TANGAZO


Sunday, July 12, 2015

Serikali ya Zanzibar yaidhinisha miradi ya Kiuchumi ya uwekezaji 153, ya mtaji wa dola bilioni 1.493,139,968

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi  akitoa Taarifa ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Utekelezaji wa wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kipindi cha miaka mitano kuanzia Novemba mwaka 2010 hadi Julai 2015 kwenye Mkutano Mkuu wa CCM wa siku mbili uliofanyika katika Ukumbi wake Mpya uliopo Mjini Dodoma. 
Wagombea kuomba nafasi ya urais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Tiketi ya CCM waliongia kwenye mchakato ya tatu bora Balozi Amina Salum Ali Kulia na Dr. Ash Roze Migiro, wakipongezana kabla ya kutangazwa aliyefanikia kupeperusha Bendera ya chama hicho Dr. John Pombe Magufuli.
Dr. John Pombe Magufuli Mgombea nafasi ya Urais wa Serikali ya Muungano kwa tiketi ya CCM Kushoto na Mgombea mwenza wake Mh. Samia Suluhu Hassan wakipongezana mara baada ya kutangazwa Mh. Samia kwenye wadhifa huo. (Picha zote na Hassan Issa – OMPR – ZNZ)

Na Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
12/7/2015.

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imeidhinisha miradi ya Kiuchumi ya uwekezaji ipatayo 153, yenye Mtaji wa Dola za Kimarekani Bilioni Moja, Mia 493 Milioni, laki 139,968 katika azma yake ya kuongeza mapato na kusaidia kupunguza ukali wa maisha kwa Wananchi wake.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alitoa kauli hiyo wakati akitoa Taarifa ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Utekelezaji wa wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kipindi cha miaka mitano
kuanzia Novemba mwaka 2010 hadi Julai 2015 kwenye Mkutano Mkuu wa CCM wa siku mbili uliofanyika katika Ukumbi wake Mpya ulioo Mjini Dodoma.


Mkutano huo pamoja na Mambo mengine umepokea na kupitisha Ilani ya Uchaguzi ya Chama hicho ya mwaka 2015 hadi 2020 itakayonadiwa kwa
wananchi ili ipate ridhaa ya kuongoza  Dola katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika mwezi Oktoba Mwaka huu.


Balozi Seif alisema miradi hiyo ya uwekezaji 153 kati yake miradi 53 inamilikiwa na wawekezaji wazalendo ambao sekta ya Utalii ikiongoza kwa asilimia 52 ya miradi iliyoidhinishwa katika kipindi hichi.


Alisema uwekezaji huo wa miradi ya Kiuchumi unatarajia kutoa ajira zipatazo elfu 6,658 kwa wananchi wazalendo hali itakayosaidia kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira hasa kwa Vijana hapa Nchini.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ambae Pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM alisema Serikali imefanya tafiti tofauti katika kuibua maeneo mapya ya kuwekeza sambamba na utafiti wa mwenendo wa mitaji Binafsi ili kuona namna gani mitaji hiyo inatoa mchango katika kuimarisha uchumi wa Taifa.


Akizungumzia kuhusu suala la mikopo Balozi Seif alisema katika kipindi cha miaka mitano iliyopita Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetoa mikopo 1,603 yenye thamani ya shilingi Bilioni 1.45 katika shehia 305 za Unguja na Pemba.


Alisema Mikopo hiyo imeongeza ajira za moja kwa moja zipatazo 20,614 kwa makundi mbali mbali ya Jamii ambazo zimewahakikishia kufaidika na
upatikanaji wa ajira.


Balozi Seif alifahamisha kwamba mikopo hiyo iliyotolewa na Serikali imekwenda sambamba na ule mpango wake wa kuweka fedha za dhamana
shilingi Milioni 1,000,000,000/- kwenye Benki ya CRDB ili kuviwezesha vikundi vya Vijana kujipatia mikopo kutokana na dhamana hiyo.


Alieleza kwamba huduma za mikopo kwa wajasiri amali wadogo wadogo zimeimarishwa kwa kuunganisha mifuko iliyokuwepo zamani chini ya mfuko ulioanzishwa wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi.


Balozi Seif alifahamisha kuwa mfuko huo wa uwezeshaji wananchi Kiuchumi una lengo la kupanua fursa za mikopo nafuu kwa wajasiri amali hususan, wanawake, vijana na watu wenye kipato cha chini ili waweze kuanzisha na kuimarisha shughuli za kiuchumi zitakazowasaidia kujiajiri na kunyanyua kipato chao.


Kuhusu mafanikio ya Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM katika kipindi cha miaka mitano iliyopita Balozi Seif alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeongeza ukusanyaji wa Mapato kutoka vianzio
mbali mbali vilivyopo hapa Nchini.


Balozi Seif alisema Mapato ya Serikali yameonyesha kuongezeka  kutoka shilingi Bilioni 181 kwa mwaka 2010/2010 hadi kufikia shilingi Bilioni mia Mia Tatu na Thalathini kwa Mwaka 2013/2014.


Alisema makusanyo hayo hayo ya shilingi Bilioni  Mia 330 ni sawa na asilimia 94% ya makadirio yaliyokusudiwa kukusanywa ya  shilingi Bilioni Mia 338.45 katika kipindi hicho.


Alieleza kuwa ongezeko hilo la mapato ya ndani limetokana na juhudi tofauti zilizochukuliwa na Serikali zikiwemo kuziba miaya ya uvujaji wa mapato ya Taifa kwa kuyafanyia kazi mapendekezo  yaliyotolewa kupitia maabara ya upatikanaji  wa rasilmali fedha na mapitio ya Sekta ya Fedha.


Katika juhudi za kuendeleza ujenzi wa skuli mpya za sekondari Nchini Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Serikali imekamilisha ujenzi wa Skuli 19 Unguja na Pemba ambao
umefanya idadi ya skuli za Sekondari  kuongezeka na kufikia Skuli 263 mwaka 2015 kutoka skuli 194 mwaka 2010.


Balozi Seif alisema kukamilika kwa ujenzi wa skuli hizo  kumesaidia kupunguza msongamano wa wanafunzi kwa baadhi  ya skuli za sekondari kwa vile idadi ya wanafunzi katika ngazi ya sekondari kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne imeongezeka.


Alieleza kwamba katika kwenda sambamba na ongezeko hilo la idadi kubwa ya wanafunzi Wizara inayosimamia sekta ya Elimu imewapatia mafunzo
walimu Wakuu 350 juu ya miiko na maadili ya kazi za ualimu ili kuwajengea uwezo wa kumudu kazi zao.


Balozi Seif alisema mafunzo hayo yamekwenda sambamba na uimarishaji wa ufundishaji wa masomo ya sayansi ambapo jumla ya walimu 10 wamepatiwa
mfunzo nje ya Nchi na walimu 450 wa sekondari wamejengewa uwezo wa kitaaluma.


Alifahamisha kwamba hatua hizo zote zimelenga kuwajengea mazingira bora wanafunzi nchini kujikita katika kuwavutia kupenda kusoma masomo ya sayansi na hesabu yanayoonekana kuwa na idadi ndogo ya wanafunzi na hatimae huchangia kupunguza idadi ya wataalamu wa sayansi Nchini.


Hata hivyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema zipo changamoto zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM mwaka
2010 – 2015 ambazo zilichangia kupunguza kasi ya harakati za Maendeleo Nchini.


Balozi Seif alizitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na kutokea kwa vitendo vilivyoashiria kuvunjika kwa hali ya amani nchini, kutokea kwa maafa tofauti na kuleta usumbufu kwa jamii pamoja na mfumko wa bei za vyakula uliotokana na kupanda kwa bei ya mafuta na chakula katika soko la Dunia.


Alisema Serikali Kuu ililazimika kuchukuwa hatua za dharura kukabiliana na changamoto hizo na kufanikiwa kuzidhibiti hasa lile suala zima la udhibiti wa amani ya Taifa ambalo lilihitaji kuchukuliwa hatua za haraka.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewashukuru na kuwapongeza Wananchi, sekta binafsi asasi za Kiraia, Washirika wa Maendeleo na Nchi marafiki kwa ushirikiano na mahusiano yao yaliyoiwezesha Serikali
kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa.


Alisema kutokana na mashirikiano na mafanikio yaliyopatikana kati ya pande hizo mbili ni dhahiri kwamba Wananchi wameonyesha Imani  kwa Ilani ya Chama cha Mapinduzi na ni vyema wakaiunga mkono katika kipindi chengine cha miaka mitano ijayo.


Alisema uungaji mkono huo utachangia kuiwezesha Nchi kupiga hatua Zaidi ya maendeleo katika sekta ya kiuchumi,uz alishaji mali,huduma za Kijamii na sekta nyengine muhimu.

No comments:

Post a Comment