Baadhi ya madishi ya setilite ya kupokela picha na matangazo ya Digitali yakiwa kwenye jengo lililozinduliwa leo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, Rahaleo, mjini Zanzibar, ikiwa ni katika shamrashamra za maadhimisho ya miaka 49 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Na Khadija Khamis –Maelezo Zanzibar 08/01/2013.
SHIRIKA la Utangazaji Zanzibar (ZBC), limetakiwa kuhakikisha kwamba linafanyakazi kwa ufanisi mkubwa kulingana na mfumo uliopo hivi sasa.
Alisema kuwa wafanyakazi wa Shirika hilo, wameonakana wakifanya kazi kimazowea tu, bila kufuata taratibu za kikazi.
Hayo, yameelezwa leo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohammed Shein katika Uzinduzi wa Miundombinu ya Dijitali na Jengo la Studio ya Kisasa.
Alisema kuwa kubadilika kwa watendaji kazi ni suala la lazima kutokana na mabadiliko makubwa yalioko duniani .
Dk. Shein alisema kuwa ZBC wananchi wengi wanapiga kelele juu ya utendaji wa wafanyakazi wa ZBC kutokana na vipindi vyao kutoridhisha na kukatika katika kwa matangazo yao zaidi wakati wa taarifa ya habari.
Alisema kuwa Zanzibar inaheshima yakekatika masuala ya Utangazaji kwani Redio nyingi za Nje zinawatangazaji kutoka Zanzibar ambao ni mahiri katika masuala ya Utangazaji.
Dk. Shein amesema kuwa hivi sasa hatoweza kuvumilia tena kutokana na utendajihuo ambao hauridhishi hata kidogo na hasa sasa tulivyoingia katika mfumo huu wa DIGITALI.
“Sitaki kuiona Serikali ambayo ninayoiongoza mie, iwe ‘tiro’ (mwisho), alisema Dk. Shein.
Alisema kuwa kuingia katika mfumo mpya wa dijitali ni kazi kubwa lazima watendaji wafanyekazi kwa mashirikiano na kuwe na uwiano baina yao ili kuweze kuwa na kiwango ambacho kitaweza kuwajengea sifa wafanyakazi hao.
Alieleza kuwa madhumuni makubwa ya Mapinduzi ni kuweza kuwakomboa wanyonge na kuwabadilisha maisha yao sitofurahishwa na kuona gharama zote zilizotumika katika kuingia katika mfumo huo mpya wa Digitali kuweza kupotea bure lazima viongozi waweze kusimamia majukumu yao na kuanzia hivi sasa lazima mambo yaende.
‘Hakuna aliekamilika lakini tujitahidi’’, alisema Dk. Shein .
Dk. Shein alimtaka Waziri wa Habari Utamaduni Utalii na Michezo Zanzibar Said Ali Mbarouk pamoja na Katibu wake kuisimamia ipasavyo Shirika hilo la ZBC na kuhakikishakuwa mambo yanakwenda vizuri.
Akizungumzia juu ya Studio ya Kurikodia Dkt Shein amesema kuwa madhumuni ya kutengeneza Studio hiyo ni kwaajili ya Wasanii wa Zanzibar waweze kupata nafasi nzuri za kurekodia nyimbo zao na hapo hapo kuwa na pahala ambapo wataweza kurekodi michezo ya kuigiza napia kuonesha maigizo mbali mbali katika ukumbi huo.
Naye Waziri wa Wizara ya Habari Utamaduni Utalii na Michezo, Said Ali Mbarouk alisema kuwa miundombinu mipya ya Digitali ni mkataba baina ya Serikali ya Zanzibar na Kampuni ya Ágape na imeagharimu jumla ya Sh. billion 8 za Tanzania na kuweza kujengea vituo 6 vya kurushia matangazo vikiwamo vya Kizimkazi, Nungwi na Masingini. Kwa upande wa Pemba ni Konde,Mizimiumbi na Mkanjuni.
Aidha alisema kuwa ifikapo tarehe 28 /2/ 2013 analogi itazimwa na kuanza mfumo mpya wa dijitali na kuwaeleza wananchi wasiwe na wasiwasi ya upataji wa vingamuzi ambavyo vitakuwa vyakisasa na madhubuti.
Said alisemakuwa vingamuzi hivyo vitapatikana kwa katika sehemu mbali mbali za Wilaya zote kumi za Zanzibar na hakutakuwa na haja kwa watu kufuatia Mijini.
Alisema kuwa kila kingamuzi kimoja kinatarajiwa kuuzwa si zaidi ya shs za Tanzania 50,000 na malipo ya matangazo yatakuwa si zaidi ya shiling za Tanzania 8000 vikiwa na chanal 36-38.
|
No comments:
Post a Comment