TANGAZO


Tuesday, April 11, 2017

JESHI LA ZIMA MOTO LAJIZATITI KUTOA HUDUMA BORA

Mkuu wa Jeshi la Zima Moto na Uokoaji, Kamishna Jenerali Thobias Andengenye akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam kuhusu mikakati ya Jeshi hilo kuboresha huduma wanazotoa katika maeneo yote hapa nchini ikiwa ni sehemu ya maboresho ya kiutendaji. Kushoto ni Afisa Habari Mwandamizi wa Idara ya Habari, Maelezo, Bw. Casmir Ndambalilo.(Picha zote na Frank Mvungi)
Mkuu wa Jeshi la Zima Moto na Uokoaji Kamishna Jenerali Thobias Andengenye akifafanua kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu umuhimu wa wananchi kutoa taarifa za matukio ya moto na ajali kwa wakati ili hatua za uokoaji ziweze kuchukuliwa kwa wakati muafaka, Kushoto ni Afisa Habari Mwandamizi wa Idara ya Habari, Maelezo, Bw.Casmir Ndambalilo na kulia ni Msemaji wa Jeshi hilo, Mrakibu Msaidizi Puyo Nzalayaimisi. 
Baadhi ya Waandishi wa habari wakifuatilia mkutano Mkuu wa Jeshi la Zima Moto na Uokoaji Kamishna Jenerali Thobias Andengenye  Leo Jijini Dar es Salaam kuhusu mikakati ya Jeshi hilo kuboresha huduma wanazotoa  kwa kushirikisha wadau wa Maendeleo.
Mkuu wa Jeshi la Zima Moto na Uokoaji nchini Kamishna Jenerali Thobias Andengenye.


Na Nuru Juma, Maelezo
JESHI la Zimamoto nchini limedhamiria kuimarisha huduma zake na limefanikiwa kutoa elimu kwa wananchi zaidi ya laki tisa juu ya namna ya kuzuia majanga ya moto na maafa.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam, Mkuu wa Jeshi la Zima Moto na Uokoaji nchini Kamishna Jenerali Thobias Andengenye alitoa wito kwa wananchi kuwasiliana na jeshi hilo mara tu panapotokea ajali au majanga ili kuharakisha uokoaji.

Kamishna Jenerali Andengenye alisema Jeshi hilo limeweza kutoa elimu kwa wananchi kupitia njia mbalimbali zikiwemo vituo vya redio, televisheni na magazeti ili kuwaelimisha zaidi kuhusu hatua za kuchukua mara yanapotokea majanga.

 “tunaendelea kutoa elimu kwa watanzania na toka Januari mwaka jana tumeweza kufikia takribani watu laki tisa na tunaendelea kuweka programu ya kuzifikia taasisi za elimu kama vile shule za msingi na sekondari.” alisema Andengenye.

Aliongeza kuwa Jeshi hilo limekuwa likifanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maeneo mbali mbali hususan majengo kuhakikisha kuwa hatua zote za tahadhari zinachukuliwa kuepusha na kukabiliana na ajali na majanga yanayoweza kutokea.

Kamishna Jenerali huyo alibainisha kuwa kwa sasa Jeshi lake limefanikiwa kuwa na vituo katika viwanja vyote vya ndege nchini na jitihada zaidi zinafanyika ili kuhakikisha Jeshi hilo linakuwa na ofisi zake katika maeneo yote nchini.

Alieleza pia kuwa katika kuongeza ufanisi, Jeshi hilo linatarajia kuajiri watumishi zaidi kulingana na mahitaji ya jeshi hilo hasa kwa kuzingatia vituo vipya ambavyo jeshi hilo inatarajia kuvifungua.

Kamishna Jenerali Andengenye aliwataka wananchi hasa madereva kutoa ushirikiano kwa jeshi lake kwa kuyapisha magari ya zima moto yawapo barabarani kwenda kutoa msaada kunakotokea.

No comments:

Post a Comment