TANGAZO


Tuesday, December 24, 2013

MAAZIMIO YA KIKAO CHA BARAZA KUU LA UONGOZI LA CUF TAIFA KILICHOFANYIKA UKUMBI WA SHABAN HAMISS MLOO MJINI DAR ES SALAAM TAREHE 21-22 Disemba, 2013


Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam leo, wakati alipokuwa akitoa maazimio ya Baraza Kuu la Uongozi la chama hicho. Kulia ni Naibu Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CUF, Abdul Kambaya.
Baadhi ya waandishi wa habari, wakimsikiliza Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba wakati alipokuwa akisoma maazimio ya Baraza Kuu la Uongozi Taifa la chama hicho, jijini Dar es Salaam leo. (Picha zote na Kassim Mbarouk-www.bayana.blogspot.com)

BARAZA Kuu la Uongozi Taifa la The Civic United Front (CUF- Chama Cha Wananchi) limekutana katika kikao chake cha kawaida kwa mujibu wa Katiba ya Chama, kikao ambacho kimeongozwa na Mwenyekiti wa Chama Taifa, Mhe. Prof Ibrahim Lipumba na kufanyika katika Ukumbi wa Shabani Hamisi Mloo , Dar es salaam, tarehe 21-22 Dec, 2013. Katika kikao hicho, Baraza Kuu la Uongozi la Taifa limepokea,  limejadili na kuzifanyia maamuzi Agenda zilizowasilishwa na Kamati ya Utendaji ya Taifa na kufikia maazimio yafuatayo:-

1.      KUHUSU MPANGO MKAKATI WA CHAMA

Baraza Kuu limepokea Taarifa ya Mpango Mkakati wa Chama kuelekea Chaguzi za Serikali za Mitaa,Vijiji na Vitongoji 2014 na Uchaguzi Mkuu 2015, na limeridhia Mpango huo baada ya Kujadili kwa Kina na linaamini kupitia Mpango huu Chama kitapata Mafanikio Makubwa.

2.      KUHUSU UCHAGUZI WA NDANI YA CHAMA

(a)    Baraza Kuu limepokea Taarifa ya Maendeleo ya Uchaguzi wa Ndani ya Chama na kuridhia utaratibu unaoendelea katika Uchaguzi na kuiagiza Kamati Tendaji kusimamia kwa karibu Uchaguzi huo.

(b)   Baraza Kuu linatoa wito kwa Wanachama wa CUF kushiriki kwenye Uchaguzi kwa kufuata taratibu za kidemokrasia bila ya kufanya kampeni za kuchafuana wala kutoa au kupokea rushwa.

3.      KUHUSU TAARIFA ZA FEDHA

Baraza Kuu la Uongozi ilinampongeza Mkurugenzi wa Fedha kwa kuandaa Taarifa za Fedha kuanzia za kila mwaka toka 2009 mpaka 2012 na kuziwasilisha kwa Msajili wa Vyama na Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa wakati.

4.      KUHUSU MAPENDEKEZO YA KAMATI YA BUNGE JUU YA OPERESHENI TOKOMEZA UJANGIRI

(a)    Baraza Kuu linapongeza Bunge la Jamuhuri ya Muungano na kukubaliana na Mapendekezo hayo yaliotolewa na Kamati ndogo ilioongozwa na Mhe. James Limbeli nakupelekea Mawaziri watatu kuvuliwa nyadhifa zao na Mmoja kujiuzulu mwenyewe. Kamati hii imetoa mapendekezo mazuri juu ya uhalifu na unyanywasaji waliofanyiwa Wananchi.

(b)   Baraza Kuu linamtaka Waziri Mkuu kuwajibika kwa matokeo ya Operesheni Tokomeza Ujangiri, kwa kuwa yeye ndiye chanzo kikuu cha udhalilishaji wa wananchi na hata kupoteza maisha kwa baadhi ya wananchi. Kauli yake ya PIGA TU, TUMECHOKA aliyoitamka ndani ya Bunge imehamasisha unyanywasaji wa Wananchi unaofanywa na vyombo vya dola, kwa hivyo Waziri Mkuu anapaswa kujiuzulu kwa matukio haya. La sivyo Rais amfukuze kazi.

(c)    Baraza Kuu linatoa wito kwa Serikali kuwachukulia hatua za kisheria wale wote waliohusika na uvunjwaji wa Haki za Binadamu na unyanyasaji wa Wananchi kwa kuwafikisha Mahakamani.

(d)   Baraza Kuu linatoa wito kwa Serikali kutazama utaratibu wa kuwalipa fidia Wananchi wote walioathirika na Vitendo hivyo.

5.      RAIS SHEIN AJIFUNZE TOKA KWA RAIS KIKWETE

Baraza Kuu la Uongozi linamtaka Rais wa Serikali ya Zanzibar kuiga mfano wa Rais Kikwete katika kushughulikia kero zinazoibuliwa na Vikao vya Baraza la Wawakilishi kwa kuwawajibisha Mawaziri wanaohusika kama ambavyo Rais Kikwete amekua akifanya katika kuunga mkono hoja  zinazoibuliwa Bungeni.

6.      KUHUSU TUHUMA ZA KATIBU MKUU WA CCM DHIDI YA MAWAZIRI MIZIGO

Baraza Kuu la Uongozi limesisitiza kuwa mara kadhaa CUF imekua ikieleza na kuonyesha OMBWE LA UONGOZI ndani ya Nchi yetu unaosababishwa na CCM na Serikali yake. CUF inaona kwamba, kutokana na Hoja nzito zinazojengwa na Katibu Mkuu wa CCM na Katibu wa Itikadi wa CCM ni kielelezo tosha cha uwepo wa OMBWE LA UONGOZI. Katika hali kama hii ambapo Katibu Mkuu wa Chama kinachotawala anaposhindwa kujenga hoja kwenye vikao vya Chama chake na kuwachukulia hatua wahusika na badala yake analazimika kujenga kwenye mikutano ya hadhara inaonyesha kuwa tuna Serikali inayokosa usimamizi kutokana na udhaifu wa Chama kinachounda Serikali.  

7.      KUHUSU UVUNJIFU WA HAKI ZA BINADAMU UNAOFANYWA NA VYOMBO VYA DOLA

Baraza Kuu linatoa wito kwa vyombo vya dola kuwa na weledi na uadilifu na kuheshimu na kulinda haki za binadamu za wananchi. Vyombo vya dola viache kujibu malalamiko na hoja za wananchi kwa matumizi makubwa kupita kiasi ya nguvu za dola. Matumizi ya nguvu kubwa kupita kiasi ya vyombo vya dola ni tatizo kubwa linalokua kwa kasi ndani ya nchi yetu. Wakati mwingine imefikia wananchi kuamua kujibu mapigo kwa kuchukua hatua za sheria mikononi mwao. CUF Inatoa wito kwa Vyombo vya Dola kuheshimu sheria na haki za binadamu na wasitekeleze amri za wanasiasa zisizojali utawala wa sheria na haki za binadamu ili kujijengea heshima na kupunguza uhasama baina ya vyombo vya dola na wananchi.

8.      KUHUSU MIGOGORO YA WAKULIMA NA WAFUGAJI

Baraza Kuu linatoa wito kwa Serikali kutafuta utaratibu wa kumaliza migogoro kati ya wakulima na wafugaji ambayo inachochewa na kukithiri kwa rushwa kwa viongozi wa serikali katika ngazi ya vijiji, kata na wilaya. Ni muhimu kuwa na sera  nzuri zinazotenga maeneo ya ufugaji na kuhamasisha ufugaji wa kisasa unaozingatia ulinzi wa mazingira na kuitumia mifugo kuongeza kipato na kuboresha maisha ya wafugaji. Sera hii itapunguza tatizo la uhasama kati ya wakulima na wafugaji ambalo limekua tatizo kubwa ndani ya nchi yetu.

9.      WITO KWA SERIKALI KUTOTUMIA VYOMBO VYA DOLA KIOPERESHENI

Baraza Kuu Iinatoa wito kwa Serikali kujenga uwezo endelevu wa kusimamia sheria za nchi ikiwemo kulinda hifadhi za taifa na kuepuka kulazimika kutumia operesheni baada ya tatizo kuwa sugu. Serikali isilitumie Jeshi la Wananchi wa Tanzania katika kushughulikia masuala ya uvunjifu wa sheria katika maeneo mbali mbali ya nchi yetu, na badala yake kazi hiyo ifanywe na Jeshi la Polisi kwa mujibu wa taratibu za kisheria. Jeshi la Polisi liongezewe uwezo wa kutimiza majukumu yake huku likiheshimu haki za kisheria za watuhumiwa. Jeshi la Wananchi liachiwe majukumu yake ya kulinda mipaka ya nchi yetu. CUF Inaona kwamba si vyema kulitumia Jeshi letu la kulinda mipaka ya nchi katika Operesheni zinazohusu uvunjaji wa sheria unaofanywa na wananchi. Askari wa JWTZ hawana mafunzo ya kukamata mwananchi mwenye tuhuma za uhalifu bila kuvunja haki zake za kisheria.

10.  KUHUSU MUUNDO WA MUUNGANO NA MCHAKATO WA KATIBA

Baraza Kuu linaamini kwamba rasimu ya mwisho ya katiba ya Tume ya Jaji Warioba haitakuwa na mabadiliko makubwa kuhusu muundo wa muungano wa serikali tatu uliopendekezwa katika rasimu ya kwanza ya katiba. Baraza Kuu linaamini kwamba uwepo wa serikali tatu katika muundo wa muungano ni jambo muhimu na ni njia mojawapo ya kumaliza kero za muungano. Baraza Kuu linaitaka Serikali kusimamia kikamilifu mchakato wa Katiba Mpya ili iweze kupatikana kabla ya Uchaguzi wa 2015. Ni wazi wananchi hawatakubali kuingia kwenye Uchaguzi 2015 kwa kwa kutumia katiba ya sasa ambayo imekataliwa na Watanzania wengi waliotoa maoni yao kwa Tume ya Jaji Warioba.

11.  KUHUSU HOJA YA UUNDAJI WA SERIKALI YA UMOJA WA KITAIFA

Baraza Kuu linamshauri Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, aunde Serikali ya Umoja wa Kitaifa ili iweze kusaidia kupatikana kwa Katiba mpya katika kipindi hiki cha mpito. Uwepo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa utarahisisha mjadala wa Bunge la Katiba na kulifanya bunge la Katiba kuchukua sura ya Kitaifa zaidi na hivyo kurahisha upatikanaji wa Katiba ya Taifa kwa misingi ya utashi wa Wananchi. Serikali ya Umoja wa Kitaifa itampa fursa Rais kuteua Baraza la Mawaziri lililo imara na kuondokana na Mawaziri wanaonekana ni mizigo ili ashughulikie matatizo mazito yanayolikabili taifa ikiwemo ongezeka ya gharama ya maisha, ukosefu wa ajira, kuporomoka kwa elimu, huduma hafifu za afya na maji safi na salama na ukosefu wa umeme wa uhakika.

12.  MKUTANO WA WADAU KUJADILI RASIMU YA KATIBA KABLA YA KUANZA BUNGE LA KATIBA

Baraza Kuu linatoa wito wa kuwepo mkutano wa wadau hususan vyama vya siasa na asasi za kiraia kujadili rasimu ya mwisho ya katiba kwa lengo la kufikia maridhiano ya mambo muhimu yaliyomo ndani ya rasimu ya katiba ili kurahisisha kazi ya Bunge la Katiba kufikaia muafaka kuhusu vipenger muhimu vya katiba mpya

13.  KUHUSU VITAMBULISHO VYA TAIFA VYA NIDA

Baraza Kuu linakumbusha kauli ya Mheshimiwa Rais Kikwete mwezi wa Februari 2013, siku ya uzinduzi wa vitambulisho vya taifa katika viwanja vya Karimjee Hall, alieleza kuwa vitambulisho hivyo ndivyo vitakavyotumika katika kura ya maoni na uchaguzi mkuu ujao. Kasi ya uandikishaji wa vitambulisho hivyo ni ndogo sana na haiwezi kufanikisha kuwapa vitambulisho Watanzania wote wenye umri wa miaka 18 au zaidi kabla ya kura ya maoni na hata mwaka 2015. Mpaka hivi sasa mwaka wa 2013 unamalizika Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) haijakamilisha utoaji wa vitambulisho mkoa wa Dar es Salaam. Lakini pia kuna vikwazo vingi katika uandikishaji wa vitambulisho hivyo na hasa pale unpohitajika kupata barua toka kwa Mjumbe wa Nyumba kumi kumi, ambae Sheria haimtambui na kwa hakika wajumbe hawa ni wa CCM. Baraza Kuu linatoa wito kwa Serikali kuondosha utaratibu huu wa kutumia Wajumbe wa Nyumba kumi kumi katika zoezi hili il kuleta ufanisi.

14.  KUHUSU DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA KATIKA KUFANIKISHA KURA YA MAONI YA KATIBA

Baraza Kuu limesikitishwa na hali ya kuwa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura halijaboreshwa tangu kumalizika uchaguzi wa 2015. Sensa ya mwaka 2012 inaonyesha kuwa kuna wananchi zaidi ya milioni 3.5 watakaokuwa wamefikisha umri wa miaka 18 kati ya 2010 na 2014. Wananchi wengi na hasa vijana wamepoteza vitambulisho vyaovya kupigia kura. Baraza Kuu linatoa wito kwa serikali na Tume ya Uchaguzi kuboresha daftari la wapiga kuandikisha wapiga kura wapya na kwapa vitambulisho vipya waliopoteza vitambulisho vya ili kutoa fursa kwa wananchi wenye haki ya kupiga kura kushiriki kupiga kura ya maoni ya kuridhia au kukataa Rasimu ya Katiba baada ya kujadiliwa na kupitishwa na BUNGE LA KATIBA la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

15.  DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA LA ZANZIBAR

Baraza Kuu linaitaka Serikali ya Mapinduzi iongeze uwajibikaji na kutoa Haki za kimsingi za Wananchi wa Zanzibar ikiwemo utoaji wa ZANID na kuandikisha Wananchi waliofikisha umri wa Miaka 18 katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura wa Zanzibar chini ya ZEC. Sheria ya ZANID inavunja Katiba ya Zanzibar kifungu cha 5 kinachoeleza kuwa “Zanzibar itafuata mfumo wa Kidemokrasia wa Vyama Vingi vya Siasa wenye kuheshimu utawala wa sheria, haki za binaadamu, usawa, amani, haki na uadilifu.” Na kifungu cha 7 (1) kinachoeleza kuwa “Kila Mzanzibari aliyetimiza umri wa miaka kumi na nane anayo haki ya kupiga kura katika uchaguzi unaofanywa Zanzibar na wananchi.” Baraza Kuu linatoa wito kwa Tume ya Uchaguzi ya Taifa (NEC) kuwaandikisha Wazanzibari wote walionyimwa ZANID alau wapate fursa ya kupiga kura ya maoni kama Wazanzibari kuikubali au kuikataa Katiba Mpya itakayopitishwa na Bunge la Katiba.

16.  UKOSEFU WA UADILIFU NA UZEMBE WA ZEC

Baraza Kuu la Uongozi linalaani upoteaji wa Takwimu za Uandikishaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa Majimbo ya Donge, Kitope, Bumbwini, Mfenesini na Bububu. Baraza Kuu linaitaka ZEC kuwaandikisha wananchi wote bila usumbufu waliyokuwemo ndani ya daftari ambazo takwimu zake zinasemekana zimefutika.

17.  KUHUSU MBINU ZA KUPUNGUZA MAJIMBO YA PEMBA

Baraza Kuu limejadili kwa kina uvumi na mbinu za ZEC kutaka kupunguza baadhi ya majimbo kwa upande wa Pemba na kuongeza majimbo kwa upande wa Unguja. Baraza Kuu linaipinga vikali dhana hii inayoweza kuturudisha kwenye siasa za uhasama katika kipindi hiki ambacho Zanzibar imeshaanza kutulia. Baraza Kuu linaitaka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na ZEC kutopunguza Majimbo ya Uchaguzi ya Pemba

18.  KUHUSU SHEREHE YA MIAKA 50 YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR

Baraza Kuu linaipongeza Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kutimiza Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar, na linaitaka kuendeleza maridhiano, mshikamano na umoja wa Kitaifa uliopo hivi sasa na kutumia umoja huo kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Baraza Kuu Linawataka Wazanzibari kutumia sherehe za Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar kuimarisha umoja wao na kuendelea kuondosha siasa za chuki zilizodumu kwa miaka mingi na linatoa wito kwa Wazanzibari na Watanzania wote na hususan wana CUF kushiriki kikamilifu katika kusheherkea miaka 50 ya Mapinduzi.

19.  KUHUSU MGOGORO WA CHADEMA

Baraza Kuu linatoa wito kwa CHADEMA kumaliza mgogoro wao ili kuweka nguvu kwenye Bunge la Katiba. Suala la kupata Katiba Mpya yenye misingi imara ya demokrasia na utawala bora linapaswa kupewa kipaumbele na kuwaunganisha viongozi wa CHADEMA katika kulisimamia. Kwa hali ilivyosasa na kama itaendelea kuwa hivyo, basi ni dhahiri kwamba nguvu kubwa ya CHADEMA itaelekezwa kwenye kushughulika na mgogoro wao, jambo ambalo litaathiri ushiriki wao katika mjadala wa Katiba kwenye Bunge la Katiba. Katika mchakato wa kupata katiba mpya CHADEMA ni miongoni mwa vyama vilivyotoa mchango mkubwa. Umoja wa CHADEMA unahitajika kuhakikisha kuwa Chama hicho kinaitumia fursa hii muhimu na adimu kwa maslahi ya taifa letu.

20.  WITO KWA VYAMA KUWEKA MASLAHI YA TAIFA KWENYE BUNGE LA KATIBA

Baraza Kuu linatoa wito kwa Vyama Vyenye Wabunge kuacha kupigania maslahi ya Vyama vyao wakati wa Mjadala wa Bunge la Katiba. Ni dhahiri kwamba Katiba inayoandikwa ni Katiba ya Nchi na si ya Chama chochote, hivyo ni muhimu kwa wabunge wa Bunge la Katiba kuwa Wazalendo, kwa kutoa michango itayowezesha kupatikana Katiba bora ya Nchi yetu badala ya kutoa michango itayowezesha kupatikana kwa Katiba yenye maslahi na Vyama vyetu.

MWISHO;
The Civic United Front (CUF-Chama Cha Wananchi) na viongozi wake inawahakikishia Watanzania wote kuwa Wabunge na Wawakilishi wa CUF watakaoingia katika Bunge la Katiba watakuwa wazalendo na waadilifu na wataweka mbele maslahi ya taifa letu na wananchi wa pande mbili za Muungano wetu ili tupate katiba yenye misingi imara ya demokrasia na utawala bora na itakayohakikisha kuwa raslimali na maliasili ya taifa letu inatumiwa kwa manufaa ya wananchi wote.
HAKI SAWA KWA WOTE.
Imetolewa na;
Baraza Kuu La Uongozi Taifa,                                                                                               Tarehe 24 Disemba 2013
PROF IBRAHIM HARUNA LIPUMBA                                                            MWENYEKITI WA CUF TAIFA.

No comments:

Post a Comment