TANGAZO


Thursday, July 11, 2013

Tanzania na Sweeden zatiliana saini mikataba ya maendeleo yenye thamani ya bilioni 231.


Balozi wa Sweden nchini Tanzania, Lennarth Hjelmaker akiweka saini kati ya mikataba miwili iliyosainiwa kwa ajili ya kusaidia bajeti ya Serikali katika juhudi za kukuza uchumi nchini (MKUKUTA), Dar es Salaam leo. Kushoto ni Waziri wa Fedha Dk. William Mgimwa.(Picha zote na Lorietha Laurence)
Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa wakipena mkono wa shukrani na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, Dk.Tonia  Kandiero baada ya hafla ya kutiliana saini mkataba wa mkopo wa kusaidia ujenzi wa barabara ya Arusha - Holili mpaka Taveta - Voi nchini Kenya leo, jijini Dar es Salaam.
Mwakilishi mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, Dk.Tonia  Kandiero akitoa shukrani baada ya hafla ya kusaini mkataba wa mkopo wa kusaidia ujenzi wa barabara ya Arusha - Holili mpaka Taveta - Voi nchini Kenya leo, jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa. 

Na Lorietha Laurence, MAELEZO
SERIKALI ya Tanzania na Sweden leo, zimetiliana saini ya mikataba miwili yenye thamani ya shilingi bilioni 231 kwa ajili ya kusaidia bajeti ya serikali katika mwaka wa fedha 2013/2014 na kukarabati chanzo cha umeme wa maji cha Hale kilichopo mkoani Tanga.

Hafla ya utiaji saini wa mikataba hiyo imefanyika  jijini Dar es Salaam ambapo Waziri wa Fedha Dkt. William Mgimwa ametia saini kwa upande wa Tanzania na Balozi wa Sweeden nchini Bw Lennarth Hjelmaker amesaini kwa niaba ya Sweeden.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri Mgimwa ameeleza kuwa kati ya fedha hizo, bilioni 202 ndani ya miaka miwili kuanzia mwaka huu wa fedha na zitatumika kwa ajili ya kuhamasisha ukuaji wa uchumi kuangalia malengo ya MKUKUTA awamu ya pili kwa ajili ya kupunguza umaskini. 

“Bilioni 29 zitatolewa katika kipindi cha miaka minne kuboresha mitambo ya kuzalisha nishati ya umeme katika mtambo wa Hale, Tanga. Hatua hii itasaidia kupatikana kwa nishati ya kutosha ya umeme, ambayo kwa muda wa miaka 40 upatikanaji wake umekuwa na uhitaji mkubwa,” amesema.

Kwa upande wake Balozi Hjelmaker ameeleza kuwa nchi yake imetoa msaada huo chini ya shirika la msaada la nchi hiyo (SIDA) kutokana na kutambua juhudi za serikali ya Tanzania za kuwapunguzia wananchi wake umaskini kupitia bajeti ya serikali.

“Lengo la kuchangia bajeti ya serikai ni kuiunga mkono Tanzania katika kufikia lengo lake la kuwapunguzia wananchi umaskini chini ya mpango wa MKUKUTA awamu ya pili inayotekelezwa kati ya mwaka 2010 hadi 2015,” amesema na kuongeza kuwa msaada huo pia una lengo la kuimarisha mfumo bora wa utawala wa nchini.

Kuhusu mradi wa umeme wa Hale Balozi huyo wa Sweeden nchini amesema kuwa baada ya ukarabati wa mitambo hiyo ya kuzalisha umeme, Kituo cha hale kitakuwa na uwezo wa kuzalisha MW 21 zitakazoingizwa  katika gridi ya Taifa na kupunguza tatizo la mara kwa mara la upatikanaji wa nishati ya umeme.

Uhusiano kati ya Sweeden na Tanzania umeanza tangu miaka ya 1960 na Tanzania imekuwa ikipata msaada wa mara kwa mara wa kifedha kwa ajili ya kuboresha miradi mbalimbali ya kiuchumi.

No comments:

Post a Comment