TANGAZO


Tuesday, May 20, 2014

Rais Dk. Shein atembelea Bandari ya Malindi mjini Unguja


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein (wa pili kushoto), akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Shirika la Bandari Zanzibar, Abdalla Juma (katikati), alipofanya ziara ya kutembelea katika Ofisi ya Shirika hilo leo, Wilaya ya Mjini Unguja. (Picha zote na Ramadhan Othman, Ikulu)
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein (wa pili kushoto), akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Shirika la Bandari Abdalla Juma (katikati) alipofanya ziara ya kutembelea katika Ofisi ya Shirika hilo leo Wilaya ya Mjini Unguja,(kushoto) Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano Seif Rashid (kulia), Naibu Waziri Issa Haji Gavu, na wapili kulia ni Katibu Mkuu wizara hiyo, Juma Akili.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein (katikati), akipata maelezo kutoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo na Maliasili, Affani Othman Maalim (kulia), alipotembelea Ghala linalomilikiwa na wizara hiyo, akiwa katika ziara ya kutembelea Maghala mbalimbali katika bandari ya Unguja leo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein, akisalimiana na Maofisa wa Shirika la Biashara (ZSTC), alipotembelea maghala yanayomilikiwa na Shirika hilo, katika  Bandari ya Malindi mjini Unguja leo, alipofanya ziara maalum.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein (wa pili kulia), akipata maelezo kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko, Julian Raphael (kulia), alipokuwa akiangalia mashine ya kusindika karafuu ambayo kwa hivi sasa iko katika hali ya uchakavu na kutofanya kazi, wakati alipofanya ziara ya kutembelea maghala ya karafuu yaliyopo bandarini, Malindi mjini Unguja leo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein (wa pili kulia), akipata maelezo kutoka kwa  Mkurugenzi wa Shirika la Bandari, Abdalla Juma (katikati), alipofanya ziara ya kutembelea eneo la kuhifadhia Makontena katika Bandari ya Malindi Mjini Unguja leo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein (wa tatu kulia), akiuliza suala kwa Mkurugenzi wa Shirika la Bandari, Abdalla Juma (wa pili kulia) wakati alipofanya ziara ya kutembelea eneo la kuhifadhia Makontena katika Bandari ya Malindi Mjini Unguja leo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein (wa pili kushoto), akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Shirika la Bandari, Abdalla Juma (kushoto), wakati alipofika kuiangalia mashine ya kufanya uchunguzi wa vitu vilivyomo ndani ya makontena, alipofanya  ziara ya kutembelea eneo la kuhifadhia makontena katika Bandari ya Malindi, Mjini Unguja leo.

Na Said Ameir, Zanzibar

SERIKALI imelitaka Shirika la Bandari kuchukua hatua za haraka kushughulikia tatizo la msongamano wa makontena katika Bandari ya Malindi ili shughuli za bandari hiyo ziweze kufanyika kwa ufanisi.


Akizungumza mara baada ya kutembelea bandari hiyo pamoja na eneo linalohifadhia makontena matupu karibu na hoteli ya Bwawani wilaya ya mjini Unguja, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alisema kwa ujumla hali hairidhishi katika bandari hiyo kutokana na msongomano wa makontena.


“Bandari haina nafasi ya kuweka makontena yote yanayoingia na yanayotoka. Hali hainiridhishi mimi na kila mtu hapa. Kwa mfano leo hii bandarini kuna meli inashusha makontena karibu 350 mengine yakijazana kila mahala mpaka hapa Bwawani” Dk. Shein alifafanua.


Alijibu swali kuhusu madhumuni ya ziara hiyo alisema ilikuwa ni kuona maeneo yote ya bandari yakiwemo ya kuwekea makontena na pamoja na maghala mbalimbali ili kuona kipi kinaweza kufanyika kupata eneo kwa ajili ya kuondoa tatizo la msongomano wa makontena katika bandari hiyo.


Aliukumbusha uongozi wa Shirika hilo kuwa sehemu ya kuwekea makontena la Bwawani ni ya muda tu kama ilivyokubaliwa wakati wa uongozi uliopita wa Shirika hilo ulipokabidhiwa eneo hilo hivyo ana hakikika kuwa tangu wakati huo walikuwa wanafanya mipango mbadala wa kupata eneo jingine.



Alifafanua kuwa eneo hilo limo katika mpango wa Serikali wa uwekezaji kwa shughuli nyingine za maendeleo ambapo wakati wo wote linaweza kuchukuliwa kwa shughuli hizo hivyo uongozi wa bandari hauna budi kuzingatia hilo kwa kuharakisha mipango yake ya kuondoka katika eneo hilo.


Hata hivyo Dk. Shein alikiri kuwa Bandari ya Malindi hivi sasa imeshakuwa ndogo na itakuwa vigumu kukidhi mahitaji ya matumizi ya sasa ya bandari hasa baada ya mfumo wa usafirishaji wa bidhaa kubadilika kuwa wa kutumia makontena.


Kwa hiyo alieleza kuwa ndio maana jitihada za Serikali zimeelekezwa katika kutekeleza mpango wake wa ujenzi wa bandari mpya na ya kisasa huko katika eneo la Mpigaduru liliko kilomita chache kutoka bandari ya sasa ya Malindi.


Katika ziara hiyo Dk. Shein amelitaka Shirika hilo kuangalia upya matumizi bora ya baadhi ya majengo yake kwa kuyajenga upya ili kupata ofisi za kisasa na bora ili Shirika liweze kutoa huduma vizuri kwa wateja wake.


Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Bandari Bwana Abdalla Juma Abdalla alisema lengo la kuhifadhi makontena matupu katika eneo la Bwawani ni kutoa nafasi kwa makontena yenye bidhaa kuweza kushushwa kutoka melini na kuokoa gharama na usumbufu pindi makontena hayo yakichelewa kushushwa kutoka melini.


Alibainisha kuwa Shirika lake inalipa kipaumbele suala la kuondosha msongomano wa makontena bandarini hapo na kwamba uongozi wa bandari wakati wote umekuwa ukihakikisha kunakuwepo na ufanisi katika utendaji wake.


Katika ziara hiyo Dk. Shein alifuatana na viongozi mbalimbali kutoka Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano, Wizara ya Kilimo na Maliasili pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Maalim Abdalla Mwinyi Khamis.

No comments:

Post a Comment