TANGAZO


Saturday, July 27, 2013

TUME YA KUREKEBISHA SHERIA TANZANIA: MAPITIO YAANZA YA MFUMO WA SHERIA WA HUDUMA ZA JAMII KWA WAZEE

Ofisa Habari na Mawasiliano, Munir Shemweta toka Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, akizungumza na waandishi wa habari juu ya faida za kuimarishwa kwa mfumo wa sheria wa huduma za jamii kwa wazee utakaowezesha upatikanaji wa huduma muhimu za maisha kwa kundi hilo, Jijini Dar es Salaam. Katikati ni Ofisa Habari toka Idara ya Habari, Frank Mvungi na kulia ni Ofisa Sheria Mkuu wa Tume hiyo, Anjela Shila.
Ofisa Sheria Mkuu toka Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Anjela Shila (kulia), akisisitiza jambo juu ya faida za kuimarishwa kwa mfumo wa sheria wa huduma za jamii kwa wazee utakaowezesha upatikanaji wa huduma muhimu za maisha kwa kundi hilo, wakati wa mkutano na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam.
Katibu Msaidizi Elimu ya Sheria kwa Umma toka Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Agnes Mgeyekwa (kushoto), akitoa ufafafanuzi kuhusu namna tume hiyo, inavyotimiza majukumu yake katika kurekebisha sheria mbalimbali nchini, wakati wa mkutano na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam leo. Kulia ni Ofisa Habari na Mawasiliano wa tume hiyo, Munir Shemweta.
Katibu Msaidizi Elimu ya Sheria kwa Umma toka Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Agnes Mgeyekwa (kushoto), akitoa ufafafanuzi kuhusu namna tume hiyo, inavyotimiza majukumu yake katika kurekebisha sheria mbalimbali nchini, wakati wa mkutano na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam leo. Kulia ni Ofisa Habari na Mawasiliano wa tume hiyo, Munir Shemweta.

Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania imeanza kupitia mfumo wa sheria wa huduma za jamii kwa wazee (elderly social care) kwa nia ya kubaini mapungufu yaliyoko kwenye mfumo huo na kutoa mapendekezo  stahiki ili kuweza kuwa na mfumo mzuri wa sheria   utakaolenga ustawi na hifadhi kwa wazee wote waliohitimu miaka 60 na zaidi wa mijini na vijijini.
Wazee wanapofikia umri mkubwa, uwezo wao wa kujihusisha na shughuli mbalimbali hupungua na hivyo hushindwa kijihudumia mahitaji yao muhimu ya kila siku kama vile chakula, mavazi, malazi, pamoja na kushiriki katika shughuli mbalimbali za ujenzi wa taifa ziwe za kitamaduni, kijamii au kiuchumi.
Tume imeona kuna umuhimu wa kuimarisha mfumo wa sheria  wa huduma za jamii kwa wazee ili kuwezesha wao kupata huduma muhimu za maisha.   Pamoja na kuwa na Sera ya Taifa ya Wazee (National Ageing Policy, 2003) Tanzania haina sheria maalum katika eneo hili.   Sheria mbalimbali za mafao zinawagusa wazee wanaostaafu kazi serikalini na sekta binafsi ambao ni sehemu ndogo sana ya kundi la wazee wengi wanaokosa huduma muhimu za maisha.
Ikumbukwe kuwa wazee hawa ni wale waliotumikia taifa kwa nguvu na moyo wote kwenye ngazi mbalimbali wakati wakiwa na nguvu zao hivyo wanapokuwa wamezeeka ni muhimu wakawekewa mfumo bora wa kisheria ili kuhakikisha wanaishi maisha mazuri bila kujali kupungua kwa uwezo wao wa kujishughulisha katika nyanja mbalimbali.

Kwa sasa Tume inaendelea na rasimu ya awali ya kuangalia hali halisi ya Tanzania kuhusiana na suala zima la wazee ikiwemo mikataba ya kimataifa, mifumo ya kisheria na kijamii pamoja na sera na na baada ya hapo itatembelea mikoa mbalimbali ya Tanzania bara kwa nia ya kukusanya maoni ya wananchi juu ya mfumo huo wa kisheria.  Maoni hayo yatahusisha wazee wenyewe, maofisa kazi, afya, ustawi wa jamii, watendaji wa vijiji, taasisi zisizokuwa za kiserikali zinazojishughulisha na wazee pamoja na wananchi kwa ujumla.

Ni Matarajio ya Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania kuwa baada ya kukamilika kwa mapitio ya mfumo huo wa kisheria kuhusiana na huduma za jamii kwa wazee, Tume itakuja na mapendekezo ya kisheria na yasiyo ya kisheria ambayo yataleta tija kwa taifa kwa ujumla.
Kuhusu Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania

Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania ni Idara ya Serikali inayojitegemea chini ya Wizara ya Katiba na Sheria.  Ilianzishwa kwa mujibu wa sheria kupitia kifungu cha 3 cha Sheria ya Tume ya Kurekebisha Sheria, Namba 11 ya mwaka 1980.  Sheria hii kwa sasa ni Sura ya 171 ya Sheria za Tanzania kama sheria zilivyorekebishwa katika toleo la mwaka 2002.  

Majukumu ya Tume katika ujumla wake ni kutoa mapendekezo ya marekebisho ya Sheria mbalimbali kwa Serikali, kwa kutafiti na kutathmini maeneo yote ya sheria husika na kuyatolea mapendekezo kwa lengo la kuyaboresha.  Baada ya utafiti, Tume huwasilisha taarifa yake kwa Waziri anayehusika na masuala ya sheria.

Moja ya mafanikio ya Tume yaliyopatikana kutokana na mapendekezo ya Taarifa zake zinazopelekwa kwa Waziri anayehusika na masuala ya sheria ni pamoja na kutungwa kwa sheria mbalimbali ikiwa ni pamoja na:-

·         Marekebisho ya Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 1985 Kuhusu Kuwalipa Fidia Wahanga Wa Makosa Ya Jinai;
·         Kuchapishwa kwa Tangazo la Serikali Na. 192 la mwaka 1988 kuhusu Uharakishwaji wa Mashauri Mahakamani;
·         Mapitio ya Sheria ya Udhibiti wa Ubadilishaji wa Fedha za Kigeni;
·         Uanzishwaji wa Mfumo wa Wafungwa Kutumikia Sehemu ya Vifungo Nje ya Gereza;
·         Marekebisho Makubwa Yalifanywa Kwenye Sheria 28 Kati ya 40 Zilizopendekezwa na Tume ya Nyalali Ikiwa ni Sehemu ya Mapendekezo Yaliyotolewa na Tume ya Kurekebisha Sheria Baada ya Kusoma Taarifa Hiyo ya Tume ya Nyalali
·         Kutungwa kwa Sheria ya “Makosa ya Kujamiiana” Na. 4 ya 1998;’
·         Marekebisho ya Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Madai Ili Kutambua Utatuzi wa Migogoro kwa Njia za Usuluhishi;
·         Kutungwa kwa Sheria za Kazi za Mwaka  2004;
·         Kurekebishwa Sheria ya Ushahidi Ili Kutambua Ushahidi wa TEKNOHAMA (Electronic Evidence) Mwaka 2007;
·         Kutungwa kwa Sheria ya Vinasaba vya BinadamuMwaka 2009;
·         Kutungwa kwa Kanuni Mpya za Mahakama ya Rufaa (Court of Appeal Rules) za Mwaka 2009
·         Kutungwa kwa Sheria Zinazohusu Haki za Watu Wenye Ulemavu za Mwaka 2009;na
·         Kutungwa kwa Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009.

 Imetolewa na:

Munir Shemweta
Afisa Habari na Mawasiliano
TUME YA KUREKEBISHA SHERIA TANZANIA
27 JULAI 2013


No comments:

Post a Comment