Mhandisi wa Meli
kutoka Chuo cha Bahari Dar es Salaam, Capt. Jumanne Karume. akimwelezea Naibu
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani namna meli
inavyoendeshwa kwenye chumba cha nahodha, alipotembelea chuo hicho wakati wa
mahafali ya 12 ya chuo hicho jijini Dar es Salaam.
Naibu Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani (kushoto), akiwatunuku
wahitimu wa moja ya kozi zinazotolewa na Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI),
jijini Dar es Salaam. Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani (kulia), akimkabidhi zawadi mwanafunzi aliyefanya vizuri katika mahafali ya Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI), jijini Dar es Salaam.
Naibu Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani (kulia) na Makamu
Mwenyekiti wa Bodi ya DMI, Bi. Rukia Shamte, wakiangalia zawadi aliyopewa mgeni
rasmi na Chuo hicho katika mahafali ya chuo hicho, jijini Dar es Salaam.
NAIBU Waziri wa Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Edwin Ngonyani, ameutaka uongozi wa Chuo cha Bahari
cha Dar es salaam (DMI), kubuni na kutafuta vyanzo madhubuti vya mapato ili
kusaidia kutatua changamoto zilizopo chuoni hapo.
Akizungumza katika
Mahafali ya 12 ya Chuo hicho yaliyofanyika jijini Dar es salaam, Mhandisi
Ngonyani amesema kuwa uwepo wa vyanzo imara vya mapato chuoni hapo utapelekea
kutimiza malengo yake ya kutoa elimu na mafunzo yanayokubalika ndani na nje ya
nchi.
“Wizara ingependa
kuona DMI inaongeza ubunifu wa kutafuta vyanzo madhubuti vya mapato, Mkiwa na
fedha mtaweza kutatua changamoto ndogo ndogo mlizonazo na kufikia malengo
mliojiwekea”, amesema Mhandisi Ngonyani.
Ameutaka uongozi huo
kukamilisha na kuwasilisha haraka upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa
mahitaji halisi ya majengo ya madarasa na ofisi za walimu ili kuiwezesha
serikali kuchukua hatua stahiki.
Aidha, amewahakikishia
wanafunzi kuwa Serikali itaendelea kusimamia mazoezi ya vitendo kwa wanafunzi
wanaochukua fani mbalimbali chuoni hapo ili waweze kukubalika ndani na nje ya
nchi.
Kwa upande wake Mwenyekiti
wa Bodi chuoni hapo Bi Rukia Shamte, amemhakikishia Naibu Waziri huyo
kukamilisha taarifa ya Upembuzi yakinifu na kuiwasilisha kwake ili kuweza
kufanyiwa kazi.
Ameiomba Serikali
kuongeza bajeti kwa ajili ya chuo hicho ili kuboresha miundombinu ya chuo
ikiwemo ununuzi wa vifaa mbalimbali vya
mafunzo na ujenzi wa madarasa.
“ Kwa sasa tupo katika
hatua ya mwisho za kumaliza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa ujenzi wa
jengo la wakufunzi pamoja na madarasa ili kukifanya chuo kibaki kwenye hadhi ya
kimataifa, tukimaliza tutawasilisha serikalini kwa hatua zaidi, amesema
Mwenyekiti wa Bodi.
Zaidi ya wahitimu 70
wa fani mbalimbali wamehitimu katika mahafali ya 12 ya chuo hicho yaliyofanyika
jijini Dar es salaam.
Imetolewa
na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano.
No comments:
Post a Comment