TANGAZO


Tuesday, November 21, 2017

NCC YATAKIWA KUZINGATIA UBORA WA MIUNDOMBINU NCHINI

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Elias Kwandikwa akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kukaribishwa kwa mara ya kwanza kwa ajili ya kujitambulisha na kuongea na wafanyakazi wa Baraza la Taifa la Ujenzi (NCC), leo jijini Dar es Salaam 
Mtendaji Mkuu wa Baraza la Taifa la Ujenzi (NCC), Matiko Mturi (kulia), akizungumza na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta), Elias Kuandikwa mara baada ya kuripoti Ofisini leo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujitambulisha na kuongea na wafanyakazi wa baraza hilo.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, (Sekta
ya Ujenzi), Elias Kwandikwa akisaini kitabu cha wageni
mara baada ya kukaribishwa kwa mara ya kwanza kwa ajili
ya kujitambulisha na kuongea na wafanyakazi wa Baraza la
Taifa la Ujenzi (NCC) leo Jijini Dar es Salaam.Na Jacquiline Mrisho – Maelezo.
BARAZA la Taifa la Ujenzi (NCC) limetakiwa kuzingatia ubora katika kutekeleza kazi zake ili kuokoa fedha zinazotolewa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali nchini.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, (Sekta ya Ujenzi), Elias Kwandikwa alipokuwa akijitambulisha na kuongea kwa mara ya kwanza na Wafanyakazi wa Baraza hilo leo Jijini Dar es Salaam.

Kwandikwa amesema kuwa Taasisi hiyo ni muhimu na ina manufaa kwa nchi ingawa kuna maeneo ambayo yanahitaji kusukumwa zaidi ili kazi zinazofanywa zizidi kuleta tija zaidi kwa Taifa.

“Baraza hili ni kama jicho katika Wizara kwa sababu majukumu yake yamejikita katika kusimamia Sera, hivyo Wafanyakazi tunatakiwa tujikite zaidi katika kufanya kazi zinazoonyesha ubora wa hali ya juu”, alisema Kwandika.  

Akizungumzia juu ya upunguzaji wa gharama za ujenzi, Naibu Waziri amesema kuwa gharama za ujenzi zinabadilika mara kwa mara, hivyo ni lazima zichunguzwe ili ujenzi ufanyike kwa bei ndogo lakini uwe katika kiwango bora zaidi na fedha zinazobaki zitumike kwa shughuli nyingine.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa NCC, Matiko Mturi amesema ili kutekeleza majukumu yake kikamilifu, kwa mwaka huu wa fedha Baraza limejiwekea malengo mbalimbali yakiwemo kukusanya maoni ya Wadau na kuandaa kuhusu utendaji wake ili kufanya maboresho ya utoaji wa huduma na shughuli zinazotekelezwa na Baraza.

Malengo mengine ni kuandaa na kukamilisha Kanuni za utekelezaji washeria, kuratibu na kutoa mafunzo kwa Wadau, kutoa ushauri wa kiufundi na kutatua migogoro, kufanya ukaguzi wa miradi ya ujenzi inayotumia fedha za Umma pamoja na jitihada za kutunisha Mfuko wa Maendeleo ya Ujenzi.

“Katika kipindi cha kuanzia Julai hadi Oktoba mwaka huu, tumetoa ushauri mbalimbali ikiwa ni jukumu letu la msingi katika mradi wa ujenzi wa nyumba za kuishi za magomeni, tulitathmini usahihi wa idadi ya nondo katika ujenzi wa jengo la maabara iliyopo katika eneo la Mabibo, pia tulifanya tathmini ya thamani ya pesa katika jengo la dharura lililopo Makumbusho pamoja na tathmini ya kiufundi ya miradi inayotekelezwa kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara”, alisema Mturi

Baraza la Taifa la Ujenzi lilianza kazi rasmi mwaka 1981 likiwa na lengo kuu la kuboresha shughuli zinazofanywa na Sekta ya ujenzi ambapo jukumu lake kubwa ni kutoa uongozi wa kimkakati wa kuendeleza Sekta ya ujenzi kwa nia ya kuboresha uwezo wa Wataalam na Taasisi za ndani zinazotoa huduma katika Sekta ya ujenzi.

No comments:

Post a Comment