TANGAZO


Monday, August 4, 2014

Makalla-Uwezeshaji wa Viwanda na Changamoto ya Kuhifadhi Mazingira

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Binilith Mahenge (katikati) akiambatana na mwenyeji wake Mkurugenzi wa Miradi ya kiwanda cha M.M Integrated Steel Mills Ltd, Lawrence Manyama (kulia) wakati walipowasili kwenye kiwanda hicho kwa ukaguzi.Kushoto ni Mwanasheria wa Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira (NEMC)Manchare heche.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Binilith Mahenge (mwenye koti la bluu) akijadili jambo na maafisa wa Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira (NEMC) juu ya madini tembo yanayotumika kwenye kiwanda cha M.M Integrated Steel Mills Ltd.
Mkurugenzi wa Miradi ya kiwanda cha M.M Integrated Steel Mills Ltd, Lawrence Manyama (anayeonesha chini) akimuonesha Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Binilith Mahenge( kulia kwake) sehemu yenye mchanganyiko wa mabaki ya madini yanayotumika kiwandani hapo.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Binilith Mahenge( kulia) akitoa msimamo wa Serikali kuhusu kiwanda hicho baada ya kukikagua.Katikati ni Mkurugenzi wa Miradi ya kiwanda cha M.M Integrated Steel Mills Ltd, Lawrence Manyama na Mkuu wa Biashara wa kiwanda hicho Shashikant Modi.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Binilith Mahenge, akitoa maelekezo kwa wamiliki wa kiwanda cha BIDCO Oil & Soap Ltd( hawapo pichani) juu ya kusitisha kutumia magogo kama chanzo cha nishati.Aliyevaa overall ya njano ni Msimamizi Mkuu wa kiwanda hicho David Kiawa akimsikiliza.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Dk. Mhandisi Binilith Mahenge (kulia) akipiga picha bomba linalotiririsha maji machafu kutoka kiwanda cha NIDA.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Dk. Mhandisi Binilith Mahenge, akiwaonesha wamiliki wa kiwanda hicho maji yanayotoka kiwandani kwao.Kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa  NEMC Bonaventure Baya.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Binilith Mahenge (mwenye koti la bluu) akijadili jambo na maafisa wa Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira (NEMC) juu ya madini tembo yanayotumika kwenye kiwanda cha M.M Integrated Steel Mills Ltd.
 ia kitu wakati alipokuwa akikagua mfumo wa majitaka wa kiwanda cha Murzah Oil MilWaziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Dk. Mhandisi Binilith Mahenge, (anayeonesha kidole) akiashirls Ltd.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Dk. Mhandisi Binilith Mahenge, (anayeonesha kidole) akiashiria kitu wakati alipokuwa akikagua mfumo wa majitaka wa kiwanda cha Murzah Oil Mills Ltd.

Hussein Makame-MAELEZO
UWEKEZAJI katika sekta ya viwanda ni moja ya chanzo muhimu katika maendeleo ya nchi.Kutokana na umuhimu huo Tanzania kila mwaka imekuwa ikiweka mikakati ya kuwavutia wawekezaji ili kukuza uchumi wake.
Mbali na kukuza uchumi wa nchi,  uwekezaji umekuwa ukitoa mchango mkubwa katika ustawi wa jamii ya Watanzania katika nyanja mbalimbali hasa nyanja ya kijamii.

Ripoti ya uwekezaji Tanzania ya mwaka 2012, inaonesha kuwa kampuni zilizowekeza kwenye shughuli za uzalishaji viwandani ziliongoza kutoa huduma kwa jamii kwa wastani wa Dola za Kimarekani Milioni 3.6 kwa mwaka 2008 na 2009.

Pamoja na mchango huo wa uwekezaji wa viwandani, baadhi ya viwanda vimekuwa chanzo cha kuhatarisha maisha ya wananchi wanaozunghuka maeneo ya viwanda hivyo.
Hivi karibuni, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Dk. Mhandisi Binilith Mahenge alifanya ziara ya kutembelea baadhi ya viwanda vilivyopo jijini Dar es Salaam kuangalia utekelezaji wa Sheria ya Mazingira hasa udhibiti wa majitaka kutoka viwandani.
Waziri Dkt. Mahenge alitembelea kiwanda cha NIDA Textile Mills Ltd, M.M Integrated Steel Mills Ltd, BIDCO Oil & Soap Ltd, Basic Element Ltd, Cocacola Kwanza, Murzah Oil Ltd na kutembelea dampo la Pugu Kinyamwezi na bwawa la majitaka la Vingunguti.
Matokeo ya ziara hiyo yanaonesha kuwa karibu asilimia 75 ya viwanda hivyo havizingatii Sheria ya Mazingira na hivyo kusababisha uchafuzi wa mazingira na kuathiri afya za wananchi, huku kiwancha cha Cocacola Kwanza kikwa mfano mzuri kwa kuzingatia sheria hiyo.
Ziara hiyo ilionesha kuwa karibu viwanda vitatu kati ya hivyo havitumii mitambo maalum ya kutibu majitaka yanayozalishwa, kimoja kinatumia chanzo cha nishati kinachochafua mazingira na kingine kikichangia uchafuzi.
Katika ziara hiyo ya kustukiza aliyoifanya kwenye kiwanda cha NIDA Textile Mills Ltd, Waziri aligundua udanganyifu unaofanywa na kiwanda hicho kwa kumwaga majitaka yanayoathiri afya za wananchi na mazingira kupitia mto Kibangu unaopita maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam.
Mmoja wa wakazi wa eneo la mto huo ambaye ni mjumbe wa shina namba 45 Asha Mbwembwe, analalamika kwamba, wakazi wa eneo hilo wanaathirika sana na maji ya kiwanda hicho cha NIDA.
“Tunashukuru leo mheshimiwa amefika kwani kwa huruma yake anaweza akasababisha yale maji yakatoka safi, watoto wanaenda shuleni wanapita kwenye maji haya wanayakanyaga, wakirudi miguu yote imebabuka, mboga zinalimwa tunakula, kwa hiyo hatujui kwa sababu hatuna utaratibu wa kwenda hospitalini kujicheki afya zetu  kutokana na hali zetu duni kifedha,  pengine tumeshaathirika hatujui lakini wenzetu hawana huruma na sisi kwa hayo maji yanayotoka” anasema Asha.
Mjumbe huyo anaiomba Serikali ilifuatilie suala hilo  kwa makini na kulipatia ufumbuzi.
Waziri Dkt. Mahenge anasema alipokea malalamiko karibu mara nne kutoka kwa wananchi juu ya NIDA kutiririsha maji machafu yanayowaathiri wananchi.
Na baada ya Waziri na timu ya Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira (NEMC) kukagua alibaini uchafuzi huo ingawa alipokutana na uongozi wa kiwanda hicho na kurudi kuthibitisha kile walichokiona waligundua kuwa maji yanayotoka ni tofauti na yale waliyoyashuhudia awali wakati walipokagua kabla.
Waziri akazungumza, “kinachofanyika hapa ni kama vile mwekezaji anajali cha kwake hajali maisha ya Watanzania…, tulipita mara ya kwanza na sasa tumeona haya, maana yake ni kwamba wenzetu hawa wanaidanganya sekta ya uwekezaji.”
Anaongeza kuwa “Maji tuliyoyakuta asubuhi sio haya ambayo mmeenda kuyafungua sasa hivi, maana yake mitambo (ya kutibu majitaka) mnayo isipokuwa mnaogopa gharama zenu, hamfungulii, na mnaonekana hamuwajali Watanzania”
Kiwanda hicho, awali kiliomba cheti cha kuhifadhi mazingira kutoka NEMC, na Waziri aliombwa kutia saini ili kuthibitisha kwamba kiwanda hicho kinahifadhi mazingira.
Ingawa Afisa Tawala wa kiwanda hicho Mohamed Honelo alijitetea na kuahidi kujirekebisha, lakini Waziri Dkt. Mahenge hakukubaliana nao na hivyo kutangaza kutotoa cheti hicho kama hatapata uhakika kwamba maji yataendelea kuwa mazuri kwa muda wote.
Waziri Dk. Mahenge pia alionesha hofu kuwa iwapo watapewa cheti wataendelea kudanganya Watanzania na kusababisha madhara kwa wananchi, kisha akatoa somo kwa Watanzania na wawekezaji:
“La kwanza ambalo ninataka Watanzania walifahamu ni kwamba tunataka sana wawekezaji na Serikali imeweka mazingira mazuri sana kuwavutia, lakini mwekezaji mzuri atakuwa ni yule tu anayejali mazingira”
Baada ya kuhitimisha ziara kwenye kiwanda hicho, Waziri Dkt. Mahenge alikitembelea kiwanda cha M.M Integrated Steel Mills Ltd.
Alibaini kuwa kiwanda hicho hakitumii mitambo ya kutibu majitaka na kuagiza ndani ya miezi minne kiwe kimeanza kuitumia mitambo hiyo.
Anauagiza uongozi wa kiwanda hicho kuwasilisha Mpango wa Kuhifadhi Mazingira wa kiwanda hicho baada ya miezi mitatu kutokana na uongozi huo kushindwa kuthibitisha kuwa nao.
Mbali na hayo, Waziri Dkt. Mahenge ametoa miezi mitatu wawasilishe tathimini ya ukaguzi wa mazingira kinyume cha hapo wataadhibiwa kwa kutozwa faini na NEMC.
Waziri Mahenge pia anabaini  kuwa, kiwanda hicho hakina sehemu maalum ya kumwaga kifusi cha madini tembo yanayokana na mabaki ya madini yanayotumiwa na hivyo kusababisha athari za kiafya kwa wananchi na mazingira.
Pia amekiagiza Kiwanda hicho kupeleka sehemu ya kivusi kwa mkemia mkuu ili kikapimwe.
Madini hayo ambayo ni metali nzito yanaweza kusababisha athari kubwa kwa binadamu ikiwa ni pamoja na kuathiri mfumo wa fahamu na wa kizazi.
Mkurugenzi wa Miradi ya kiwanda hicho, Lawrence Manyama ameahidi kutekeleza maagizo hayo baada ya kukiri kuwepo kwa upungufu huo kwenye kiwanda chao.
Kiwanda cha BIDCO Oil & Soap Ltd, hakikuwepo kwenye orodha ya kukaguliwa isipokuwa kilikuwa kikikilalamikia kiwanda jirani nacho (Basic Element Ltd) kuziba njia inayopitisha majitaka kutoka kiwandani kwao.
Lakini baada ya Waziri kutembea kiwandani hapo anagundua kuwa kiwanda hicho kinaendelea kutumia magogo ya miti kama chanzo cha nishati, jambo ambalo Waziri Dkt. Mahenge alilikemea vikali na kukipa miezi 6 kiwanda hicho kuacha kutumia magogo.
Waziri Dkt Mahenge anasema kuwa matumizi ya magogo yanachangia kuharibu mazingira kwa kiwango kikubwa ikiwemo kusababisha mabadiliko ya tabia nchi.
“Gharama za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ni kubwa mno, Serikali inahitaji kutumia fedha hizo kwenye masuala ya maendeleo, hivyo hatutakuwa tayari kuwaacha mkitumia chanzo hiki cha nishati”anasema Waziri Dkt. Mahenge.
Kiwanda cha Basic Element Ltd, kutokana na kuziba njia inayopitisha majitaka kutoka kiwanda cha BIDCO,Waziri Dkt. Mahenge ameitaka NEMC isimamie kuhakikisha njia hiyo inazibuliwa ndani ya mwezi mmoja.
Kwenye kiwanda cha Murzah Oil Mills Ltd, Waziri Dkt. Mahenge alikaribishwa na changamoto za kiwanda hicho kukosa maji kutoka Kampuni ya Kusambaza Maji mkoa wa Dar es salaam (DAWASCO).
Meneja Rasilimali Watu wa kiwanda hicho, Sam Mbuli, anasema kuwa ukosefu huo wa maji hukwamisha usafi wa kiwanda, pia bomba la majitaka ni bovu, mfumo wa majitaka umeziba, hivyo majitaka yanashindwa kupita.
Anasema kutokana na changamoto hizo, majitaka ya kiwanda hicho badala ya kupita kwenye bomba kwenda Vingunguti yanaishia maeneo ya wananchi.
Baada ya maelezo hayo, Waziri akaomba kupitishwa kuangalia mfumo wa majitaka wa kiwanda hicho, ambao baada ya kushuhudia hakuridhika nao.
Pia inabainika kuwa kiwanda hicho hakina mitambo ya kutibu majitaka yanayozalishwa na hivyo kusababisha majitaka kuathiri mazingira na afya za wananchi.
“Hali hii haikubaliki hata kidogo, hivyo lazima mtumie mitambo inayotakiwa kutibu majitaka, na tunasema hivi si kwa kiwanda chako tu, hivyo tunataka hili litekelezwe” anasema Waziri Dkt. Mahenge akimuagiza Meneja wa kiwanda hicho Dinesh Kana.
Kuhusu kufunga mitambo ya kutibu majitaka Waziri anatoa mwezi mmoja wa utekelezaji na ametoa wiki mbili kukutana na viwanda vilivyoko barabara ya Nyerere, DAWASCO na wengine kutatua changamoto ya maji na miundombinu ya majitaka.
Afisa Mazingira Manispaa ya Ilala Abdon Mapunda amemueleza Waziri kuwa baadhi ya viwanda vilivyoko barabara ya Nyerere hutiririsha majitaka kupitia mtaro unaokwenda bwawa la majitaka la Vingunguti, na kuwasababishia wananchi madhara makubwa.
Kutokana na athari hizo Waziri Dkt. Mahenge ameiagiza NEMC kuhakikisha inabaini viwanda vinavyopitisha majitaka hayo na kuvichukulia hatua za kisheria.
Akihitimisha ziara hiyo ya wiki mbili, Waziri Dkt. Mahenge anasema suala la mazingira lina changamoto kubwa, hivyo linahitaji kupewa kipaumbele na wenye viwanda.
Anasema kwa kuwa baadhi ya changamoto alizozishuhudia zinachangiwa na Sheria ya Mazingira iliyopo, Serikali imeamua kupitia upya sheria hiyo ili iendane na wakati.
“Yapo baadhi ya mambo yanayohitaji kuongezwa kwenye sheria hiyo ikiwemo suala la mabadiliko ya tabianchi, hivyo tutapita kwa wananchi kupata maoni yao kuhusu sheria hiyo” anasema Waziri Dkt. Mahenge.

Ziara hiyo ya kukagua utekelezaji wa Sheria ya Mazingira kwa viwanda hapa nchini ni endelevu, hivyo anawataka wenye viwanda kuhakikisha wanaizingatia Sheria hiyo.

No comments:

Post a Comment