TANGAZO


Saturday, March 7, 2015

Viongozi wa Dini waaswa kuhubiri amani na utulivu kuelekea mchakato wa Katiba Mpya

Mkuu wa Wilaya ya Mjini Magharibi Bw.Ayoub Mohamed Mahmoud akiongea na Viongozi mbalimbali wa Dini na kuwataka kuhubiri amani na utulivu hasa katika kipindi hiki cha kuelekea upigaji kura ya maonikwa  Katiba Inayopendekezwa pamoja uchaguzi Mkuu. 
Mwenyekiti wa Kamati ya Amani na utulivu Tanzania Sheikh Noman Thabit Jongo akiwaeleza viongozi wa Dini mbalimbali suala la amani na utulivu katika kuelekea katika kuipigia kura ya maoni Katiba Inyopendekezwa na kuwaasa kuwaelimisha waumini wao juu ya ubora wa Katiba Inayopendekezwa kwani imegusa makundi yote katika Jamii. 
Mbunge wa WAWI kupitia chama cha wananchi CUF Mh. Hamad Rashid Mohamed akiongea na viongozi wa Dini mbalimbali na kuwaasa kuisoma, kuielewa Katiba Inayopendekezwa na kuacha kupotoshwa kwa kusomewa vipengele vya Katiba hiyo bila kupewa ufafanuzi, wakati wa mkutano ulioratibiwa na Kamati ya Amani na Utulivu Tanzania kushirikisha viongozi wa Dini leo Zanzibar. 
Mwenyekiti wa Kamati ya Amani na utulivu Tanzania Sheikh Noman Thabit Jongo akisisiza kwa viongozi wa Dini kuisoma na kuielewa Katiba Inayopendekezwa ili kuepuka chuki zinazosambazwa kuhusu katiba hiyo ili baadae waweze kufanya uamuzi sahihi utakaopelekea uwepo wa amani nchini. 
Katibu wa Kamati ya Amani na utulivu Tanzania Padri. Damas Mfoi akiongea katika mkutano wa Kamati ya Amani na Viongozi wa Dini mbalimbali Zanzibar na kuwaasa kusambaza ujumbe wa Amani na kuepuka mambo yoyote yatakayoashiria uvunjifu wa amani hasa katika kipindi hiki Taifa likielekea katika Mchakato wa upatikanaji wa Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu. 
Baadhi ya Viongozi mbalimbali wa Dini Zanzibar wakifuatilia Mada zilizokuwa zikiwasilishwa katika Mkutano huo.
Mmoja ya Mjumbe wa Mkutano akifanya rejea katika Katiba Inayopendekezwa wakati wa uwasilishwaji wa Mada katika Mkutano huo. (Picha zote na Hassan Silayo)


Na Hassan Silayo
VIONGOZI wa Dini nchini wameaswa kuhubiri suala amani na utulivu nchini hasa katika kipindi hiki taifa likielekea upatikanaji wa Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa wilaya ya Mjini Magharibi Bw. Ayoub Mohamed Mahmoud wakati wa mkutano wa Kamati ya amani Tanzania na Viongozi wa Dini Mbalimbali leo Zanzibar
Bw. Ayoub alisema kuwa suala la amani na utulivu linamhusu kila mtu kwenye jamii na Taifa kwa ujumla hivyo ni budi kuepuka vishawishi vya uvunjifu wa amani hasa katika wakati huu wa kuelekea upatikanaji wa Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu.

“ Kama tunavyofahamu sasa taifa linaelekea katika mambo makubwa mawili ya upatikaji wa  Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu hivyo ninyi kama viongozi wa Dini hamna budi kuhubiri Amani na Utulivu ili Taifa kwa ujumla liweze kufikia dhamira na malengo yaliyowekwa” Alisema Ayoub.

Aidha Bw. Ayoub aliongeza kuwa nchi yetu ina sheria, kanuni na taratibu zinazotuongoza hivyo wananchi hawana sababu ya kugombana hasa kwenye mambo yanayolenga kuliletea taifa maendeleo kwani hatuna pengine pa kwenda pindi machafuko yanapotokea.
Akizungumzia kuhusu mchakato wa Katiba Inayopendekezwa Bw. Ayoub alisema kuwa wananchi hawana budi kujitokeza katika kuipigia kura ya maoni Katiba Inayopendekezwa kwani katiba hii imegusa makundi yote katika jamii.

Pia Bw. Ayoub aliwaasa viongozi wa dini kuisoma katiba hii kifungu kwa kifungu, ibara kwa ibara ili kwenda kutoa elimu kwa waumini wao ili kuepuka upotoshaji unaofanywa na baadhi ya watu wasioitakia mema nchi yetu.

Naye Mbunge wa WAWI kupitia tiketi ya Chama cha Wananchi (CUF) Mh. Hamad Rashid Mohamed alisema kuwa amekuwa akishangazwa na baadhi ya watu wanaopita mitaani na kutoa upotoshaji wa baadhi ya vipengele vilivyo katika Katiba Inayopendekezwa bila kuangalia madai yaliyopelekea kuanzishwa kwa mchakato wa upatikaji wa Katiba  Mpya.

Mh. Rashid alisema kuwa maaandamano mengi yaliyokuwa yakifanyika kudai upatinaji wa Katiba Mpya yalitaka uwepo wa Tume huru ya uchaguzi,Mgombea huru na  matokeo ya Tume kuhojiwa mahakamani na si suala la Serikali tatu au Serikali ya Mkataba jambo ambalo limejumuishwa vyema katika Katiba  Inayopendekezwa na kutoa  fursa pana zaidi ya kile walichokuwa wakidai.
Alieleza kuwa wananchi hawana budi kusoma na kuelewa maudhui yaliyomo Katiba Inayopendekezwa ili kuona fursa zinazopatikana na jinsi gani Katiba hiyo imegusa maisha ya kila kundi katika Jamii ikiwemo watoto, wavuvi, walemavu, vijana, wanawake na wazee.
Pia Mh. Rashid alisema kuwa viongozi wa dini hawana budi kuhubiri amani hasa katika kipindi hiki cha upatinaji wa Katiba Mpya na kuwaepuka wale wote wanaotaka kulipeleka taifa katika hali uvunjifu wa amani kwa kuhubiri chuki hasa juu ya Katiba Inayopendekezwa.

Akizungumzia kuhusu suala la amani na utulivu katika mchakato huu wa Upatikanji wa Katiba Mpya Mwenyekiti wa Kamati ya Amani na Utulivu Tanzania Sheikh Noman Thabiti Jongo alisema kuwa njia pekee ya kuepuka uvunjifu wa amani ni kwa kuisoma na kuielewa Katiba Inayopendekezwa na kuacha kusikiliza chuki zinazoenezwa na baadhi ya watu kuhusu mchakato huu.


Naye Katibu wa Kamati ya amani na Utulivu Padri Damas Mfoi aliwataka viongozi wote wa dini katika nafasi zao kuhubiri amani na utulivu hasa katika kipindi hiki cha kuelekea upatikanaji wa Katiba Mpya na Uchaguzi mkuu.

No comments:

Post a Comment