Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Mhe. Sophia Simba
A: UTANGULIZI
1. Mheshimiwa
Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo
ndani ya Bunge lako Tukufu na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Maendeleo ya Jamii iliyoichambua bajeti ya Wizara yangu, naomba kutoa hoja
kwamba sasa Bunge lako tukufu likubali kupokea na kupitisha makadirio ya
Matumizi ya Kawaida na ya Maendeleo ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na
Watoto kwa mwaka 2015/16.
2. Mheshimiwa
Spika, niruhusu nianze kwa kumshukuru
Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema na utukufu kwa kuniwezesha kusimama mbele ya
Bunge lako Tukufu nikiwa na afya njema na hivyo kuweza kushiriki mkutano huu wa
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
3. Mheshimiwa
Spika, napenda pia kutumia fursa hii
kuwapongeza kwa dhati Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Mohammed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Mizengo Peter Pinda (Mb.), Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi wao mahiri na maelekezo yao
ambayo yamewezesha kushamiri kwa usawa wa jinsia na uzingatiaji wa haki za
mtoto katika jamii ya Watanzania. Mwenyezi Mungu awajalie afya njema ili
waendelee kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
4. Mheshimiwa
Spika, napenda kukupongeza Mhe Spika, Naibu
Spika na Wenyeviti wa Bunge kwa uendeshaji bora wa shughuli za Bunge.
Tunaendelea kumuomba Mwenyezi Mungu awajalie afya njema ili muweze kusimamia na
kuratibu shughuli za Bunge kwa ufanisi.
5. Mheshimiwa
Spika, kwa namna ya pekee napenda kuishukuru
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii ikiongozwa na Mwenyekiti mahiri
Mheshimiwa Said Mohamed Mtanda na Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Albert Obama
Ntabaliba, kwa kuchambua na kujadili bajeti ya Wizara yangu. Ushauri na
maelekezo ya Kamati hiyo yamewezesha Wizara yangu kuandaa bajeti kwa ufanisi.
6. Mheshimiwa
Spika, naomba kuchukua fursa hii kuwapongeza wabunge
waliochaguliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao ni Dkt. Grace
Khwaya Puja na Innocent Rwabushaija Sebba kuwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania.
7. Mheshimiwa
Spika, naomba kutoa salamu za pole kwako,
Bunge lako Tukufu, familia na wananchi wa Jimbo la Mbinga Magharibi kwa kifo
cha aliyekuwa Mbunge wao na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Maendeleo ya Jamii Mheshimiwa Kapteni Mstaafu John Damiani Komba. Bunge hili
litamkumbuka daima kwa michango yake. Aidha, kwa masikitiko makubwa natumia
fursa hii kuwapa pole wale wote waliopatwa na majanga ya ajali na mafuriko
pamoja na kufiwa na ndugu, jamaa na wapendwa wao katika matukio mbalimbali
yaliyotokea hapa nchini. Nitangulize dua zangu kwa Mwenyezi Mungu awapokee na
kuwalaza mahali pema peponi. Amina.
B: MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA ILANI YA
UCHAGUZI YA CCM KWA KIPINDI CHA MWAKA 2005 HADI 2015
I. Ajira
na Uwezeshaji wa Wananchi
Mheshimiwa Spika, Udahili wa
washiriki katika Elimu ya Wananchi na ufundi stadi kupitia vyuo vyetu vya
maendeleo ya wananchi umeongezeka kutoka washiriki 25,486 mwaka 2005 hadi
kufikia washiriki 40,692 mwaka 2015 na idadi ya wasichana waliopata mafunzo ya
“Mama course” iliongezeka kutoka 60 mwaka 2005 hadi kufikia wasichana 449 mwaka
2014. Wizara yangu ilibuni “mama course” mwaka 2000 kwa lengo la kuwapa
wasichana waliopata mimba wakiwa shuleni fursa ya kujiendeleza kielimu kupitia
mafunzo ya elimu ya wananchi baada ya kupoteza fursa hiyo katika mifumo rasmi
kutokana na kanuni na taratibu za uendeshaji wa Elimu ya Msingi na Sekondari
Tanzania. Aidha, kwa mwaka, jumla ya washiriki 36,838 walihitimu katika Vyuo
vya Maendeleo ya Wananchi, kati yao, 22,939 ni wanaume na 13,899 ni wanawake.
Wahitimu 33,319 sawa na asilimia 90.44 ya wahitimu kutoka katika vyuo vya
Maendeleo ya wananchi wamejiajiri na wahitimu 3,047 sawa na asilimia 8.27 ya
wahitimu wa Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi wameajiriwa katika makampuni ya watu
binafsi na Taasisi mbalimbali za Serikali.
II. Uendelezaji
wa Makundi Mbalimbali
Maendeleo ya Watoto
8. Mheshimiwa
Spika, Wizara iliwasilisha taarifa ya 3, 4
na 5 za Nchi yetu kuhusu utekelezaji wa Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Mtoto.
Aidha, Wizara inaandaa taarifa ya 2 na 3 ya utekelezaji wa Mkataba wa Afrika
Kuhusu Haki na Ustawi wa Mtoto ambayo itawasilishwa katika Kamati ya Umoja wa
Afrika ya Haki na Ustawi wa Mtoto.
9. Mheshimiwa
Spika, Wizara imeandaa na kuanza kutekeleza
Mpango Kazi wa Taifa wa Miaka Mitano wa Ushiriki wa Watoto. Mpango huo utatoa
fursa kwa wazazi na walezi kujifunza njia bora za mawasiliano na mahusiano
mazuri kati yao na watoto. Aidha, Mpango Kazi huu utabainisha namna ya
kuwashirikisha watoto katika majadiliano na hata kunufaika na michango yao
kimawazo, kiushauri na katika utekelezaji wa maamuzi mbalimbali ya kutatua
matatizo yao.
Maendeleo ya Wanawake
10. Mheshimiwa
Spika, Serikali imeendelea kuwahamasisha
wanawake kujiendeleza kielimu na kujenga uelewa wao katika kuweka nguvu za
kutetea haki zao na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kimaendeleo. Aidha,
wanawake wamejengewa uwezo wa ujasiriamali, utaalam wa biashara, jinsi ya kupata
mitaji zaidi, masoko pamoja na kutoa mikopo mbalimbali.
III. Taasisi
ya Maendeleo ya Jamii Tengeru
11. Mheshimiwa
Spika, Wizara kupitia Chuo cha Maendeleo ya
Jamii Tengeru iliendelea kudahili wanafunzi katika ngazi ya Shahada ya Kwanza
kuanzia mwaka 2008/09 katika fani ya uandaaji na usimamizi shirikishi wa
miradi, usimamizi wa programu za maendeleo ya jamii, maendeleo ya jinsia na
stashahada ya uzamili ya maendeleo ya jamii. Udahili wa wanachuo umeendelea
kuongezeka mwaka hadi mwaka, katika mwaka 2012/13, jumla ya wanachuo 139
wakiwemo wanaume 64 na wanawake 75, walidahiliwa. Mwaka 2013/14, jumla ya
wanachuo 234 wakiwemo wanaume 88 na wanawake 146 walidahiliwa na katika mwaka
2014/15, jumla ya wanachuo 276, wakiwemo wanawake 189 na wanaume 87 walidahiliwa.
12. Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha mwaka 2014/15,
Serikali ilikipandisha hadhi Chuo cha Maendeleo ya Jamii Tengeru kuwa Taasisi
ya Maendeleo ya Jamii Tengeru kupitia Azimio Na.1 la Bunge la Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania la mwezi wa Aprili, 2014, katika Mkutano wake wa 17 Kikao
cha 27 Taasisi hii inatarajiwa kuongeza Wataalamu wa Maendeleo ya Jamii wa
Ngazi ya Shahada ya maendeleo ya jamii ambao ni muhimu sana katika kuimarisha
utendaji wa shughuli za Maendeleo ya Jamii. Hasa katika ngazi ya Halmashauri
ambapo kuna uhaba mkubwa wa watumishi hawa.
IV. Demokrasia
na Mamlaka ya Umma
13. Mheshimiwa
Spika Wizara yangu kupitia Baraza la Taifa
la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ilitunga na kupitisha Kanuni za Maadili ya
NGOs. Utekelezaji wa Kanuni za Maadili ya NGOs umelenga kukuza uwazi,
uwajibikaji na uwezo wa Mashirika haya kujitathimini na kujikagua katika
utekelezaji wa shughuli zao kulingana na katiba au miongozo ya kusajiliwa kwao.
Kanuni hizi zimeamsha ari ya wadau wa NGOs kujitafiti na kubaini maeneo ambayo
wana uwezo mkubwa wa kusaidia jamii na kuyaendeleza maeneo ambayo wako dhaifu
kubuni mikakati ya kujijengea uwezo ili kutekeleza kwa ufanisi majukumu yao
katika sekta mbalimbali nchini.
14. Mheshimiwa
Spika, hatua nyingine ambazo Wizara yangu
imechukua ni pamoja na kuanzishwa kwa Tovuti Maalum ya Uratibu wa Mashirika
Yasiyo ya Kiserikali (http//:www.tnnc.go.tz) ambayo hutumiwa na wadau
mbalimbali ikiwemo wanufaika wa miradi ya NGOs kutolea mrejesho kuhusu utendaji
wa NGOs katika maeneo yao. Idadi ya wadau ambao wametoa mrejesho kuhusu
utendaji wa NGOs hadi kufikia Machi, 2015 ni 30,679. Aidha, Wizara imekuwa
ikitembelea na kukagua shughuli/kazi, miradi na program mbalimbali
zinazotekelezwa na NGOs nchini kwa lengo la kutathimini utendaji na uendeshaji
wa Mashirika hayo, ambapo jumla ya Mashirika 66 yamefikiwa hadi kufikia Machi,
2015.
Pamoja na mafanikio hayo, NGOs
zinakabiliwa na changamoto zifuatazo: Baadhi ya Wilaya na Halmashauri za Majiji
katika maeneo yao wameshindwa kuunda Kamati za Maadili ya NGOs ili kuwezesha
mashirika haya kujidhibiti, kutandaa na kutathmini utendaji wao katika maeneo
mbalimbali wanakoendesha miradi ya kusaidia na kukuza uwezo wa jamii
C: HALI HALISI YA SEKTA YA MAENDELEO
YA JAMII NA CHANGAMOTO ZILIZOPO
Hali ya Maendeleo ya Jamii nchini
15. Mheshimiwa
spika, utekelezaji wa dhana ya Maendeleo ya
Jamii ambayo ni dhana shirikishi unajenga na kuimarisha misingi ya watu katika
jamii kujitambua kwa kutambua uwezo walionao wa kubaini matatizo yao, kuweka
vipaumbele, kubaini fursa na rasilimali walizonazo, kupanga na kutoa maamuzi ya
kazi au miradi ya kutekeleza ili kutatua kero na matatizo yao. Kipimo cha
mafanikio ya dhana hii ni ongezeko la watu katika jamii kubadilika katika
kifikra na kimtazamo na kushiriki kikamilifu katika masuala yanayowaletea
maendeleo endelevu. Katika kufanikisha haya, Wataalam wa maendeleo ya Jamii ni
muhimu katika kuhamasisha, kuraghabisha, kushauri, kushawishi na kuelimisha
wananchi na viongozi wao kwa kuwapatia elimu, maarifa na taarifa mbalimbali ili
kuwaongezea uelewa, uwezo wa kufikiri na kufanya maamuzi sahihi ya utekelezaji
wa dhana hiyo.
16. Mheshimiwa
Spika, Pamoja na umuhimu wa Wataalam wa
Maendeleo ya Jamii kama ilivyobainishwa katika Sera ya Maendeleo ya Jamii
(1996) inayosisitiza kuwepo kwa Mtaalam wa Maendeleo ya Jamii mmoja kila kata
ili kuchochea ari na mwamko wa wananchi katika kujiletea maendeleo yao, Sekta
hii bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazosababisha utekelezaji
usioridhisha wa dhana ya maendeleo ya jamii nchini. Hadi sasa Wataalam, waliopo
katika Halmashauri za Wilaya na Manispaa ni 2,774, kati ya hao walioko Makao
Makuu ya Wilaya ni 1,464, kwenye Kata ni 1,310. Kwa sasa kuna jumla ya kata
3,339 nchini na hivyo kufanya upungufu wa Wataalam wa Maendeleo ya Jamii kuwa
2,029 katika Kata.
Aidha, wataalamu hao wanakabiliwa na
changamoto ya ukosefu wa vitendea kazi na vyombo vya usafiri. Changamoto hizi zimesababisha
maeneo mengi hasa vijijini kukosa wahamasishaji na waraghibishi na hivyo kubaki
nyuma katika suala zima la kujiletea maendeleo. Aidha, wananchi wameendelea
kukosa elimu, ujuzi na taarifa mbalimbali zihusuzo maendeleo. Upungufu huo pia
umesababisha ufuatiliaji usioridhisha wa shughuli mbalimbali za maendeleo
katika Jamii.
17. Mheshimiwa
Spika, katika kukabiliana na changamoto
hizo, Wizara inaendelea kuwasiliana na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi
wa Umma juu ya uwezekano wa kuwaajiri wataalam wa Maendeleo ya jamii moja kwa
moja kutoka vyuoni.
Vyuo vya Maendeleo ya Jamii
18. Mheshimiwa
Spika, Mwaka 1960 serikali ya kikoloni
ilianzisha Chuo cha Maendeleo ya Jamii Tengeru. Chuo hiki kilianza kwa kutoa
mafunzo ya ngazi ya Astashahada. Mwaka 1983 chuo kilianza kutoa mafunzo ya
Stashahada ya juu. Hivi sasa Chuo hiki ni Taasisi inyotoa mafunzo ya Shahada za
Maendeleo ya Jamii, Jinsia na maendeleo na Mipango na usimamizi shirikishi wa
miradi ya maendeleo ya jamii. Halikadhalika, Taasisi inatoa Stashahada ya
Uzamili katika masuala ya maendeleo ya jamii. Aidha, Vyuo vya Maendeleo ya
Jamii Buhare, Rungemba na Misungwi vinatoa wataalam wengi zaidi wenye viwango
tofauti vya taaluma, ili kukidhi mahitaji ya maendeleo ya jamii ngazi ya cheti
na diploma. ya wataalamu wa Maendeleo ya Jamii katika Vijiji, Kata na
Halmashauri.
19. Mheshimiwa
Spika, Vyuo hivi vinakabiliwa na uhaba wa
majengo, vifaa vya kufundishia na kujifunzia, vyombo vya usafiri, na upungufu
wa watumishi hasa wakufunzi. Licha ya changamoto hizi, udahili umeongezeka
kutoka wanachuo 940 mwaka 2005/06 hadi kufikia 3,634 mwaka 2014/15 kama inavyoonekana
katika Hali ya Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi.
20. Mheshimiwa
Spika, Vyuo hivi vilianzishwa kati ya miaka
ya 1970 na 1980 kwa kurithi majengo yaliyokuwa yakitumika na taasisi mbalimbali
kama vile Vyuo vya Maendeleo Vijijini (Rural Training Centre’s), Shule za Kati
(Middle Schools), Vituo vya Mafunzo ya Ushirika na Vituo vya Mafunzo ya
wakulima (Farmers Training Centres). Majengo haya yalijengwa kati ya mwaka 1950
hadi 1963. Kutokana na umri wa majengo haya, kwa sasa ni machakavu na
hayaendani na mahitaji ya kutolea mafunzo kwa sasa. Madhumuni ya kuanzishwa kwa
vyuo vya Maendeleo ya Wananchi ni kujenga uwezo wa wananchi wa kujitegemea kwa
kuinua hali za maisha yao na ya Taifa kwa ujumla.Tangu kuanzishwa kwake vyuo
hivi vimekuwa vikitoa mafunzo ya stadi na maarifa ya kuwawezesha wananchi
kuajiriwa, kujiajiri na kuajiri wengine. Mafunzo haya huwajengea wananchi uwezo
wa kuongeza uzalishaji mali wenye tija na ambao huongeza pato la kaya na hivyo
kupunguza umasikini katika familia na Taifa kwa ujumla.
21. Mheshimiwa
Spika, Hivi sasa kuna jumla ya vyuo 55 vya
Maendeleo ya Wananchi ambavyo vipo katika wilaya mbalimbali nchini na baadhi ya
wilaya zina zaidi ya chuo kimoja. Vyuo hivi vinatoa mafunzo na stadi mbalimbali
kwa wananchi kama matumizi bora ya pembejeo, kilimo, uashi na useremala pamoja
na stadi nyingine za maisha. Vyuo hivi pia vinatoa mafunzo ya Ufundi Stadi kwa
kushirikiana na VETA. Kutokana na uchakavu wa majengo na miundombinu ya vyuo
hivi, wizara inaendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia, jitihada mbalimbali
zimefanywa na Wizara za kujenga majengo mapya, kufanya ukarabati wa majengo ya
zamani na kuboresha mifumo ya maji na umeme.
Changamoto na namna ya kuzitatua
22. Mheshimiwa
Spika, Pamoja na mafanikio yaliyopatikana,
Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi vinakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo:
mahitaji makubwa ya rasilimali fedha na watumishi, ubovu na uchakavu wa majengo
na miundombinu, ukosefu wa vifaa vya mafunzo, vyombo vya usafiri na maeneo ya
vyuo kuvamiwa na wananchi kwa shughuli za kilimo na ujenzi wa makazi.
23. Mheshimiwa
Spika, katika kukabiliana na changamoto
hizi, Wizara imeendelea kuboresha mazingira ya utoaji mafunzo Vyuoni kwa
kuajiri watumishi wa kada mbalimbal,i kufanya ukarabati wa majengo na
miundombinu na kuvipatia vyuo nyenzo na zana za kufanyia kazi kulingana na rasilimali
zilizopo.
Hali ya Maendeleo ya Jinsia nchini
Uwezeshaji wa wanawake
24. Mheshimiwa
Spika, Serikali imekuwa mstari wa mbele
katika kuhakikisha kuwa usawa wa jinsia nchini unazingatiwa katika mipango na
mikakati ya utekelezaji katika nyanja za kiuchumi, kijamii na kisiasa. Kupitia
programu na mikakati mbalimbali ya kuleta usawa wa jinsia, mafanikio makubwa
yamepatikana kwa mfano: Idadi ya Mawaziri wanawake imeongezeka kutoka Mawaziri
wanawake 6 kati ya Mawaziri 25 mwaka 2005 hadi kufikia Mawaziri wanawake 10
kati ya Mawaziri 30 mwaka 2015; Wakuu wa Wilaya wanawake wameongezeka kutoka 20
kati ya Wakuu wa Wilaya 104 mwaka 2005 hadi kufikia Wakuu wa Wilaya wanawake 46
kati ya Wakuu wa Wilaya 133 mwaka 2015; Majaji wanawake wameongezeka kutoka
Majaji wanawake 8 kati ya Majaji 50 mwaka 2005 hadi kufikia Majaji wanawake 24
kati ya Majaji 67 mwaka 2015; na Wabunge Wanawake wameongezeka kutoka Wabunge
wanawake 62 kati ya Wabunge 288 mwaka 2005 hadi kufikia Wabunge wanawake 127
kati Wabunge 357 mwaka 2015. Aidha, Katika kuhakikisha wanawake
wanapata fursa ya elimu, mafunzo na ajira, idadi ya Madirisha ya Taarifa kwa
Wanawake yameongezeka kutoka madirisha manne mwaka 2005 hadi kufikia madirisha
12 mwaka 2014. Jumla ya wanawake 14,589 wamefikiwa na watoa huduma wa dirisha
kupitia huduma ya mmoja mmoja katika ofisi za Madirisha ya Taarifa kwa
Wanawake.
25. Mheshimiwa
Spika, katika kuwezesha wanawake kiuchumi,
Wizara kupitia Benki ya Wanawake Tanzania imetoa mafunzo ya ujasiriamali na
mikopo yenye thamani ya Sh. bilioni 24.86. Mikopo hiyo imewezesha wajasiriamali
kujiajiri katika shughuli mbalimbali za biashara na hivyo kuinua vipato vyao
kiuchumi na kijamii. Aidha, Benki ya Wanawake imeongeza vituo vya kutolea
huduma za kibenki kutoka vituo 18 mwaka 2012/13 hadi kufikia vituo 81 mwaka
2013/14.
26. Mheshimiwa
Spika, Idadi ya wanawake wanaopata mikopo
kutoka Mfuko wa Maendeleo wa Wanawake imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka.
Kiasi cha fedha kilichokopeshwa kimeongezeka kutoka Sh. 260,000,000 mwaka 2005
hadi kufikia Sh. bilioni 1,900,000,000 mwaka 2014. Mikopo hiyo imewawezesha wanawake
kufanya shughuli za ujasiriamali ikiwa ni pamoja na: ufugaji; utengenezaji wa
mvinyo; usindikaji wa mazao, mbogamboga, matunda na nafaka; kilimo cha bustani
za mboga na mazao mbalimbali; biashara ya kuuza na kununua mazao kama mahindi,
mpunga, ufuta, karanga, alizeti na mchele; ufumaji; ususi wa mikeka na vikapu.
Aidha, mikopo hiyo imewawezesha kuinua vipato vyao na kuweza kugharamia
mahitaji mbalimbali ya msingi kama vile; kulipia gharama za matibabu, kusomesha
watoto, kujenga na kukarabati nyumba zao.
Ukatili na ubaguzi wa kijinsia
27. Mheshimiwa
Spika, Wizara pia imeendelea kutekeleza
Mpango Kazi wa Kitaifa wa Kuzuia na Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na
Watoto (2001-2015) kwa kuijengea uwezo Kamati ya Kitaifa ya Kuzuia Ukatili
Dhidi ya Wanawake na Watoto ili iweze kushughulikia masuala ya ukatili,
kuratibu Kampeni za Kutokomeza Vitendo vya Ukatili Dhidi ya Wanawake ili
kuongeza uelewa wa madhara ya vitendo vya ukatili katika jamii na kuandaa
Mwongozo wa Kuzuia na Kudhibiti Ukatili wa Kijinsia kwa Kamati za Vijiji,
Mitaa, Kata na Wilaya.
Utekelezaji wa mikataba ya kikanda na
kimataifa
28. Mheshimiwa
Spika, Katika kutekeleza mikataba na
maazimio mbalimbali ya kikanda na kimataifa ambayo nchi imeridhia, Wizara
imeendelea kushiriki katika mikutano na kutekeleza mikataba mbalimbali ya
kikanda na kimataifa ikiwa ni pamoja na kutoa michango na uzoefu wake katika kuboresha
na kuimarisha usawa wa jinsia na uwezeshaji wa Wanawake. Mikutano hiyo hutoa
fursa kwa washiriki kujadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya
wanawake na haki za wasichana na kutoa mapendekezo ya kiutekelezaji katika
kufikia usawa wa jinsia.
Changamoto za Kuleta Maendeleo ya
Jinsia
29. Mheshimiwa
Spika, Pamoja na mafanikio yaliyopatikana
bado zipo changamoto mbalimbali ambazo ni; Mahitaji makubwa ya mikopo ya Mfuko
wa Maendeleo wa Wanawake, mafunzo ya ujasiriamali yanayotolewa kwa wakopaji
kutotosheleza kujenga uwezo unaohitajika, marejesho hafifu ya mikopo, mahitaji
makubwa ya huduma za Benki ya Wanawake Tanzania hususan kwa wanawake
wajasiriamali wa vijijini. Aidha, wanawake wengi kushindwa kushika nafasi za
uongozi na maamuzi kutokana na majukumu mengi ya familia. Kuendelea kuwepo kwa
mila na desturi ambazo zinahamasisha ndoa za utotoni na hivyo kuendeleza
ukandamizaji kwa watoto wa kike na kusababisha mimba za utotoni.
30. Mheshimiwa
Spika, Katika kukabiliana na changamoto hizo
hatua mbalimbali zimechukuliwa ikiwa ni pamoja na kufuatilia na kutathmini
matokeo ya Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake; kutoa mafunzo kwa wanawake
wajasiriamali kuhusu utunzaji wa kumbukumbu za biashara, jinsi ya kutumia
mikopo na kulipa, kuweka akiba na kukuza biashara; kutafuta vyanzo vingine vya
uwezeshaji wa wanawake kiuchumi na kufungua vituo vya kutolea mikopo vya Benki
ya Wanawake Tanzania katika Wilaya zote za Mikoa ya Mwanza, Dar es Salaam na
Dodoma.
Hali ya Maendeleo ya Watoto
31. Mheshimiwa
Spika, Takwimu za idadi ya watu na Makazi
nchini ya mwaka 2012 inaonyesha kuwa kwa sasa Tanzania inakadiriwa kuwa na
watoto 24,377,052 chini ya miaka 18 ambao kati yao 12,201,122 ni wasichana na
12,175,930 ni wavulana sawa na asilimia 50.1 ya Watanzania. Kundi hili linahitaji
mipango madhubuti ili kuweza kuwalea na kuwaendeleza katika nyanja za afya,
elimu, Lishe bora na ulinzi ili waweze kushiriki katika ujenzi wa Taifa.
32. Mheshimiwa
Spika, Katika kuhakikisha kwamba watoto nchini wanapata haki
yao ya ulinzi, Wizara imeendelea kuratibu shughuli za Kikosi Kazi cha Taifa cha
Kuzuia na Kupambana na Ukatili Dhidi ya watoto ambacho kinasimamia utekelezaji
wa Mpango Kazi wa Taifa wa Mwitikio na Kuzuia Ukatili Dhidi ya Watoto kuanzia
mwaka 2013 hadi 2016 kwa kushirikiana na wadau.
33. Mheshimiwa
Spika, haki ya watoto ya kushiriki ni muhimu
kwa kuwa inampa fursa ya kujadili na kutoa maoni kwa uhuru kuhusu mambo
yanayowahusu na hivyo kumjengea uwezo wa kujiamini na kujieleza. Kwa kutambua
hilo, Wizara imeendelea kuratibu shughuli za Baraza la Watoto la Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania ambapo vikao vyote vya Baraza Kuu na Kamati kuu
vilifanyika. Hadi sasa mabaraza ya watoto katika ngazi ya Mikoa yameongezeka
kutoka 12 mwaka 2005 hadi kufikia 22 mwaka 2014 na Wilaya kutoka mabaraza 57
mwaka 2005 hadi mabaraza 93 mwaka 2014.
34. Mheshimiwa
Spika, Pamoja na mafanikio niliyoyataja,
Wizara imekabiliwa na changamoto mbalimbali katika kusimamia utoaji wa haki za
watoto hapa nchini kama ifuatavyo; kuongezeka kwa vitendo vya ukatili Dhidi ya
watoto ambapo kuanzia mwaka 2000 hadi 2014 matukio 150 ya ukatili dhidi ya watu
wenye ulemavu wa ngozi yameripotiwa na kusabaisha vifo 74 ambapo asilimia 45 ni
watoto. Kushuka kwa kiwango cha ukeketaji kusikoridhisha kwa asilimia 3 kutoka
18 mwaka 1999 hadi 15 mwaka 2014. kuwepo kwa tatizo kubwa la ndoa na mimba za
utotoni ambazo zinasababisha matatizo makubwa katika maendeleo ya kielimu na
afya kwa wasichana hapa nchini. Takwimu zinaonyesha kwamba wasichana 2 kati ya
5 wanaolewa kabla hawajafikisha umri wa miaka 15. Mikoa inayoongoza kwa ndoa za
utotoni ni Mara (43%), Shinyanga (37%) na Tabora (38%). Aidha, takwimu za mwaka
2014 zinaonyesha kuwa asilimia 43 ya wasichana wanazaa kabla hawajafika umri wa
miaka 18.
35. Mheshimiwa
Spika, Ajira hatarishi kwa watoto ni tatizo
jingine ambalo limeanza kushamiri hapa nchini. Inakadiriwa kwamba asilimia 28
ya watoto hapa nchini wenye umri kati ya miaka 5 hadi 17 wanafanyishwa kazi
katika mashamba, migodi, viwanda, uvuvi na majumbani. Watoto hawa wanakosa haki
yao ya kupata elimu na baadae wanakuja kuwa wategemezi katika taifa lao. Aidha,
Idadi ya watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani imeongezeka kwa kasi hapa
nchini hasa katika majiji, miji mikubwa, mipakani na katika mikusanyiko ya
watu. Mwaka 2012 (Dogodogo Centre na Ustawi wa Jamii) takwimu zinaonyesha Jiji
la Dar es salaam ambalo lina watu zaidi ya million 5 lilikuwa na watoto
wanaofanya kazi na kuishi mitaani zaidi ya 5,000.
36. Mheshimiwa
Spika, sababu kubwa zinazochangia matatizo
haya ni uelewa mdogo wa jamii kuhusu haki za mtoto, mamlaka mbalimbali
kushindwa kuchukua hatua zinazostahili kukabiliana na matatizo punde
yanapotokea na kuendelezwa kwa mila na desturi zenye madhara katika jamii yetu.
Wizara yangu imepanga mambo yafuatayo kukabiliana na changamoto hizi: Kudurusu
Sera ya Mtoto ya 2008 kwa kuingiza masuala ya Malezi, makuzi na maendeleo ya
Awali ya Mtoto katika kuimarisha misingi ya malezi ya watoto hasa katika umri
mdogo; Kuimarisha mikakati ya ulinzi wa mtoto na kuboresha uratibu wa masuala
ya watoto. Aidha, jamii itaendelea kuhamasishwa kutoa taarifa za vitendo vya
ukatili kwa vyombo vya ulinzi na usalama. Sera hii ikikamilika italeta
uwajibikaji shirikishi kwa sekta na wadau wote katika malezi ya watoto.
Hali ya Mashirika Yasiyo ya
Kiserikali
37. Mheshimiwa
Spika, Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya
Kiserikali ya mwaka 2001 na Sheria ya NGOs Na. 24 ya mwaka 2002 kama
ilivyorekebishwa mwaka 2005 zimechangia kuimarisha hali ya Mashirika Yasiyo ya
Kiserikali hapa nchini. Lengo kuu la Sera hii ni kujenga mazingira wezeshi kwa
ajili ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kushiriki kikamilifu na kuchagia kwa
ufanisi katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Aidha, Sheria ya NGOs ilitungwa
ili kuupa utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nguvu
ya kisheria.
38. Mheshimiwa
Spika, kutokana na utekelezaji wa sera na
sheria hiyo, idadi ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali imeongezeka kutoka 3000
iliyokadiriwa kwa mujibu wa Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya
mwaka 2001 hadi kufikia 7,060 mwezi Machi, 2015. Kati ya mashirika hayo, 277 ni
ya kimataifa na mashirika 6,783 ni ya ndani ya nchi yanayofanya kazi katika
ngazi ya wilaya, mkoa na taifa. Aidha, Wizara ilifuta usajili wa NGOs 24, kati
ya hizo, NGOs 10 ziliomba kuondolewa kwenye rejista ya NGOs baada ya kukamilika
kwa miradi na programu zao. Utekelezaji huo upo kwa mujibu wa Sheria ya
Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ambayo inampa Msajili wa NGOs mamlaka ya kuyafutia
usajili mashirika ambayo yanakiuka masharti ya usajili wao au pale mashirika
husika yanapoomba kuondolewa kwenye rejista ya usajili kutokana na sababu
mbalimbali.
39. Mheshimiwa
Spika, mchango wa Mashirika Yasiyo ya
Kiserikali katika kutoa huduma kwa jamii katika masuala mbalimbali umeendelea
kuimarika. Mchango huo unaonekana zaidi katika sekta na maeneo ya elimu, afya,
maji, maendeleo ya jinsia, maendeleo shirikishi, mazingira, ustawi wa jamii,
kilimo, utawala bora, haki za binadamu, huduma za sheria na ujasiriamali.
Mfano, Shirika la CCBRT liliwezesha matibabu ya akina mama 868 wenye tatizo la
fistula katika Hospitali za Seliani (Arusha), KCMC (Kilimanjaro) na CCBRT
(Makao Makuu Dar es Salaam). Aidha, wanawake hao baada ya kupona walipatiwa
ujuzi mbalimbali kupitia mafunzo yatolewayo na Kituo cha Mabinti kilichopo Dar
es Salaam ili kuwawezesha wanawake hao kujitegemea kiuchumi.
40. Mheshimiwa
Spika, Mashirika Yasiyo ya Kiserikali pia
yameendelea kukuza fursa za ajira kwa kuhimiza na kutekeleza vyema dhana ya
kujitolea. Taarifa ya mwaka 2012 ya Wizara kuhusu mchango wa Mashirika Yasiyo
ya Kiserikali katika maendeleo inaonesha kuwa, mashirika haya yaliajiri jumla
ya watu 60,700 ambapo kati yao, watu 27,312 wanafanyakazi kwa kujitolea.
41. Mheshimiwa
Spika, pamoja na uwepo wa michango mingi na
mizuri ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika utekelezaji wa mipango na
program mbalimbali za nchi ikiwemo Dira ya Taifa ya Maendeleo (2025), MKUKUTA I
na II, bado kuna changamoto mbalimbali zinazohitaji kufanyiwa kazi. Baadhi ya
changamoto hizo ni pamoja na Mashirika mengi Yasiyo ya Kiserikali kujikita
zaidi mijini badala ya vijijini ambapo kuna wananchi wengi wenye kuhitaji
huduma zao na kuendelea kutegemea ufadhili wa nje katika kutekeleza shughuli
zao ambapo masharti ya ufadhili huo yanapelekea baadhi ya mashirika haya
kukiuka mila, desturi, taratibu na sheria mbalimbali za nchi.
42. Mheshimiwa
Spika, katika kutatua changamoto hizo, hatua
mbalimbali zimechukuliwa ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa NGOs kuhusu umuhimu
wa taasisi hizi kuwafikia wadau wengi zaidi nchini hususan vijijini. Jitihada
hizi zimefanyika kupitia Ofisi za Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali,
mikutano kati ya wadau wa mashirika haya na Bodi ya Uratibu wa Mashirika Yasiyo
ya Kiserikali nchini pamoja na Wasajili Wasaidizi wa ngazi ya Wilaya na Mikoa.
Aidha, Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yameendelea kuhimizwa kutumia fursa ya
marekebisho ya Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya mwaka 2005 kwa
kuanzisha miradi ya kujipatia kipato kitakachoyawezesha kuepukana na utegemezi
uliokithiri kwa wafadhili wa nje katika kuwahudumia walengwa wao.
D: MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO
WA MWAKA 2014/15 NA MALENGO YA MWAKA 2015/16.
Sekta ya Maendeleo ya Jamii
43. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2014/15, Wizara yangu
iliendelea kusimamia utekelezaji wa majukumu yake kulingana na malengo na
shabaha zilizopangwa. Katika bajeti ya mwaka huo, Wizara ilikisia kukusanya
jumla ya Sh.1,845,360,000 kutoka vyanzo mbalimbali. Hadi Machi 2015, makusanyo
yalifikia Sh. 1,815,145,600 sawa na asilimia 98.4 ya lengo.
Aidha, Wizara iliidhinishiwa jumla ya Sh. 29,453,599,000 ambapo kati ya
hizo, Matumizi ya Kawaida ni Sh. 20,526,055,000 yakijumuisha Sh.
12,818,434,000 kwa ajili ya mishahara na Sh. 7,707,621,000 kwa ajili
ya Matumizi Mengineyo. Bajeti ya Matumizi ya Miradi ya Maendeleo
iliyoidhinishwa ni Sh. 8,927,544,000
44. Mheshimiwa
Spika, hadi kufikia Aprili, 2015, Wizara
ilikuwa imepokea jumla ya Sh. 8,639,231,903 sawa na 67% ya Bajeti ya Mishahara iliyoidhinishwa
na matumizi yakiwa Sh.8,639,231,903 sawa na 100% ya fedha za Mishahara
zilizotolewa, fedha za Matumizi Mengineyo Sh. 3,260,825,060 ikiwa ni 42% ya
fedha za matumizi mengineyo zilizopokelewa na Sh. 3,260,825,000 sawa na 100% ya
fedha zilizotolewa zimetumika. Aidha, fedha za ndani za maendeleo
Sh.1,700,000,000 zilitolewa sawa na 25% ya fedha zilizoidhinishwa na Sh.
338,634,000 sawa na 17% ya fedha za nje zilitolewa ambapo Sh. 1,450,000,000
sawa na 85% ya fedha za ndani zilizotolewa na Sh.338,634,000 sawa na 100% ya
fedha za nje zilizotolewa zilitumika.
45. Mheshimiwa
Spika, Wizara yangu inatambua mchango wa
Wataalam wa Maendeleo ya jamii katika kusaidia jamii ili ziweze kujiletea
maendeleo. Katika mwaka 2015/16, Wizara yangu itaendelea kuwajengea uwezo
Maafisa Maendeleo ya Jamii ngazi ya Mkoa na Halmashauri za Wilaya kuhusu mbinu
shirikishi jamii, utatuzi wa migogoro ya kijamii na mbinu za ujasiriamali ili
kuboresha utendaji kazi wa wataalam hawa waweze kutekeleza majukumu yao kwa
ufanisi zaidi.
Vyuo vya Maendeleo ya Jamii
46. Mheshimiwa
Spika, Wizara imeendelea kutoa mafunzo ya
Taaluma ya Maendeleo ya Jamii katika ngazi ya Astashahada ambapo jumla ya
wanachuo 1,885 walidahiliwa katika mwaka 2014/15, ambapo kati yao wanaume 758
na wanawake ni 1,128, Stashahada ni 1,430 wakiwemo wanaume 378 na wanawake1,052
kwa Vyuo nane vya Maendeleo ya Jamii ambavyo ni Buhare, Rungemba, Missungwi,
Monduli, Uyole, Ruaha, Mlale na Mabughai. Aidha, Taasisi ya Maendeleo ya Jamii
Tengeru wanachuo 276 walidahiliwa katika ngazi ya Shahada ambapo wanaume
walikuwa 87 na wanawake 189. Hali kadhalika wanachuo watatu (3) walidahiliwa
katika ngazi ya Stashahada ya Uzamili kati yao kulikuwa na mwanume mmoja (1) na
wanawake wawili (2).
47. Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka 2015/16, Wizara
itaendelea kudahili na kutoa mafunzo kuanzia ngazi ya Astashahada hadi
Stashahada ya Uzamili. Mafunzo haya yanahusu misingi ya maendeleo ya jamii,
mipango shirikishi, ubunifu na uandishi wa miradi, mbinu za uongozi na utawala,
mbinu za kuendesha biashara, uchambuzi na upangaji wa masoko. Lengo la mafunzo
hayo ni kutoa elimu, ujuzi na mbinu mbalimbali zitakazowasaidia wataalam wa
Maendeleo ya Jamii kutekeleza dhana ya maendeleo ya jamii kwa vitendo katika
jamii kwa kuwawezesha watu kutambua uwezo walio nao wa kubaini matatizo na
uwezo wao wa kutumia raslimali zilizopo ili kuongeza kipato na kupunguza
umaskini. Aidha, Wizara itaendelea kukamilisha jengo la maktaba katika Chuo cha
Tengeru, ujenzi wa uzio katika Chuo cha Rungemba na Ruaha, kujenga jengo la
utawala, jengo la maktaba, ukumbi wa mikutano, nyumba za watumishi katika Chuo
cha Uyole, kukarabati majengo na miundombinu katika Vyuo vya Buhare, Mlale,
Ruaha, Mabughai, Missungwi na Monduli ili kuboresha mazingira ya kufundishia na
kujifunzia.
Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi
48. Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka 2014/15, Vyuo vitano vya
Maendeleo ya Wananchi vya Sofi, Mputa, Kilwa Masoko, Tarime na Mwanhala
vilifanyiwa ukarabati mkubwa na mdogo wa madarasa, mabweni, majengo ya utawala,
ujenzi wa vyoo, mabwalo ya kulia chakula, miundombinu ya mifumo ya umeme, maji
safi na maji taka. Aidha, Vyuo vya Nandembo, Sengerema na Chala vilipewa magari
ili yatumike kwa usafiri na kutolea mafunzo kwa vitendo. Katika mwaka wa fedha
wa 2015/16, Wizara itaendelea kuboresha maeneo ya kutolea mafunzo kwa kujenga madarasa,
nyumba za watumishi na majengo ya utawala katika vyuo vya: Ilula na Newala,
kuweka mfumo wa umeme katika vyuo vya Munguri, Ulembwe, Rubondo, Msingi, Malya
na Mwanhala na kugharamia upimaji na upatikanaji wa Hati Miliki wa vyuo vya:
Ifakara, Ikwiriri, Msingi, Mwanva, Musoma, Arnautoglu, Chilala, Kilwa Masoko,
Chisalu na Kisarawe kwa lengo la kupunguza migogoro inayosababishwa na wananchi
kuvamia maeneo ya vyuo kwa shughuli za kilimo na ujenzi wa makazi. Wizara
itaendelea kujenga na kufanya ukarabati wa majengo na miundombinu kwa awamu
kadri fedha zinavyotengwa kwa ajili ya kazi hizi zitakavyopatikana kutoka
Hazina.
Maendeleo ya Jinsia
49. Mheshimiwa
Spika, Wizara imeendelea kushiriki na
kutekeleza mikataba na maazimio mbalimbali ya kikanda na kimataifa ambayo nchi
imeridhia, Wizara ilishiriki katika mkutano wa‘’ African Regional Conference’’
uliofanyika tarehe 17-19 Novemba, 2014 Addis Ababa - Ethiopia. Mkutano huo
ulilenga kupitia taarifa ya nchi ya Beijing+20 na kutoa maazimio ya utekelezaji
wa maeneo 12 yaliyoanishwa. Taarifa hiyo iliwasilishwa katika kikao cha 59 cha
Kamisheni ya Hali ya Wanawake ambacho kilifanyika nchini Marekani Machi, 2015.
Aidha, mkutano huo ulitoa fursa kwa
washiriki kujadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya wanawake na haki
za wasichana na kutoa mapendekezo ya kiutekelezaji katika kufikia usawa wa
kijinsia. Katika mwaka 2015/16, Wizara itaendelea kushiriki katika utekelezaji
wa mikataba ya kikanda na kimataifa ikiwa ni pamoja na kutoa michango na uzoefu
wake katika kuboresha na kuimarisha usawa wa jinsia na uwezeshaji wa wanawake
pamoja na kushiriki mikutano mbalimbali.
50. Mheshimiwa
Spika, Ili kufikia lengo la kuwepo kwa usawa
wa jinsia, uingizwaji wa masuala ya jinsia katika mipango, mikakati, bajeti,
sera na programu mbalimbali bado unaendelea kutiliwa mkazo. Katika kipindi cha
mwaka 2014/15, Wizara iliendesha mafunzo ya ukusanyaji wa takwimu
zilizochambuliwa kijinsia kwa maafisa 50 kutoka Wizara mbalimbali, Taasisi
zisizo za serikali na Taasisi za Elimu. Mafunzo hayo yaliwezesha ukusanyaji
wa takwimu zilizochambuliwa kijinsia
na hivyo kuweza kukamilisha Taarifa ya Hali ya Jinsia Nchini (Tanzania Country
Gender Profile - TCGP). Taarifa hizo zitatumiwa na serikali pamoja na wadau
mbalimbali katika kufanya maamuzi, ushawishi, utungaji sera na mipango
mbalimbali ya maendeleo kwa kuzingatia usawa wa jinsia. Aidha, Wizara
itaendelea kutoa mafunzo kwa ngazi mbalimbali za uongozi ili kujenga uelewa wa
pamoja kuhusu uingizwaji wa masuala ya jinsia, uboreshaji wa Taarifa ya Hali ya
Jinsia Nchini pamoja na usambazaji wa taarifa hiyo.
51. Mheshimiwa
Spika, Wizara kupitia vikao vya robo mwaka
vya kikundi cha uingizaji wa masuala ya kijinsia katika Sera za Kitaifa na
Kisekta (Gender Mainstreaming Working Group for Macro Policies) imeweza kuandaa
Mwongozo wa Uingizaji wa Masuala ya Jinsia katika Mpango wa Matokeo Makubwa
Sasa (Big Results Now - BRN). Lengo ni kuwezesha kuwepo kwa matokeo makubwa kwa
kuzingatia mahitaji ya makundi yote ya wanawake na wanaume. Mwaka 2015/16,
Wizara itaendelea kuratibu uingizwaji wa masuala ya jinsia katika Sera za
Kitaifa pamoja na kujenga uwezo kuhusu uingizwaji wa masuala ya kijinsia.
52. Mheshimiwa
Spika, Benki ya Wanawake Tanzania (TWB)
ambayo ni mali ya umma inayomilikiwa kwa kiasi kikubwa na Serikali ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania na kufikia mwaka 2014/15, Benki ina wanahisa
wadogowadogo wanaokadiriwa kufikia 160 wanaomiliki hisa zisizozidi asilimia 2.
Katika mwaka, 2014/15, Benki ilitoa mikopo kwa wajasiriamali wapatao 10,847. Kati
ya idadi hiyo wanawake ni 8,135 sawa na asilimia 75 ya wateja wote waliopatiwa
mikopo. Thamani ya mikopo iliyotolewa ni kiasi cha Sh. 12,469,650,000. Kati ya
kiasi hicho, jumla ya Sh. 8,561,200,000 zilikopeshwa kwa wanawake, sawa na
asilimia 69 ya mikopo iliyotolewa. Benki imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya
mtaji kwa kutafuta fursa mbalimbali za kupata fedha za kujiendesha na kutanua
mtaji wake.
53. Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka 2015/16, benki
inatarajia kuendelea kutoa huduma zake katika maeneo mengi zaidi kupitia njia
ya wakala wa benki (Agency Banking) na kufungua ofisi za kutolea huduma za
mikopo mikoani. Aidha, katika mwaka wa kibenki wa 2014, Benki ya Wanawake
imetengeneza faida ya shilingi milioni 141 kabla ya kodi (Profit Before Tax).
Menejimenti na Bodi ya Wakurugenzi wa benki wanaona mwaka 2015 ni kipindi
mwafaka cha kuanza mchakato rasmi wa kuuza hisa ili kukuza mtaji wa benki na
kuiwezesha Benki kujiendesha na kupanua wigo wa huduma pasipo kutegemea mtaji
kutoka Serikalini.
54. Mheshimiwa
Spika, kwa mwaka 2014/15, Mfuko wa Wanawake umetoa jumla ya Sh.
31,000,000 kwa Halmashauri tatu ambazo ni Bunda, Iringa pamoja Mkalama. Aidha,
Wizara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeadhimisha Siku ya Wanawake
Duniani iliyofanyika Mkoani Morogoro katika Uwanja wa Jamuhuri na Mgeni Rasmi
alikuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho
Kikwete. Kaulimbiu ya siku hiyo ilikuwa ‘’Uwezeshaji Wanawake; Tekeleza
Wakati ni Sasa’. Aidha, siku ya Maadhimisho shughuli mbalimbali zilifanyika
ikiwemo maonyesho ya biashara kutoka Wizara mbalimbali, vikundi vya wanawake
Wajasilimali pamoja na wadau wa maendeleo.
Maendeleo ya Watoto
55. Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka 2014/15, Wizara iliandaa Mpango Kazi wa
Taifa wa Miaka Mitano wa Ushiriki wa Watoto (2014-2019). Lengo la Mpango Kazi
huo likiwa ni kuongeza ushiriki wa watoto katika masuala mbalimbali
yanayowahusu. Katika mwaka 2015/16, Wizara itaendelea kusambaza mpango kazi huu
katika Halmashauri za Wilaya.
56. Mheshimiwa
Spika, Wizara imekamilisha uandaaji wa
rasimu ya Sera ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Mtoto pamoja na Mkakati wake
wa Utekelezaji. Sera hii ipo katika ngazi za juu za maamuzi kwa ajili ya
kupitishwa. Sera imeandaliwa mahsusi ili kuhakikisha uwepo wa mfumo
fungamanishi na shirikishi wa utoaji huduma za Malezi Makuzi na Maendeleo ya
Awali ya Mtoto. Katika mwaka 2015/16, Wizara inataraji kukamilisha mchakato na
kutoa nakala 3,000 za sera hiyo pamoja na mkakati wake wa utekelezaji na
kusambaza kwa wadau kwa ajili ya utekelezaji.
57. Mheshimiwa
Spika, Wizara iliendelea kuratibu utoaji wa
taarifa zinazohusu vitendo vya ukatili dhidi ya watoto kwa kushirikiana na
Asasi isiyokuwa ya Kiserkali ya C-SEMA ambapo kati ya mwezi Julai, 2014 na
Machi, 2015 jumla ya simu 21,960 zilipigwa kupitia mtandao wa simu namba 116.
Taarifa hizo zilishughulikiwa kulingana na aina ya tatizo/suala
lililowasilishwa. Katika mwaka 2015/16, Wizara itaendelea kuratibu utoaji wa
huduma hii kwa kushirikiana na asasi husika.
58. Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka 2014/15, Wizara
iliratibu maandalizi ya taarifa ya kujibu hoja mbalimbali zilizotolewa na
Kamati ya Haki za Watoto ya Umoja wa Mataifa kuhusu ripoti ya nchi ya 3, 4 na 5
ziliyowasilishwa katika kamati hiyo mnamo mwezi Januari, 2012 na kuwasilisha
majibu ya hoja kwenye kamati hiyo mwaka 2015. Katika mwaka 2015/16, Wizara
itaendelea kuyafanyia kazi maoni ya jumla ‘’Concluding Observation’’
yaliyotolewa na Kamati hiyo ya Haki za Watoto ya Umoja wa Mataifa.
59. Mheshimiwa
Spika, Mwaka 2014/15, Wizara yangu ilizindua rasmi Zana za
Mawasiliano kwa ajili ya kuzuia ukatili dhidi ya watoto yenye lengo la
kuelimisha wazazi, watoto, wanahabari na wanajamii jinsi ya kujizuia na kutoa
taarifa kuhusu matukio mbalimbali ya ukatili dhidi ya mtoto ambapo nakala 1,000
za zana hizo zilisambazwa kwa wadau wa masuala ya ulinzi na haki za watoto hapa
nchini. Katika mwaka wa fedha 2015/16, Wizara itasambaza nakala 2,000 za zana
hizo na kuratibu utekelezaji wake.
60. Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka 2014/15, Wizara yangu
imeratibu Maadhimisho ya Siku ya Familia Duniani ambayo huadhimishwa kila mwaka
tarehe 16 Juni na mwaka huu yameadhimishwa katika ngazi ya Mkoa. Kaulimbiu ya
mwaka 2015 ni “Usawa wa Kijinsia na Haki za Watoto katika Familia: Wanaume
Wawajibike’’
Kaulimbiu hii inaelekeza umuhimu wa
wanaume katika kutambua na kuheshimu usawa wa kijinsia katika jamii zetu.
Kuachana na mfumo dume ndani ya jamii kutompa fursa mwanamke/msichana kupata
maendeleo ya kiuchumi, kisiasa, kielimu, afya na kiutamaduni.
Aidha, Wizara imeratibu maandalizi ya
Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika ambayo kila mwaka yanaadhimishwa tarehe
15 Mei. Kaulimbiu ya mwaka 2015 ni “Tokomeza Mimba na Ndoa za Utotoni: Kwa Pamoja
Tunaweza”. Kaulimbiu hii inatukumbusha sisi
wadau wa maendeleo ya watoto pamoja na wananchi jukumu letu katika kuwalinda
watoto dhidi ya ndoa na mimba za utotoni, ambazo zina athari kubwa katika
maendeleo ya elimu na afya ya mtoto. Aidha, kuachana na kupiga vita mila na
desturi zenye athari katika jamii zetu ndio silaha pekee katika kukabiliana na
tatizo la mimba na ndoa za utotoni.
Mashirika Yasiyo ya Kiserikali
61. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2014/15, Wizara yangu iliendelea kusajili
NGOs ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya
mwaka 2001 pamoja na Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Na. 24/2002
iliyorekebishwa mwaka 2005. Hadi kufikia Mwezi Machi, 2015 jumla ya mashirika
7,060 yalipatiwa usajili katika ngazi mbalimbali ili kuyawezesha kutambulika
kisheria na kutekeleza malengo yaliyokusudiwa. Katika kipindi cha mwaka
2015/16, Wizara itaendelea na usajili wa Mashirika hayo.
62. Mheshimiwa
Spika, mwaka 2014/15, Wizara yangu ilichukua
hatua mbalimbali za kuimarisha uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali
nchini. Hatua hizi ni pamoja na: kuendelea kuliwezesha Baraza la Taifa la NGOs
kutekeleza majukumu yake ya kisheria kwa kupitisha Kanuni za Uendeshaji wake na
Kanuni za Chaguzi za Baraza hilo za ngazi mbalimbali. Kanuni hizi zitaliwezesha
Baraza na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa ujumla kujiendesha kwa ufanisi
zaidi kwa kujidhibiti ili kuimarisha taswira na mchango wao katika jamii.
63. Mheshimiwa
Spika, hatua nyingine iliyochukuliwa katika
uratibu wa NGOs ni kukuza ubia baina ya Serikali na Mashirika Yasiyo ya
Kiserikali kwa kuingia makubaliano ya kufanya kazi kwa pamoja na NGOs 20
zinazojihusisha na maendeleo ya wanawake na watoto. Aidha, Wizara iliendelea
kuhamasisha ubia baina ya mashirika haya na Taasisi nyingine za Serikali
zikiwemo Mamlaka za Serikali za Mitaa. Pia, Wizara yangu iliboresha Benki ya
Taarifa na Takwimu za NGOs kwa kuingiza masuala ya jinsia. Taarifa na takwimu
hizi zinatumiwa na wadau katika kufikia maamuzi mbalimbali ya kimaendeleo.
Katika mwaka 2015/16, Wizara itaendelea kuratibu na kufuatilia shughuli za NGOs
kwa lengo la kuendelea kujenga mazingira wezeshi ya NGOs katika kushiriki na
kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.
Uhamasishaji, Uelimishaji na
Ushawishi
64. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2014/15, Wizara yangu
iliandaa vipindi vya luninga na redio, matangazo kupitia magazeti, vipeperushi
na mabango, mikutano ya waandishi wa habari kwa ajili ya kuelimisha umma kuhusu
masuala ya maendeleo ya jamii, jinsia, wanawake, familia, haki za watoto na
uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Aidha, kwa kushirikiana na UNICEF,
Wizara yangu imeandaa kipindi maalum cha ‘WALINDE WATOTO’ ambacho kinatangazwa kupitia
redio 14 zenye usikivu wa kitaifa na kikanda Tanzania Bara na Zanzibar. Lengo
la kipindi ni kuhamasisha wadau wa maendeleo ya mtoto kushiriki kikamilifu
katika jitihada za kuzuia na kutokomeza ukatili dhidi ya watoto nchini. Katika
mwaka 2015/16 Wizara itaendelea kuhamasisha, kuelimisha na kushawishi umma
kuhusu masuala ya maendeleo ya jamii, jinsia, wanawake, familia, haki za watoto
na uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.
Uratibu wa Sera, Programu na Mipango ya Wizara.
65. Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka
2014/15, Wizara yangu imeandaa Andiko la Programu ya Maendeleo ya Elimu ya
Wananchi lenye awamu mbili za utekelezaji kwa vipindi vya miaka mitano mitano
zilizohuishwa na Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano awamu ya pili na
ya tatu. Aidha, programu hiyo ni sehemu ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya
Elimu na rasimu yake imewasilishwa na kupitishwa katika vikao vya sekta ya
Elimu. Programu inalenga kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia,
utoaji wa ujuzi na stadi mbalimbali na elimu ya ujasiriamali zitakazowezesha
vijana na wananchi kupata fursa za kuongeza vipato vyao kwa kujiajiri au
kuajiriwa na hivyo kuchangia katika kutekeleza malengo ya Dira ya Taifa 2025. Kwa
mfano, kuzalisha mafundi mchundo watakaotumika katika fursa iliyopo ya uchumi
wa gesi na mafuta katika jamii.
Aidha, Wizara inaandaa maandiko ya Programu ya Kuwezesha
Wanawake na Wasichana Kiuchumi, Programu ya Kutokomeza Ndoa za Utotoni na
Programu ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto kama sehemu ya
kutekeleza Agenda ya Maendeleo ya Afrika 2063 kwa kuanza kutoa msukumo
maalum wa kuwaendeleza wanawake na watoto. Katika mwaka 2015/16, Wizara
itaendelea kuratibu utafutaji wa fedha kutoka vyanzo mbalimbali ili kutekeleza
programu hizo.
66. Mheshimiwa Spika, Wizara yangu iliandaa Mwongozo wa Ufuatiliaji na
Tathmini utakaotumika kufuatilia utekelezaji wa sera, mikakati, mipango na
mikataba ya kikanda na kimataifa iliyoridhiwa. Katika mwaka 2015/16, Wizara
itawezesha upatikanaji wa taarifa za msingi kulingana na mfumo wa ufuatiliaji
na tathmini ulioandaliwa. Aidha, itawajengea uwezo Maafisa 25 wa Maendeleo ya
Jamii wa Mikoa kuhusu ukusanyaji, uchakataji, uchambuzi na uandaaji wa taarifa
za utekelezaji wa sera za Wizara.
67. Mheshimiwa
Spika, Wizara
imeendelea kusimamia maendeleo ya Sera na Programu za Sekta ya Maendeleo ya
Jamii. Katika mwaka 2015/16, Wizara itafanya tathmini kuhusu ufanisi wa Sera ya
Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ili kubaini changamoto na mafanikio
yaliyopatikana. Aidha, matokeo ya tathmini yatatumika kurekebisha sera iliyopo
ili kuweka mazingira wezeshi kwa NGOs na kuziwezesha kushiriki kikamilifu
katika kuleta maendeleo kwa wananchi.
Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu
68. Mheshimiwa
Spika, Wizara yangu
imeendelea kutoa huduma za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu kwa madhumuni
ya kuboresha utendaji kazi kwa kuzingatia misingi ya haki, usawa, uadilifu,
utawala bora na uwazi kwa lengo la kuongeza tija na ufanisi katika kazi. Wizara
imeendelea kuweka mkazo katika kudhibiti vitendo vya rushwa na uzembe kazini
ili kuwa na watumishi waadilifu na wawajibikaji, wenye ari, moyo na msimamo
thabiti katika utekelezaji wa majukumu katika utumishi wa Umma. Aidha, kwa mwaka
wa fedha 2015/16, Wizara itaendelea kutoa huduma za kiutawala na usimamizi wa
rasilimaliwatu kwa kuzingatia misingi ya haki, usawa, uadilifu na utawala bora.
69. Mheshimiwa
Spika, Ili kuwawezesha
watumishi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, Wizara imewawezesha watumishi
kuhudhuria mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu ndani na nje ya nchi. Kwa mwaka
2014/15, watumishi 64 wamewezeshwa kupata mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi
ndani na nje ya nchi. Katika mwaka 2015/16, Wizara itaendelea kuwajengea uwezo
watumishi kwa kuwapatia mafunzo ya kuongeza weledi na ufanisi wa kazi za
utumishi wa umma.
70. Mheshimiwa
Spika, Mwaka 2014/15,
Wizara imeendelea kutoa motisha kwa watumishi kwa kuwapandisha vyeo jumla ya
watumishi 156, kuwabadilisha kada watumishi 2 na kuwathibitisha kazini
watumishi 38 wa kada mbalimbali. Katika mwaka 2015/16, Wizara inatarajia
kuwabadilisha kada watumishi 15, kuwapandisha vyeo watumishi 355 na kati yao
watumishi 105 ni wa kada ya ualimu.
71. Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa
fedha 2014/15, Wizara yangu imeendelea kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa
kufanya ukarabati na uboreshaji wa baadhi ya maeneo ya ofisi ( Makao Makuu)
kama vile ujenzi wa eneo la kuegesha magari, ununuzi wa jenereta, uboreshaji wa
masijala pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya umeme, simu na Internet.
Kwa mwaka wa fedha 2015/16, Wizara itaendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa
kuendelea kufanya ukarabati mdogomdogo katika jengo la Wizara Makao makuu.
72. Mheshimiwa
Spika, Kwa mwaka 2014/15,
Wizara imeajiri watumishi wapya wa kada mbalimbali wapatao 148 na kufanya
Wizara kuwa na watumishi 1,122. Nafasi 428 zimekwisha tangazwa na Sekretarieti
ya Ajira,
hivyo mchakato
utakapo kamilika watumishi hao pia wataajiriwa. Hata hivyo, Wizara bado
inakabiliwa na upungufu mkubwa wa watumishi hasa wa kada ya ukufunzi katika
Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi na vya Maendeleo ya Jamii. Katika kukabiliana na
changamoto hizo, Wizara imepeleka maombi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi
wa Umma kwa ajili ya kupata kibali cha kuajiri watumishi wa kada mbalimbali.
Kwa mwaka 2015/16, Wizara itaendelea kuomba kibali cha kuajiri watumishi ili
kupunguza pengo lililopo.
73. Mheshimiwa
Spika, katika kupambana
na janga la UKIMWI na magonjwa yasiyo ya kuambukiza kama vile kisukari na
magonjwa ya moyo, mwaka 2014/15 Wizara imewawezesha watumishi 154 kupata
mafunzo, ushauri nasaha pamoja na huduma ya upimaji afya kwa hiari. Wizara
imeendelea kuhamasisha watumishi kupima afya zao kwa kutumia utaratibu wa
kuwaleta wataalamu wa huduma za afya kwa ajili ya ushauri nasaha, upimaji wa
hiari na kuwapatia watumishi wanaoishi na virusi vya UKIMWI huduma ya lishe.
Kwa kutambua umuhimu wa michezo katika kuimarisha afya za watumishi, kwa mwaka
2014/15, Wizara iliwawezesha watumishi kushiriki katika mashindano ya SHIMIWI.
Kwa mwaka wa fedha 2015/16, Wizara itaendelea kuhamasisha upimaji wa afya ikiwa
ni pamoja na kutoa huduma stahiki na kuendelea kuhamasisha watumishi kushiriki
katika michezo.
74. Mheshimiwa
Spika, Kutokana na
umuhimu wa kushirikisha watumishi kuboresha utendaji kazi, utekelezaji wa
majukumu ya Wizara na kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiutendaji,
Wizara imeweza kufanya Mkutano mmoja wa Baraza la Wafanyakazi kwa mwaka
2014/15. Kwa mwaka 2015/16, Wizara itaendelea kuhakikisha Mikutano ya Baraza la
Wafanyakazi inafanyika.
E: HITIMISHO
75. Mheshimiwa
Spika, Majukumu ya
Wizara yangu ni kuhakikisha jamii na wananchi wanabadilika kifikra na kimtizamo
ili kuwa na jamii inayoshiriki kikamilifu katika kujiletea maendeleo yao
wenyewe na Taifa kwa ujumla. Majukumu haya ni mtambuka, hivyo basi utekelezaji
wa Malengo na Mipango ya Wizara kwa mwaka 2015/16, bado utahitaji ushirikiano
mkubwa zaidi wa wadau mbalimbali hasa Mikoa na Halmashauri.
F: SHUKRANI
76. Mheshimiwa
Spika, Napenda sasa
kumshukuru sana Naibu Waziri, Mhe. Dkt. Pindi Hazara Chana (Mb.), kwa
ushirikiano mkubwa anaonipa katika kuongoza Wizara hii. Vilevile, napenda kutoa
shukrani za dhati kwa: Katibu Mkuu, Bibi Anna Tayari Maembe, Naibu Katibu Mkuu,
Bibi Nuru H. M. Millao; Wakurugenzi; Wakuu wa Vitengo; Mkurugenzi Mtendaji wa
Benki ya Wanawake Tanzania - Bibi Magreth Chacha; Wakuu wa Vyuo; na Wafanyakazi
wote wa Wizara yangu wa ngazi zote, kwa jitihada zao katika utekelezaji wa
majukumu ya Wizara ambayo ni pamoja na kuniwezesha mimi kuwasilisha hotuba hii
mbele ya Bunge lako tukufu.
77. Mheshimiwa
Spika, Napenda
kumalizia hotuba yangu kwa kuwashukuru wadau wote tunaofanya nao kazi na
kushirikiana kwa namna moja au nyingine. Peke yetu kama Wizara tusingefikia
mafanikio niliyoyataja. Naomba kupitia Bunge lako tukufu, kutoa shukrani zangu
za dhati kwa wafuatao: Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Asasi ya Wanawake
na Maendeleo (WAMA); Mfuko wa Fursa Sawa kwa Wote (EOTF); Mtandao wa Jinsia
Tanzania (TGNP); Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA); Chama cha
Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA); Shirikisho la Vyama vya Wanawake
Wafanyabiashara Tanzania (FAWETA); Medical Women Association of Tanzania (MEWATA);
White Ribon; Plan International; Save the Children na
Mashirika mengine mbalimbali Yasiyo ya Kiserikali pamoja na wale wanaofanya
kazi kwa maslahi ya jamii kwa namna moja au nyingine.
78. Mheshimiwa Spika, Napenda pia kuyashukuru Mashirika kutoka nchi rafiki
ambayo yameendelea kutusaidia na kufanya kazi na sisi. Mashirika hayo ni pamoja
na: GPE; KOICA na UK Education. Aidha, nayashukuru Mashirika ya Umoja wa
Mataifa ambayo ni: UNICEF; UNDP; UNFPA na UN WOMEN kwa misaada yao mbalimbali
iliyofanikisha utekelezaji wa majukumu mengi ya Wizara yangu.
G: MAKADIRIO YA
BAJETI YA WIZARA KWA MWAKA 2015/16
79. Mheshimiwa
Spika, Ili Wizara yangu
iweze kutekeleza majukumu na malengo yake kwa mwaka 2015/16, sasa naliomba
Bunge lako tukufu liidhinishe matumizi ya shilingi 31,421,641,000. Kati
ya fedha hizo,
(a) Shilingi 11,038,075,000 ni kwa
ajili ya Mishahara
(b) Shilingi 9,460,146,000 ni kwa
ajili ya Matumizi Mengineyo
(c) Shilingi 10,923,420,000 ni kwa
ajili ya kutekeleza Miradi ya Maendeleo ambapo Shilingi 8,000,000,000 ni
fedha za ndani na Shilingi 2,923,420,000 ni fedha za nje.
80. Mheshimiwa
Spika, naomba
kutoa hoja.


No comments:
Post a Comment