TANGAZO


Wednesday, December 26, 2012

Padri apigwa risasi Zanzibar na watu wasiojulikana, aletwa jijini Dar es Salaam kwa matibabu

Padri Ambros Mkenda, akiwa katika hospitali ya Mnazi Mmoja, mjini Zanzibar, akipatiwa matibabu baada ya kupigwa risasi na watu wasiojulikana wakati akitaka kuingia ndani ya nyumba yake huko Mpendae visiwani Zanizibar.
Padri Ambros Mkenda wa Parokia ya Mpendae katika Kanisa Katoliki Mjini Zanzibar, amepigwa risasi na watu wasiojulikana nje ya nyumba yake majira ya saa 12 jioni jana, wakati akitokea kanisani. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Aziz Juma Mohammed, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo ambalo alisema Father amepigwa risasi na ameumizwa sehemu ya kichwa na amekuwa akitoka damu nyingi kichwani na tayari anapatiwa matibabu katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja, mjini Zanzibar.
 
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx
Taarifa zilizopatikana na www.bayana.blogspot.com, wakati wa mchana wa siku ya leo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), ni kwamba Padre huyo, ameletwa jijini Dar es Salaam na tayari anapatiwa matibabu katika kitengo cha dharura, akiwa chini ya uangalizi wa madaktari bingwa hospitalini hapo na hali yake inaendelea vizuri.
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Kamanda Aziz Juma Mohammed, alisema jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo, ili kubaini wahusika waliofanya uhalifu huo, na ni kwa madhumuni gani kabla ya kuchukuliwa hatua za kisheria.

“Sisi tunahesabu kuwa kitendo hiki ni kitendo cha kihalifu na tunawatafuta wahalifu waliofanya kitendo hiki kwa hivyo bado ni mapema kusema kwamba kitendo hiki kimefanywa na nani kwa kuwa bado uchunguzi wetu unaendelea na hadi sasa hakuna mtu tuliyemshika kuhusikana na tukio hili,” alisema Kamanda Aziz.

Kamanda Aziz akisimulia tukio hilo, alisema kuwa walipata taarifa majira ya saa 2 na kwenda katika eneo la tukio ambapo Father alikuwa akitokea kanisani na kutaka kuelekea nyumbani kwake wakati akiwa ndani ya gari ndipo aliposhambuliwa na watu wasiojulikana na kuanguka chini.

“Tumekuta mabaki ya risasi ndani ya gari lake na katika vioo vyake vya gari vimevunjika na tumekuta damu chini pale” alisema Kamanda.

Aidha, Kamanda Azizi alisema kuwa Father Ambros yeye ni mhasibu pale kanisani na hivyo mara nyingi watu wanaamini kwamba katika siku za krismass mara nyingi sadaka hukusanywa fedha nyingi na hivyo, wanaamini kwamba alikuwa na fedha mikononi na ndipo inawezekana waliamua kumpiga risasi wakitaka kuchukua fedha hizo.

Hata hivyo alisema uchunguzi wa awali ndio utakaoeleza ni suala gani lililopelekea kupigwa risasi lakini wanaendelea na uchunguzi huo, ambapo uchunguzi ndio utakaotoa sababu kamili ya tukio hilo.

Akizungumzia tukio hilo, Askofu Michael Hafidh wa Kanisa la Anglikan la Mkunazini, amesema wamesikitishwa na wamepokea kwa mshituko mkubwa tukio hilo, hasa kwa kuzingatia matukio kama hayo, hayajawahi kutokea ya kuwahujumu viongozi wa dini.

Alisema tukio hilo ni miongoni mwa matukio ya kushtusha na yanaashiria hali mbaya ya kiusalama na kuwaomba viongozi wa Serikali kuchukua hatua za tahadhari kubwa kwani matukio kama hayo, yameanza kutokea kwa viongozi wa dini ambapo mwanzo ilianzia kwa Sheikh Soraga na baadaye kutokea kwa Father Ambros.

“ Hii ni hali ya hatari katika nchi yetu na haipendezi, lakini Serikali lazima ijue sisi hatuwezi kujua wala hatuwezi kujilinda lakini Serikali inapaswa kutulinda sisi ndio wananchi wake,” alisema Askofu Hafidh.

Askofu Hafidh alisema kuwa hivi karibuni kumekuwepo na vipeperushi vilivyosambazwa na watu, vikiwatisha watu wenye imani ya kikristo ambapo alisema miongoni mwao walikuwa na khofu juu ya kusambazwa kwa vipeperushi hivyo na kuiomba Serikali iongeze ulinzi.

“Tumeona hivi vipeperushi na kwa kweli tulikuwa na khofu juu ya vipeperushi hivi, lakini ndio tunasema tunaelekea wapi katika maisha haya,” alisema Akofu Hafidh.
“Sisi hatuamini kwamba kuna kisasi kwa viongozi wa dini, lakini tunachukulia hilo ni tukio la kihalifu na pia hatuna vipeperushi vya aina yoyote vinavyoelezea kuwatisha viongozi wa dini kwa hivyo tunachukulia hayo ni matukio ya kihalifu na wala hatuamini kwamba matukio haya ni ya dini fulani,” alisema Kamanda Azizi.
Akielezea kuhusiana na hilo, Kamanda Aziz alisema jeshi la polisi limejipanga na kuzidisha ulinzi katika maeneo yote ya makanisa ambapo kumesambazwa polisi wa kutosha kwa kuwa wanajua wakati wa sherehe mambo ya kihalifu hujitokeza.
"Sisi kawaida huwa tunaweka ulinzi siku za sherehe zozote lakini kwanza makanisa yote yamewekwa ulinzi wa kutosha kabisa lakini wahalifu wanapotaka kufanya uhalifu huwezi kujua watatumia mbinu gani na saa ngapi na watafanya uhalifu huo wapi, lakini ulinzi upo wa kutosha” alisisitiza Kamanda Aziz.

No comments:

Post a Comment