta mbalimbali kwani bado tunahitaji ujuzi na mchango wao katika kusongesha mbele gurudumu la maendeleo ya nchi yetu” alisema Mhe. Ummy.

Waziri Ummy ameongeza kuwa mfuko huo utawasaidia wazee kupata na kuongeza kipato chao kwa kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi ambazo zitawasaidia kupata huduma bora za afya.

“Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuwasaidia wazee, nimeshapeleka mapendekezo kwa kila halmashauri kuanzisha mfuko wa wazee utakaowasaidia kujikwamua kiuchumi katika maeneo yao” alisema Mhe. Ummy.

Naye Mwenyekiti wa wazee hao Mzee Hemed Mkali amesema wanahitaji sana mfuko huo ambao utawawezesha kujishughulisha na kupata kipato na pia kuboresha huduma za afya ambazo bado ni changamoto kwa wazee nchini.

Aidha, Waziri Ummy alisistiza kuwa wanashirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango ili kuandaa mpango wa kuanzisha mfuko huo kwa kushirikisha taasisi za kifedha, makampuni na mashirika mbalimbali katika kuchangia maendeleo ya mfuko huo kwa maendeleo ya wazee na jamii kwa ujumla.

Wazee nchini wanakabiliwa na changamoto nyingi zikiwemo upatikanaji wa huduma za afya na ushirikishwaji wao katika shughuli mbalimbali za kiuchumi na kutoa maamuzi katika jamii zao ambao idadi yao inakadiriwa kuwa ni asilimia 5.6 ya watanzania wote.

No comments:

Post a Comment