TANGAZO


Friday, September 23, 2016

RC MAKONDA: JITOKEZENI KUPIMA AFYA ZENU

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Paul Makonda akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake jana kuhusu zoezi la upimaji wa afya litakaofanyika tarehe 24 na 25 Septemba katika viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi wa Huduma Shirikishi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Dkt. Praxeda Ogweyo, Daktari Bingwa wa magonjwa ya Figo Dkt. Onesmo Kisanga na Daktari Bingwa kutoka Hospitali ya Agakhan Dkt. Omar M. (Picha zote na Frank Shija, Maelezo)
Mmoja wa Madaktari Bingwa akifafunua jambo wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika katika Ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam jana. Madaktari hao kwa kushirikiana na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam wameandaa zoezi wa upimaji wa Afya kwa wakazi wa jiji hili litakalofanyika mapema wikiendi hii katika viwanja vya Mnazi Mmoja kuanzia saa 2:00 Asubuhi.

Na Frank Shija, MAELEZO.
23/09/2016.
WAKAZI wa jiji la Dar es Salaam na viunga vyake wametakiwa kujitokeza katika zoezi la upimaji wa Afya zao siku ya jumamosi na jumapili za tarehe 24 na 25 Septemba katika viwanja vya mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda alipokuwa akiongea na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusiana na zoezi hilo jana Jijini Dar es Salaam.

Makonda amesema kuwa Ofisi yake  imeandaa zoezi la kiafya kwa wanachi wote wa mkoa wa Dar es Salaam ili wapate fursa ya kujua afya zao ili waweze kujikinga na magonjwa yanayoweza kujitokeza, na kuepuka matumizi ya gharama kubwa za matibabu na kuzia vifo visivyo vya lazima.

“Natoa wito kwa wananchi wote wa Mkoa wa Dar es Salaam na viunga vyake wajitokeze kwa wingi siku za jumamosi tarehe 24 na jumapili tarehe 25 Septemba katika Viwanja vya Mnazi Mmoja kuanzia majira ya saa mbili asubuhi waje kuchunguza Afya zao, huduma hii itatolewa na Madaktari Bingwa bila malipo yoyote” Alisema Makonda.

Aliongeza kuwa upimaji huo umelenga zaidi magonjwa kumi makubwa yasiyopewa kipaumbele ambapo aliyataja kuwa ni pamoja na Shinikizo la Damu, Kisukari, Saratani ya Matiti, Saratani ya Shingo ya uzazi, Tezi Dume,Saratani ya ngozi kwa watu wenye Alibinism, na magonjwa mengiyo kadri ya uhitaji wa mwananchi.

Zoezi hilo halitakuwa na ubaguzi hivyo ni vyema mtanzania yeyote atakayekuwepo Jijini Dar es Salaam katika siku hizo za zoezi la upimaji, akatumia fursa hiyo kujipatia huduma ya kuchunguza hali ya Afya yake bila ya malipo.

Awali akizungumza katika kikao hicho Mganga Mkuu wa Manispaa ya Kinondoni Dkt. Aziz Msuya amesema kuwa watanzania wengi wamekuwa wanashindwa kupata huduma ya vipimo kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo gharama kubwa kwa baadhi ya vipimo na umbali wa mahali inapopatikana huduma husika.

Huduma hii ya upimaji wa Afya unafanyika ikiwa ni mara ya kwanza kwa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa kushirikiana na Madaktari Bingwa kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, Taasisi ya Moyo ya Jakaya Mrisho Kikwete, Hospitali za Rufaa za Mkoa wa Dar es Salaam, Hospitali ya Agakhan pamoja na Taasisi ya CCP Medicine.

No comments:

Post a Comment