TANGAZO


Wednesday, October 22, 2014

Shule ya Sekondari Manzese kunufaika na mradi wa Biogas


Meneja Uhusiano wa Jamii Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es salaam (DAWASA) Bi. Neli Msuya alipokuwa akiongea na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki walipotembelea mradi wa ujenzi wa mtambo wa nishati endelevu inayohifadhi mazingira (Biogas) katika shule ya sekondari Manzese iliyopo Mtaa wa Chakula bora kata ya Manzese Wilaya Kinondoni jijini Dar es salaam. Mradi huo unatekelezwa shuleni hapo na DAWASA kwa kushirikiana na Shirika la Mpango wa Makazi la Umoja wa Mataifa (UN-HABITAT).

Meneja wa Mradi wa ujenzi wa mtambo wa nishati endelevu inayohifadhi mazingira (Biogas) kutoka UN-HABITAT Phillemon Mutashubirwa akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari walipotembelea mradi huo unaotekelezwa katika shule ya sekondari Manzese mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.

Mratibu wa Mradi ujenzi wa  mtambo wa kuzalisha gesi ambayo ni nishati endelevu inayohifadhi mazingira (Biogas) kutoka Taasisi ya Kuendeleza Nishati Asilia na Uhifadhi wa Mazingira (TaTEDO)  Shima Sago akieleza faida zitokanazo na biogas kwa waandishi wa habari walipotembelea mradi huo unaotekelezwa katika shule ya Sekondari Manzese mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.
Mwalimu wa Taaluma wa shule ya sekondari Manzese Zubeda Kindamba akiushukuru uongozi wa DAWASA kwa kuendelea kuiunga mkono shule yao katika masuala mbalimbali ukiwemo Mradi wa ujenzi wa  mtambo wa kuzalisha gesi asilia shuleni hapo.
Mwalimu wa Taaluma wa shule ya sekondari Manzese Zubeda Kindamba akiushukuru uongozi wa DAWASA kwa kuendelea kuiunga mkono shule yao katika masuala mbalimbali ukiwemo Mradi wa ujenzi wa  mtambo wa kuzalisha gesi asilia shuleni hapo.

Mwanafunzi wa kidato cha nne katika shule ya sekondari Manzese anayesoma masomo ya mchepuo wa sayansi Noela Shirima akielezea kwa waandishi wa habari namna watakavyonufaika mara utakapokamikika mradi wa gesi asilia itakayozalishwa na amesema kuwa kujengwa mradi wa gesi na maabara utawasaidia shuleni hapo kwa manufaa ya kupata elimu bora.

Meneja wa Mradi wa ujenzi wa mtambo wa nishati endelevu inayohifadhi mazingira (Biogas) kutoka UN-HABITAT Phillemon Mutashubirwa (kushoto) akifafanua jambo kwa waandishi wa habari walipotembelea mradi huo unaotekelezwa katika shule ya sekondari Manzese mwishoni mwa wiki jijini Dar es salaam. Wa kwanza kulia ni Meneja Uhusiano wa Jamii Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA) Bi. Neli Msuya.

Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Chakula bora Kata ya Manzes Salehe Rashidi akielezea kwa waandishi wa habari walipotembelea shule ya sekondari Manzese mwishoni mwa wiki namna wananchi wake wanavyoshikiana na Uongozi wa shule hiyo katika kujali taaluma ya wanafunzi na afya zao kwa kufanya usafi katika maeneo yanayozunguka shule.
Meneja Uhusiano wa Jamii Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es salaam (DAWASA) Bi. Neli Msuya (wa kwanza kulia) akiwaongoza waandishi wa habari na kujionea sehemu utakapojengwa mtambo wa kuzailsha gesi na zinapojengwa maabara katika shule ya sekondari Manzese. Kushoto ni Meneja wa Mradi wa ujenzi wa mtambo wa nishati endelevu inayohifadhi mazingira (Biogas) kutoka UN-HABITAT Phillemon Mutashubirwa.

Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari Manzese wakishiriki kuandaa eneo utakapojengwa mtambo wa kuzailsha gesi shuleni hapo.

Baadhi wa wananchi wa mtaa wa Chakula bora wakifanya usafi kuzunguka maeneo ya shule ya Sekondari Manzese. (Picha zote na Eleuteri Mangi –MAELEZO)

Na Eleuteri Mangi-Maelezo
SHULE ya Sekondari Manzese inatarajiwa kunufaika na mradi wa ujenzi wa mtambo wa kuzalisha gesi ambayo ni nishati endelevu rafiki na inayohifadhi mazingira nchini (Biogas).
Kauli hiyo imetolewa na Meneja Uhusiano wa Jamii Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA), Bi. Neli Msuya juzi, alipokuwa akiongea na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki walipotembelea mradi wa ujenzi wa mtambo wa nishati endelevu inayohifadhi mazingira (Biogas) katika shule ya sekondari Manzese iliyopo Mtaa wa Chakula bora kata ya Manzese Wilaya Kinondoni jijini Dar es salaam.
Bi. Neli alisema kuwa mradi huo unatekelezwa shuleni hapo na DAWASA kwa kushirikiana na Shirika la Mpango wa Makazi la Umoja wa Mataifa (UN-HABITAT) ili kupata gesi ambayo pia itasaidia upatikanaji wa umeme mbadala utakaotumika kwa matumizi mbalimbali na kuboresha taaluma kwa wanafunzi.
Baada ya kutambua kuwa zaidi ya asilimia 80 ya majisafi yanayotumika hugeuka kuwa maji taka, Bi. Neli amesema kuwa endapo kiasi hicho cha majitaka kisipodhibitiwa ipasavyo neema hiyo ya kuongezeka kwa majisafi inaweza isionekane.
“Shule haitalazimika kufikiria majitaka hayo yaende wapi kwani DAWASA inatoa suluhisho na imechukua jukumu la kuhakikisha maji hayo yanatumika kuzalisha gesi ambayo ni rafiki kwa mazingira na afya za wanafunzi, walimu na wanaozunguka maeneo ya shule” alisema Bi. Neli.
Bi. Neli ameongeza kuwa sanjari na ujenzi wa mtambo huo wa gesi unaoendelea, pia ujenzi wa maabara kwa masomo ya sayansi ambazo zitatumia gesi itakanayotokana na majitaka yanayozalishwa shuleni hapo unaendelea kwa ushirikiano na UN-HABITAT ili kuboresha taaluma.
Kwa upande wake Meneja wa Mradi huo nchini kutoka UN-HABITAT Phillemon Mutashubirwa amesema kuwa gesi hiyo itatumika kwenye maabara ambazo zinajengwa shuleni hapo kuitikia wito wa Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete alioutoa kuwa shule zote ziwe zimejenga maabara kwa masomo ya Kemia, Fizikia na Biyolojia ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.
Naye Mratibu wa Mradi wa kujenga mtambo wa kuzalisha gesi ambayo ni nishati endelevu inayohifadhi mazingira (Biogas) kutoka Taasisi ya Kuendeleza Nishati Asilia na Uhifadhi wa Mazingira (TaTEDO)  Shima Sago amesema kuwa kukamilika kwa mradi huo utakuwa na faida nyingi kwa shule na jamii inayoizunguka shule hiyo.
Shima amezitaja faida hizo kuwa ni pamoja na gesi hiyo itakuwa ya bei nafuu ambapo gharama yake ni ya chini kutokana na malighafi kupatikana shuleni hapo na nishati hiyo inajitosheleza kwa mazoezi ya wanafunzi maabara, kupikia kwenye kantini ya shule, kuwasha taa kwa ajili ya wanafunzi kujisomea pamoja na ulinzi na usalama wa shule. 
Shima ametaja faida nyingine ni kutibu majitaka yanayotokana vyoo na kuondoa athari ambazo ni chanzo cha magonjwa hatari kwa afya za wanafunzi na jumuiya nzima inayoizunguka shule hiyo.
Aidha, Shima amesema kuwa gesi itakayozalishwa katika mradi huo ni ujazo wa kyubiki mita 200 ambazo zitakuwa na uwezo wa kuzalisha umeme wa kilowati 50 ambao utatosha kwa matumizi ya shule.
Vilevile Shima amesema kuwa mradi huo utagharamu zaidi ya       Sh. Milioni 70 za Kitanzania ambapo mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Disemba mwaka huu tayari kuanza kutumika mwezi Januari 2015.  

Kwa upande wa wanafunzi, Noela Shirima mwanafunzi wa kidato cha nne anayesoma masomo ya mchepuo wa sayansi amesema kuwa kujengwa mradi wa gesi na maabara utawasaidia kufanya mazoezi mengi ameahidi kuwa watatumia muda wao vizuri ili kuboresha taaluma yao ili waweze kufikia malengo yao waliojiwekea kwenye maisha.
Aidha, kwa kutambua umuhimu wa uondoshaji wa majitaka, DAWASA iko mbioni kujenga mitambo yenye uwezo wa kutibu lita milioni 241 za majitaka kwa siku katika Manispaa zote tatu za jiji la Dar es salaam.
Mitambo hiyo itajengwa maeneo ya Mbezi Beach (Kinondoni), Jangwani (Ilala) na Kurasini (Temeke) ambapo wateja wakatakaounganishwa katika mfumo wa majitaka wataongezeka  kutoka 18,568 hadi 25,000 mwaka 2015/2016.

No comments:

Post a Comment