TANGAZO


Monday, July 15, 2013

Uongozi wa Wizara ya Habari wakutana na Waandishi wa habari jijini Dar es Salaam na kutoa taarifa ya bajeti yake

Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari, Bi. Zamaradi Kawawa akifungua mkutano kati ya Wizara ya Habari Vijana Utamaduni na Michezo na waandishi wa habari, uliofanyika katika ukumbi wa Idara ya Habari, Maelezo jijini Dar es salaam leo. Kushoto ni Msemaji wa Wizara hiyo, Godlease Malisa na kulia ni Profesa Elisante Ole Gabriel wa wizara hiyo.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kutoka Wizara ya Habari Vijana Utamaduni na Michezo, Godlease Malisa akizungumza na vyombo vya habari kuhusu utekelezaji wa azma ya Serikali kusaidia vijana. Jumla ya sh. bilioni 6.1 zimetengwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2013/2013. Mkutano huo, umefanyika ukumbi wa Idara ya Habari jijini Dar es salaam leo. Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari, Zamaradi Kawawa.

Mkurugenzi wa Idara ya Vijana kutoka Wizara ya Habari Vijana Utamaduni na Michezo, Profes Elisante Ole Gabriel, akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari, kuhusu utekelezaji wa azma ya Serikali kusaidia Vijana. Jumla ya sh. bilioni 6.1 zimetengwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2013/2013 kwa ajili ya shughuli hiyo. Kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari, Zamaradi Kawawa.

Mkurugenzi wa Idara ya Vijana kutoka Wizara ya Habari, Vijana Utamaduni na Michezo Profesa Elisante Ole Gabriel, akibadilishana mawazo na waandishi wa habari katika mkutano huo jijini leo. (Picha zote na Hassan Silayo-Maelezo)


NDUGU waandishi wa Habari tunatambua kwamba hivi karibuni Serikali ilipitisha bajeti yake kwa ajili ya maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo Vijana ambayo imekuwa na changamoto nyingi ikiwemo uhaba wa ajira,hata hivyo Serikali imekuwa ikifanya jitihada za makusudi ili kuhakikisha inamkwamua kutoka katika janga la umasikini.
Katika  kutekeleza azma ya kusaidia Vijana, jumla ya shilingi Bilioni 6.1 zimetengwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2013/2013 ikiwa ni kwa ajili ya kusaidia mfuko wa Maendeleo ya Vijana, ambapo Vijana watapatiwa mikopo yenye unafuu katika riba na upatikanaji wake.  Natoa wito kwa vijana kuchangamkia fursa hii ambayo  haimuhitaji mkopaji kuwa na dhamana isiyo hamishika bali kuwa na uaminifu wa kurejesha mkopo huo na kujiunga kwenye SACCOS.
Ndugu Waandishi wa Habari, kwa kutambua umuhimu wa vijana katika maendeleo ya taifa letu, Serikali iliamua kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Vijana mnamo mwaka 1993/94, chini ya Sheria Na. 21 ya mwaka 1961 kifungu cha 17(1), ukiwa  na lengo la kuwasaidia Vijana kupata mikopo yenye masharti nafuu na kuwajengea uwezo kiuchumi  ili waweze kuanzisha au kuimarisha miradi yao kwa lengo la kuwawezesha kujitegemea na kukuza uchumi wa nchi.
Takwimu zinaonyesha kuwa kuna jumla ya Vijana milioni 16,195,370 ambapo takribani vijana 1,200,000 humaliza elimu ya vyuo mbalimbali kila mwaka na kati yao ni vijana 200,000 huajiriwa kwa mwaka. Ikumbukwe kuwa Vijana wanachukua asilimi 68 ya nguvu kazi ya Taifa lakini takwimu zinaonyesha kuwa upungufu wa ajira kwa Vijana ni asilimia 14.4.
Ndugu Waandishi wa Habari Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ambayo ndiyo yenye dhamana ya kuendesha mfuko huu tayari imeshapeleke muongozo mpya wa namna bora ya vijana kunufaika na mikopo katika Halmashauri zote nchini. Hivyo Vijana mnashauriwa kujiunga katika vikundi na kufanya mawasiliano na Maafisa Vijana katika Halmashauri zenu ili kujua taratibu za kupata mikopo hiyo.
Ndugu Waandishi napenda kutumia fursa hii kuwapongeza kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kuhabarisha umma hasa katika matukio makubwa yaliyotokea hivi karibuni nchini kwetu. Mmefanya kazi kubwa sana ya kutangaza mabadiliko ya ratiba ya Bunge la Bajeti kutoka Juni – Agosti na kuwa Aprili hadi Juni kila mwaka. Kadhalika mlitangaza ziara ya Rais Obama, ziara ya Rais wa Sri Lanka, Mkutano wa Smart partnership na Maonyesho ya Sabasaba.
Ndugu waandishi wa Habari, Serikali imepokea kwa msikitiko kifo cha mwandishi mkongwe marehemu David Majebele aliyefariki jana alfajiri na msiba upo nyumbani kwake Sinza Plot Na. 262 Block E, Mtaa wa Lion Hotel, ambapo mazishi yanatarajiwa kufanyika siku ya Alhamisi katika makaburi ya Kinondoni. Wizara inatoa pole na salam za rambirambi kwa ndugu, jamaa na familia ya Marehemu, Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi AMINA.
Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ilianzishwa mwaka 2006. Wizara hii inaundwa na Idara nne za kisekta ambazo ni Idara ya Habari, Idara ya Maendeleo ya Vijana, Idara ya Maendeleo ya Utamaduni na Idara ya Maendeleo ya Michezo.
Imetolewa na
Bw. Godlease Malisa
Mkuu wa Kitengo Cha Mawasiliano Serikalini
15 Julai, 2013


No comments:

Post a Comment