Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein (wa pili kulia), akiwahutubia Wananchi, katika sherehe za ufunguzi wa jengo la Chuo cha Utumishi wa Umma, lililopo Tunguu Mkoa wa Kusini Unguja leo, katika shamra shamra za kilele cha miaka 49 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar. Kulia ni Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Iddi, Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Maalim Abdalla Suleiman (wa pili kulia) na kushoto ni Waziri wa Utumumishi wa Umma na Utawala Bora Haji Omar Kheir.
Na Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar.
Zanzibar, 5.1.2013
DHAMIRA ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba kama ilivyokuwa kwa awamu zilizotangulia, ni kuona kila mfanyakazi anaendeleza shabaha ya Mapinduzi na kunufaika na matunda yake ikiwa ni pamoja na kuwekewa maslahi na mazingira bora ya ufanyajikazi.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo, huko Tunguu, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja, katika uzinduzi wa jengo jipya la Chuo cha Utawala wa Umma, ikiwa ni miongoni mwa shamra shamra za Sherehe za Mapinduzi ya Januari 12, 1964 ambayo yanatimiza miaka 49.
Katika hotuba yake, Dk. Shein alisema kuwa Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964 ambayo sasa yanatimiza miaka 49 ndio chimbuko la mafanikio yote ya Zanzibar.
alisema kuwa kufungua kwa jengo hilo la Chuo cha Utumishi wa Umma ni juambo ambalo ni miongoni mwa uendelezaji wa shabaha ya Mapinduzi ya kuwajengea uwezo watumishi wa Serikali ili wawe na ujuzi, maarifa, bidii, uadilifu na ubunifu kwa kuweza kutoa huduma bora kwa wananchi. Alieleza kuwa tegemeo la Serikali na wananchi ni kuwa Chuo hicho kiwe ndio kituo cha kumjenga mtumishi bora.
Kutokana na hilo Dk. Shein alisisitiza kuwa ni lazima Chuo hicho kihakikishe kwamba mitaala yake, kozi wanazofundisha, wakufunzi na vifaa vya Chuo vinaendana na mahitaji ya wakati pamoja na mategemeo ya wananchi wa Zanzibar.
Dk. Shein alitoa wito kwa Taasisi za Serikali na za binafsi kukitumia Chuo hicho kwa kuwapa mafunzo wafanyakazi wao kwa mujibu wa kosi zinazotolewa na Chuo hicho.
Aidha, Dk. Shein alisema kuwa katika kipindi cha miaka 49 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar, mafanikio makubwa yamepatikana kutokana na ushirikiano, umoja na mshikamano kulikotokana na amani na utulivu nchini.
Alisisitiza kuwa hali hiyo imechangiwa na watumishi wa umma kuimarisha uwajibikaji na utoaji wa huduma bora kwa wananchi wote bila ya ubaguzi wakiamini kuwa wananchi wote wanastahiki kupatiwa huduma katika hali ya usawa.
“Jitihada zinaendelea kufanywa ili kuandaa miundombinu na mazingira mazuri katrika Ofisi za Serikali ya kufuatilia huduma kwa wananchi wetu wenye mahitaji maalumu wakiwemon wazee na watu wenye ulemavu’,alisisitiza Dk. Shein.
Sambamba na hayo, Dk. Shein aliupongeza uongozi wa Wizara ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora pamoja na wafanyakazi wake wote. Aidha, alitumia fursa hiyo kuwapongeza watumishi wote kwa kazi nzuri na mafanikio yaliopatikana.
Dk. Shein, aliahidi kufanya jitihada za kuhakikisha awamu ya pili ya ujenzi huo inaendelea vizuri, pongezi kwa wajenzi na washauri katika awamu zote mbili kwa kufanya kazi kwa umahiri mkubwa huku akitoa pongezi kwa Waziri kwa matarajio ya Chuo hicho yaliowekwa.
Pia, katika sherehe hizo Dk. Shein aliahidi kukidhamini kikundi cha sanaa cha Matofali katika kurikodi igizo lao juu ya uwajibikaji kazini waliolionesha katika hafla hiyo.
Nae Waziri wa Wizara hiyo, Mhe. Haji Omar Kheir alisema kuwa Chuo kimeweza kutoa mafunzo ya muda mrefu na mfupi kwa ajili ya kujenga uwezo katika kada mbali mbali, zikiwemo utawala, ununuzi na ugavi, utunzajiwa shughuli za afisi, ICT, ugavi na nyenginezo kwa wafanyakazi.
Alieleza kuwa vijana wengi wamepokewa katika fani mbali mbali. ikiwa ni miongoni mwa utekekelezaji Mapinduzi pamoja na Ilani ya CCM katika kuwaendeleza vijana.
Alisema kuwa Chuo kimepata usajili wa kudumu na kutambulika , kitaifa, na kikanda, NACTE, na kueleza kuwa hivi sasa tayari chuo kimeshatimiza miaka mitano tokea kuanzishwa kwake ambapo kabla ya hapo kikijulikana kama ni Chuo cha Uchumi.
Waziri huyo alieleza kuwa ni mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa chuo hicho kupata jenzo lake wenyewe, na kumpongeza Rais kwa kuliongoza Taifa sanjari na jitihafa zake za kuimarisha utumishi wa umma. Alisema kuwa kwa muda mrefu chuo hicho kilikuwa kikitumia majengo ya kuanzima na majengo ya kukodi, na kuomba kumalizika kwa sehemu iliyobaki.
Alisema kuwa azma kubwa na chuo hicho ni kuwa cha kisasa na chenye huduma zote muhimu kama nyumba na mikahawa na kueleza kuwa hivi sasa wamo katika kuangalia uwezekano wa kuzifanyia kazi changamoto hizo.
Mapema Naibu Katibu wa Wizara hiyo, Yakuti Hassan, alisema kuwa hadi hatua hiyo ya ufunguzi tayari zimetumika zaidi ya Shilingi Bilioni 1 kwa hatua ya kwanza ya ujenzi ambayo imeshakamilika na tayari katika Bajeti ya mwaka huu zimeshaobwa Shilingi milioni 300 kwa ajili ya kukamilisha ghorofa ya pili.Katika hafla hiyo viongozi mbali mbali wa vyama na serikali pamoja na wananchi walihudhuria, akiwemo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Idd.
|
No comments:
Post a Comment