TANGAZO


Wednesday, December 24, 2014

Bil. 20 zimetumika uchaguzi Serikali za Mitaa - Serikali

MKURUGENZI wa Serikali za Mitaa Kharist Luanda akizungumza na waandishi wa Habari mjini hapa ( hawapo pichani) kuhusiana na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa katika baadhi ya maeneo ambayo yalikuwa hayakamilisha uchaguzi huo na  changamoto zilizojitikeza katika maeneo hayo.Kushito kwake ni Katibu Mkuu wa Tamisemi Jumanne Sagini. (Picha na Joyce Kasiki)

Joyce Kasiki, Dodoma
UCHAGUZI wa Serikali za Mtaa ulitengewa jumla ya shilingi bilioni 20 kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi huo mpaka kukamilika kwake.
Katibu Mkuu ,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Jumanne Sagini alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza na waandishi wa Habari kuhusiana na mchakato mzima wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa .
Alisema, kutokana na bajeti hiyo ,Tamisemi imejipanga kutoa mafunzo kwa viongozi wote waliochaguliwa katika chaguzi hizo lengo likiwa ni kuwajengea uwezo ili waweze  kutekeleza majukumu yao vizuri zaidi.

"Mafunzo ni muhimu sana ,maana katika hawa waliochaguliwa wengine ni wapya kabisa,hawajawahi kuwa wajumbe ,tamisemi imejipanga kutoa mafunzo,
maana mwaka huu ,tulikuwa na bajeti kubwa ya shilingi  bilioni 20 kwa ajili ya maandalizi mpaka  na uchaguzi wenyewe,

"Kwa hiyo  hiyo suala la mafunzo  kwa wajumbe wapya wa seriaksli za mitaa ni muhimu sana."alisema Sagini

Amezitaka Halmashauri zote kuanza na mafunzo ya awali kwa viongozi hao na mwakani Ofisi hiyo itatoa mafunzo ya Kitaifa kwa viongozi wote waliochaguliwa.

Vile vile alisema,licha ya kutoa mafunzo hayo,pia ofisi hiyo itaweka kwenye tovuti majukumu ya kila kiongozi aliyechaguliwa ili kila mmoja ajue nini anachotakiwa kufanya katika nafasi yake.

Aidha alisemakatika tovuti hiyo kuna majukumu pia ya Watendaji wa vijiji  na watendaji wa mitaa lakini pia itawekwa namna ya wenyeviti wanavyopaswa kuendesha vikao vyao .

Akitoa matokeo ya jumla ya pamoja na maeneo yaliyokuwa bado hayakamilisha uchaguzi huo Mkurugenzi wa Serikali za Mitaa Kharist Luanda alisema, Chama Cha Mapinduzi  (CCM) kimeshinda nafasi ya uenyekiti katika vijiji elfu 9,378 kati ya vijiji  elfu 12,443 vilivyopo sawa na asilimia 79.81.

 Luanda alisema mpaka sasa matokeo waliyopata ni ya  vijiji  elfu 11,750 na jumla ya vyama 15 vimeshiriki katika uchaguzi huo.

Alisema katika matokeo hayo chama cha demokrasia na maendeleo(CHADEMA) kimepata vijiji elfu 1,754 sawa na asilimia 14.93, chama  cha wananchi CUf kimepata vijiji 516 sawa na asilimia 4.39.
Katika matokeo ya vitongoji kati ya vitongoji elfu 64,616 matokeo yaliyopatikana ni ya vitongoji elfu 60,688 ambapo CCM kimeshinda vitongoji elfu 48,447 sawa na asilimia 79.83.

"Upande  wa vitongoji Chadema kimepata vitongoji elfu 9,145 sawa na asilimia 15.07 huku CUF ikipata vitongoji elfu 2,561 sawa na asilimia 4.22,"alisema Luanda.

Luanda alisema upande wa matokeo ya wenyeviti yamepatikana ya mitaa yote ambapo jumla ya mitaa  nchi nzima ni elfu 3,875 na kati ya hiyo   CCM mitaa 2583 sawa asilimia 66.66, Chadema mitaa 980 sawa na asilimia 25.29 na CUF mitaa 266 sawa na asilimia 6.86.
"Katika  nafasi ya ujumbe CCM imepata wajumbe 100,436 sawa na asilimia 80.24, Chadema elfu 18,527 sawa na asilimia 14.80 na CUF wajumbe 5395 sawa na asilimia 4.31,"alisema Luanda.

Alieleza kuwa upande wa wajumbe wa viti maalum wanawake kati ya nafasi elfu 80,537 CCM imepata wajumbe elfu 66,147 sawa na asilimia 82.13,Chadema elfu 10,471 sawa na asiimia 13 na CUF wajumbe elfu 2676 sawa na silimia 3.32.

Akizungumzia muitikio wa watu katika kujiandikisha na kujitokeza kupiga kura Luanda alisema mwitikio ni mkubwa ukilinganisha na uchaguzi uliopita wa mwaka 2009.

"Mwitikio ni mzuri na hii imetokana na kazi nzuri iliyofanywa na vyombo vya habari kwa kutenga muda kabisa kuonyesha zoezi zima linavyoendelea siku ya kupiga kura."alisema Luanda

No comments:

Post a Comment