TANGAZO


Sunday, May 27, 2018

MWANRI AWATANGAZIA KIAMA WANAOSHIRIKI KULA UBWABWA NA KUSHEREHEKEA NDOA ZA WATOTO WADOGO

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri
Na Tiganya Vincent 
26 May 2018
MKUU wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri ametanga kiama kwa watu wote wanaoshiriki kuwaoza watoto wadogo wakiwemo wa Shule kwa kuwakata na kuwafikisha Mahakamani ili waweze kuadhibiwa.
Hatua hiyo inalenga kukomesha mimba na ndoa za utotoni kwa watoto wa kike ikiwa ni sehemu ya kutetea haki za watoto wa kike kupata elimu kama walivyo wavulana na vile kuokoa maisha yao ambayo yanaweza kupotea wakati wa kijifungua kwa kuwa bado ni wadogo.
Mwanri alitoa amri hiyo jana katika vijiji vya Wilaya ya Igunga na Urambo mbalimbali wakati wa kampeni yake ya kutokomeza ndoa na mimba za utotoni.
Aliwaagiza Vyenyeviti wa Serikali za Mitaa, vijiji au  kuanza mara moja zoezi la kuwakamata watu wote ambao wataokutwa wakila  wali au kushabikia sherehe za ndoa ambayo Bibi harusi ni motto mdogo au mwanafunzi.
Mwanri alisema ni jambo la aibu kuona mfumo wa serikali upo kuanzia ngazi ya kijiji hadi Mkoa lakini bado Tabora inaendelea kutajwa kuwa miongoni mwa vinara wa mimba na ndoa za utotoni.
Mwanri alisema kuwa kiongozi wa ngazi yoyote akiwemo polisi akikuta kuna harusi ya mtoto aliye chini ya miaka 18 awe mwanafunzi au sio akamate watu wote wanaosherekea tukio hilo haramu kwa sababu linarudisha nyuma juhudi za kumkomboa mtoto wa kike kutoka mfumo dume.
“Ukifika katika harusi kabla ujaanza kula chakula ulinza binti aliyefunga ndoa ana umri gani…kama ni chini ya miaka 18 usile chakula ondoka…OCD , Mtendaji ukikutana aliyefungishwa ndoa ni chini ya miaka 18 …wapambe somba… mashangazi somba…bibi harusi na bwana harusi somba” alisisitiza
“Waliokula ubwabwa somba…aliyebeba ubwabwa wa harusi hiyo na kupeleka kwake somba…tutachambua mmoja baada ya mmoja ili kujua mwenye hatia na asiye na hatia tutamwachia ili watu wanyoke na waache kuwafuata watoto wadogo”alisema .
Mkuu huyo wa Mkoa alisema ili kuepuka kuingia katika matatizo ni vema vijana na watu wazima wanaonyemelea watoto wa kike na wale wanaoshabikia ndoa za utotoni kuacha mara moja na kutoa taarifa kwa mamlaka husika wanapoona mtu mwenye tabia chafu kama hizo ili awe kuchukuliwa hatua.
Alisema akiwa amepewa dhamana ya kuongoza Mkoa wa Tabora hatakubali kuendelea kupata aibu ya kunyoshewa vidole kwa mambo mabaya kama vile kuongoza katika mauaji , watoto kuwa watoro , mimba na ndoa za utotoni.
Mwanri aliwaonya viongozi na watendaji ambao watashindwa kusimamia utekelezaji wa kukomesha tabia hizo atawachukulia hatua ikiwemo kuwasimamisha na hatimaye kupendekeza wafukuzwe kazi ambao wako katika Mamlaka za juu.

No comments:

Post a Comment