TANGAZO


Friday, February 27, 2015

Dkt. Fenella akutana na wasanii nchini

Waziri wa Habari, Vijana,Utamaduni na Michezo Dkt. Fenella Mukangara akimueleza jambo Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Dkt. Francis Michael wakati wa mkutano na wasanii uliofanyika katika ukumbi wa uwanja mpya wa Taifa leo Jijini Dar es Salaam. 
 Mkurugenzi Idara ya Utamaduni kutoka Wizara ya Habari, Vijana,Utamaduni na Michezo Prof. Herman Mwansoko akiongea na wasanii nchini na kuwaeleza kuhusu umuhimu wa sekta hiyo kushiriki kikamilifu katika masuala ya kitaifa hasa katika kipindi hiki cha kuelekea upatikanaji wa Katiba Mpya, Kulia ni Katibu wa Bodi ya Filamu Bi. Joyce Fisoo.
Waziri wa Habari, Vijana,Utamaduni na Michezo Dkt. Fenella Mukangara akiongea na wasanii nchini na kuwaasa wasanii kuielimisha na kuhamasisha Jamii kuhusu Katiba Inayopendekezwa kupitia kazi mbalimbali za sanaa, wakati wa mkutano na wasanii nchini uliofanyika leo Jijini Dar es Salaam. 
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Dkt. Francis Michael akiongea na wasanii nchini na kuwaeleza namna gani makundi mbalimbali yalivyoainishwa kwenye Katiba Inayopendekezwa ikiwemo haki za wasanii tofauti na Katiba ya Mwaka 1977. 
Waziri wa Habari, Vijana,Utamaduni na Michezo Dkt. Fenella Mukangara akiongea na baadhi ya wasanii mara baada ya kuisha kwa mkutano huo leo Jijini Dar es Salaam. 
Waziri wa Habari, Vijana,Utamaduni na Michezo Dkt. Fenella Mukangara akibadilishana mawazo na baadhi ya wasanii mara baada ya kuisha kwa mkutano huo leo Jijini Dar es Salaam. 
Waziri wa Habari, Vijana,Utamaduni na Michezo Dkt. Fenella Mukangara akiwasikiliza baadhi ya wasanii wakati wa mkutano huo. 
Waziri wa Habari, Vijana,Utamaduni na Michezo Dkt. Fenella Mukangara akiongea na wasanii nchini na kuwaasa wasanii kuielimisha na kuhamasisha Jamii kuhusu Katiba Inayopendekezwa kupitia kazi mbalimbali za sanaa, wakati wa mkutano na wasanii nchini uliofanyika leo Jijini Dar es Salaam.

Hotuba ya Waziri Fenella Mukangara kwa wasanii

Katibu Mkuu, Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo,
Viongozi wa Wasanii wa fani mbalimbali,
Wakurugenzi Wizara ya Habari , Vijana , Utamaduni na Michezo,
Mtoa Mada,
Waandishi wa Habari
Mabibi na Mabwana

Habari za Mchana,

Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kufika siku ya leo na kuuona mwaka 2015. Niwatakie wote heri ya mwaka mpya, uwe  wa baraka na mafanikio makubwa katika shughuli zenu za  kila siku.

Nichukue nafasi hii  kuwashukuru kwa kuitikia mwaliko wetu na kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Mkutano wa leo pamoja na majukumu mazito mlionayo.

Ndugu Wasanii,
Napenda kutoa pongezi za dhati kwa kazi kubwa mnayoifanya ya kueleimsha Jamii katika masuala mbalimbali. Aidha kazi zenu  zimekuwa ni chachu ya kuleta mabadiliko chanya katika Taifa letu na zimekuwa ni utambulisho wa Utaifa wetu nje ya Tanzania.  Nawapongeza wote mlioshinda tuzo mbalimbali za kitaifa na kimataifa mmekuwa mstari wa mbele kuitangaza nchi yetu nje ya mipaka yetu kupitia usanii.  Tunajivunia kazi zenu.

Ndugu Wasanii,
Niwahakikishie kuwa siku zote   tupo pamoja na nimekuwa nikifuatilia kazi zenu mbalimbali, katika Luninga, kusikiliza Nyimbo, kuona michoro mbalimbali, ubunifu katika mavazi na sanaa zinginezo. Kwa hakika ubora wa kazi zetu za Sanaa naushuhudia ukiongezeka siku hadi hadi siku.

Ndugu Wasanii,
Kama mnavyojua mwaka huu 2015, Taifa letu  linatarajia kuwa na matukio makubwa mawili, kura ya maoni ya Katiba Inayopendekezwa na Uchaguzi Mkuu. 

Serikali kwa kutambua umuhimu wenu, imeona ikutane na wadau wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kwa lengo la kuelimishana na kukumbushana kuhusu jukumu letu kama Wasanii katika  kuelimisha na kuhamasisha umma  katika masuala mbalimbali muhimu kwa taifa letu.

Katika Mkutano wa leo tutajikita zaidi katika kuelimishana juu ya wajibu wenu kama Wasanii katika kuielimisha Jamii kuhusu Katiba Inayopendekezwa  na kujadili  juu ya nafasi ya Sanaa/ Wasanii katika katiba inayopendekezwa, ikiwemo haki mbalimbali za Wasanii.

Ndugu Wasanii,
Taifa linatarajia kuendesha kura ya maoni tarehe 30 Aprili mwaka huu na ili zoezi hili lifanikiwe kwa kiasi kikubwa taaluma na nafasi yenu kama wasanii  inahitajika kutumika kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Ni ukweli usiopingika kuwa  ili wananchi waweze kufanya maamuzi sahihi  wakati utakapowadia  ni vyema wakapata  elimu  kupitia njia mbalimbali hususan kupitia sanaa juu ya katiba inayopendekezwa, bila kusahau makundi yenye mahitaji maalum.  Tunafahamu kwamba mna washabiki wengi ambao kupitia Sanaa mnaweza kuwaelimisha kuhusu mchakato wa upatikanaji wa Katiba Inayopendekezwa na umuhimu wa ushiriki wao katika kuunga mkono Katiba Inayopendekezwa.

Ndugu Waasanii
Tumeona ni vyema sisi kama Wizara yenye jukumu la msingi la kuelimisha jamii katika masuala makuu ya kitaifa pamoja na nyinyi Wasanii tukawa na ufahamu wa kutosha juu ya mategemeo yetu kwenu katika jambo hili muhimu la Kitaifa. Hasa la kuinadi Katiba Inayopendekezwa, kuhimiza wananchi kujiandikisha na kujitokeza kwa wingi kupiga kura ya maoni.

Kama mnavyofahamu na watoa mada walivyowasilisha kwenu kwamba katika Katiba Inayopendekezwa, yapo mambo mazuri yanayoendana na wakati uliopo sasa ukilinganisha na Katiba ya Mwaka 1977. Naamini kabisa baada ya kikao hiki, mmepata uelewa zaidi na ukweli kuhusu katiba Inayopendekezwa.  Tumieni sasa nafasi yenu kuwafikia wananchi kwa weledi na usahihi.  

Waifahamu Katiba Inayopendekezwa, wajiandikishe na kuipigia kura hapo ifikapo Aprili 30, 2015.  

Ni ukweli usiopingika kuwa Katiba Inayopendekezwa imesheheni haki za makundi mbalimbali bila kusahau kundi la wasanii na haki zenu zilizofafanuliwa vizuri katika Ibara ya 59 ya Katiba Inayopendekezwa.  Hii inamaanisha kwamba wasanii kwa mara ya kwanza kilio chenu kuhusu ulinzi na haki zetu kikatiba umezingatiwa.  Hivyo kazi zenu za ubunifu zitaweza kulindwa kikatiba

Ndugu Wasanii,
Nimeelezwa Mada zilizowasilishwa na kujadiliwa leo, zimetolewa na  mtu mahiri ambaye alishiriki katika Bunge Maalum la Katiba.  Hivyo ni matumaini yangu kwamba  kupitia kwake tutaongeza uelewa wetu juu ya wajibu wetu na umuhimu wa Katiba Inayopendekezwa. Ni matumaini yangu kwamba tumesikiliza, tumeuliza maswali, tumejadili na kutoa maoni ambayo yatatusaidia kutoa elimu sahihi kwa umma.  Hasa kwa kuisemea na kuitangaza Katiba Inayopendekezwa kwa mlengo wa kuvuka katika kura ya maoni na wingi wa kura ya Ndiyo.

Ndugu Wasanii,
Kwa mara nyingine nitumie nafasi hii kipekee kuwashukuru na kuwapongeza kwa kazi nzuri mnayoendelea kuifanya ya kuelimisha na kuburudisha Jamii bila kusahau kulitangaza Taifa la Tanzania . 

Mwisho nawaomba sana tusaidiane katika kufanikisha hili jambo muhimu tuweze kuendelea kujipanga vizuri katika kujenga na kuilinda nchi yetu.


Niwashukuru tena kwa kuja  na kushiriki nasi na niwatakie kazi njema ya kulijenga Taifa letu. 

No comments:

Post a Comment