TANGAZO


Tuesday, September 13, 2016

MAKALA: ZOEZI LA KUWAONDOA WATUMISHI WASIOSTAHILI KATIKA ORODHA YA MALIPO YA MISHAHARA

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angellah J. Kairuki (Mb) akitoa ufafanuzi wa masuala ya kiutumishi wakati wa kipindi cha TUNATEKELEZA kilichorushwa na Runinga ya Taifa (TBC-1). Kushoto ni muongozaji wa kipindi hicho Bi. Eshe Muhidin.

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angellah J. Kairuki (Mb) alisema hayo hivi karibuni katika kipindi cha mahojiano ya moja kwa moja katika Runinga ya Taifa (TBC) na kusisitiza waajiri wanawajibu wa kuondoa mtumishi yeyote asiyestahili mara moja.

“Tumefanya zoezi mahsusi kuwaondoa kwenye orodha ya malipo ya mishahara watumishi wasiostahili.  Watumishi wanaoondolewa ni wale walioacha kazi, kufukuzwa kazi, kumalizika kwa muda wa ajira ya mkataba na kugombea nafasi za kisiasa. Kuanzia tarehe 01 Machi, 2016 hadi tarehe 20 Agosti, 2016 jumla ya watumishi 16,127 wameondolewa na  wasingeondolewa kwa wakati  wangeisababishia Serikali hasara ya Shilingi 16,014,697,390 kwa mwezi mmoja” Mhe. Kairuki aliainisha.

Alisema hatua zinachukuliwa kwa wote waliobainika kuhusika katika suala hilo ambapo hadi  tarehe 20 Agosti, 2016 jumla ya watumishi 839 walifikishwa Polisi na TAKUKURU ili kutoa maelezo; na  uchunguzi unaendelea hatimaye hatua za kisheria zichukuliwe kulingana  wa ushahidi utakaopatikana.

Waziri Kairuki alisema lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba fedha zote zilizolipwa kwa watumishi wasiostahili zinarejeshwa Serikalini akibainisha kuwa toka mwezi Machi, 2016 hadi mwezi Julai, 2016 jumla fedha zilizorejeshwa ni Shilingi 14,403,046,089.27 na zoezi ni endelevu.

Waziri Kairuki alisema Mfumo wa Taarifa za Kiutumishi na Mishahara (HCIMS) unaimarishwa kulingana na mahitaji na kutaja maeneo yaliyoimarishwa ikiwamo; Uwezo wa kutambua na kuzuia kuajiriwa watu wenye majina yanayofanana; Kuongeza moduli ambayo inamwezesha mwajiri kufanya uhakiki wa watumishi kwa kutumia taarifa mbalimbali zikiwemo za Kitambulisho cha Taifa; Uwezo wa kuwaondoa kwenye orodha ya malipo ya mishahara watumishi waliofikisha umri wa kustaafu na ambao hawana mikataba; Kuongeza Moduli ya Utambuzi wa Kituo cha Kazi cha mtumishi (Service Delivery Point) na hilo limeanza kwa Idara za Afya, Elimu, Kilimo na Mifugo; na Wigo wa matumizi ya mfumo umepanuliwa ili kuwawezesha Wakuu wa Idara za Afya, Elimu (Sekondari/Msingi), Kilimo na Mifugo kutumia na kuona taarifa za watumishi walio chini yao.

Akiongea kuhusu mkakati wa kuboresha Maadili katika Utumishi wa Umma alisema pamoja na mambo mengine Serikali  inasimamia kukuza uelewa wa Maadili kwa Watumishi wa Umma kupitia mafunzo na kuendeleza ushiriki wa Asasi za Kiraia (AZAKI) katika kuhamasisha wananchi kuzingatia maadili na kuacha kutoa vishawishi kwa watoa huduma. Pia, kuhakikisha kila Taasisi ya Umma ina Mkataba wa Huduma kwa Mteja na dawati la kupokea, kushughulikia malalamiko na kutoa mrejesho kwa wananchi.

Waziri Kariuki aliongeza pamoja na ofisi yake kuhakikisha Watumishi  wa Umma wanatoa Kiapo cha Ahadi ya Uadilifu na kusimamia viapo hivyo, pia inaandaa Mfumo wa Kielektroniki unaojulikana kama “Watumishi Portal” ambao utakuwa na moduli ya kupokea malalamiko, maoni na kero mbalimbali kutoka kwa Watumishi wa Umma na kuhamasisha Taasisi za Umma kuwa na kituo mahususi cha utoaji huduma (One Stop Service Centre) ili kupunguza kero kwa wananchi wanaofuata huduma.


Eneo la Uwajibikaje hali ikoje?
Waziri Kariuki alisema Serikali imekuwa na utaratibu wa kupima utendaji wa Mtumishi Mmoja mmoja kwa kutumia Mfumo wa Wazi wa Mapitio na Tathmini ya Utendaji Kazi (OPRAS).

Hata hivyo, alisema “Serikali inalenga kuimarisha mfumo wa uwajibikaji katika ngazi ya Taasisi ili kuhakikisha Taasisi za Umma zinatekeleza majukumu yake ipasavyo kwa kuanzisha Mfumo wa Mikataba ya Utendaji Kazi katika Taasisi zote za Umma kuanzia mwaka wa fedha 2017/18”.
Alifafanua kuwa Mkataba huo ni makubaliano ya kimaandishi kati ya Taasisi za Umma na Serikali ambayo yatatekelezwa na Taasisi husika katika kipindi cha mwaka mmoja na Mkataba utajikita katika kupanga na kupima utendaji wa Taasisi na utakuwa na malengo, shabaha, vigezo na viashiria vya utendaji ambavyo vitatekelezwa na Taasisi katika mwaka  husika.

Waziri Kairuki alianisha kuwa Mkataba huo utaainisha wajibu wa Serikali katika kuwezesha Taasisi kufikia malengo na shabaha na utekelezaji wake utafanyiwa tathmini kila mwisho wa mwaka na matokeo yake kutangazwa kwa umma.
Miongoni mwa faida za mfumo huo ni kuziwezesha Taasisi za Umma kuimarisha uchaguzi wa vipaumbele katika ngazi ya Taasisi na upangaji mipango ya utekelezaji kila mwaka; kuimarisha ufuatiliaji na upimaji utendaji kazi; na kuimarisha uwajibikaji na uwazi.

Usimamizi wa Maadili kwa viongozi wa Umma ukoje?
Waziri Kairuki alieleza kumekuwepo na malalamiko ya ukiukwaji wa maadili dhidi ya viongozi wa Umma na hadi kufikia Agosti 2016, malalamiko 200 yalipokelewa ambapo kati ya malalamiko hayo, malalamiko 142 yalihusu Sheria ya Maadili na malalamiko 58 hayakuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

“Uchunguzi wa awali umefanyika kwa malalamiko 11 yanayohusu ukiukwaji wa Sheria ya Maadili. Aidha, malalamiko 58 ambayo hayakuhusu ukiukwaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma walalamikaji walipewa ushauri na mengine yalielekezwa kwenye mamlaka zinazohusika. Malalamiko hayo yalihusu pamoja na mambo mengine masuala ya rushwa na migogoro ya ardhi” Mhe. Kairuki alifafanua. 

Aliongeza hatua zinazochukuliwa dhidi ya Viongozi wa Umma wanaothibitika kukiuka Sheria ya maadili ni pamoja na kufikishwa katika Baraza la Maadili lililoundwa kwa mujibu wa kifungu cha 26 cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ili kufanya uchunguzi wa kina.

Kuanzia mwaka 2010/11 hadi 2015/16 jumla ya mashauri 69 ya ukiukwaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma yalifanyiwa kazi na Baraza la Maadili, kati yake mashauri 38 yalithibitika kukiuka Sheria ya Maadili na Viongozi na wahusika kupewa adhabu mbalimbali ikijumuisha Onyo (12), Onyo Kali (19), Faini ya shilingi milioni moja (1), kushushwa cheo (3) na kuondolewa katika wadhifa (3).

Waziri Kairuki mwenye dhamana na Utumishi wa Umma na Utawala Bora nchini alisema miongoni mwa mashauri hayo yalihusu kutowasilisha Tamko la Rasilimali na Madeni, kutoa tamko la uongo, matumizi mabaya ya madaraka na mali ya umma na mpaka wakati huu  Sekretarieti ya Maadili ina malalamiko 12 yakufikisha mbele ya Baraza la Maadili.

Pamoja na hayo, alisema ipo mikakati ambayo Serikali inaitumia katika kukuza maadili ya viongozi wa umma nchini ikiwamo kutoa elimu kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ambapo katika mwaka wa fedha 2015/16, Viongozi wa Umma 7,442 walipatiwa elimu kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Mgongano wa Maslahi na Maadili ya Utumishi wa Umma.

Hali ikoje kuhusu Nyaraka na Siri za Serikali?
Waziri Kairuki alisema kwa mujibu wa Sheria ya Usalama wa Taifa ya mwaka 1970 na Sheria ya Kumbukumbu na Nyaraka ya Mwaka 2002 ni kosa la jinai kwa mtu yeyote kutoa au kuvujisha taarifa zenye zuio kwa wasio walengwa.

Aliainisha kuwa Serikali  imekuwa ikichukua hatua kuhusu hilo ikiwamo kuwashitaki wahusika mahakamani kwa kuvunja sheria, Kuwachukulia hatua za kinidhamu watumishi wa Umma na hatimaye kufukuzwa kazi, kushushwa cheo na kupunguziwa mshahara, Kutoa elimu kwa watumishi na wananchi juu ya Sheria na Kanuni zinazosimamia masuala ya utoaji wa taarifa, nyaraka na siri za Serikali.  

Hatua nyingine zinazochukuliwa ni Kuendelea kusimamia Sheria ya Usalama wa Taifa Na. 3 ya mwaka 1970 na Sheria ya Kumbukumbu na Nyaraka ya Mwaka 2002, Mwongozo wa Matumizi Bora, Sahihi na Salama ya Vifaa vya TEHAMA wa mwaka 2012 na Kanuni za Maadili ya Utendaji katika Utumishi wa Umma za mwaka 2005, pia kuimarisha matumizi na usalama wa mifumo ya TEHAMA ili kudhibiti uvujaji wa nyaraka na siri za Serikali kupitia mitandao ya kijamii.

Matumizi ya TEHAMA yakoje Serikalini?
Waziri Kairuki alisema matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yamepunguza gharama za uendeshaji wa kazi mbalimbali za Serikali akitolea mfano wa uendeshaji wa semina na mikutano kwa njia ya mawasiliano ya video (Video Conference) ambapo mikutano ya Serikali hufanyika kwa gharama nafuu kwani haimlazimu mshiriki kusafiri; na uendeshaji wa mafunzo ambapo mwezeshaji mmoja anaweza kuendesha mafunzo kwa watendaji katika zaidi ya kituo kimoja.

Alisema hadi sasa huduma hii ipo katika Mikoa yote isipokuwa mikoa ya Geita, Katavi, Njombe, Simiyu na Songwe ambayo Serikali ipo katika mkakati wa kufikisha huduma hiyo, pamoja na hilo taasisi 77 zimeunganishwa kwenye Mtandao wa Mawasiliano ya Serikali (GovNet) hivyo kufanya mawasiliano kulipia muda wa maongezi.

“Azma ya Serikali  ni kutatua kero  zinazowakabili wananchi katika kupata huduma mbalimbali katika Taasisi za Umma” Waziri Kairuki alisema na kuelezea utekelezaji wa miradi kama Mawasiliano ya ndani ya ofisi (electronic Office) kupitia Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Wakala ya Serikali Mtandao (eGA), Utunzaji wa Kumbukumbu na Nyaraka (electronic Records) kupitia Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Ununuzi wa Umma kwa njia ya Mtandao (e-Procurement system) kupitia PPRA na MSD, na Huduma za Kitabibu kwa njia ya mtandao (Telemedicine system) kupitia Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Mapambano dhidi ya rushwa
Waziri Kairuki alieleza Serikali imekuwa ikichukua hatua katika kuzuia na kupambana na rushwa nchini mfano kwa kufuatilia fedha za Miradi ya Maendeleo kupitia Ofisi za Kanda za TAKUKURU kwa lengo la kuhakikisha thamani ya miradi inayotekelezwa inaendana na kiasi cha fedha kilichotolewa ambapo ufuatiliaji huo umeiwezesha Serikali kuokoa kiasi cha Shilingi Bilioni 39.34.

“Tumewasilisha majalada 297 kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) kwa ajili ya kuombewa kibali cha mashitaka ambapo majalada 229 yalipata kibali cha kuwafikisha watuhumiwa mahakamani” Waziri Kairuki alifafanua.

Aliongeza mikakati ya serikali ni pamoja na  kuhuisha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11 ya 2007 ili kujumuisha makosa ya uhujumu uchumi na kutaifisha mali zilizopatikana kwa njia ya Rushwa na Ufisadi.

Kuhusu kaya masikini hali hali ikoje?
Waziri Kairuki alisema Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini ambao utachukua miaka kumi unatekelezwa katika Halmashauri zote za Tanzania Bara pamoja na Zanzibar.

“Katika kipindi cha miaka minne mpango umetekelezwa Vijiji, Mitaa na Shehia 9,960 ambayo ni sawa na wastani wa asilimia 70. Kaya 1,358,268 zimetambuliwa ambapo kati ya hizo, Kaya 1,110,377 zimeandikishwa” Waziri Kairuki alisena na kuongeza kaya 1,110,377 zimehawilishiwa fedha kwa kulipwa ruzuku katika awamu 16 ili kuziwezesha kuwekeza katika lishe, afya na elimu.

Mpango wa Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi unatekelezeka?
Waziri Kairuki alisema Mpango wa Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi (Open Government Partnership) ulianza kutekelezwa nchini toka mwaka 2012/13, na umejikita katika kuweka uwazi zaidi katika uendeshaji wa shughuli za Serikali; Ushirikishwaji wa Sekta za Umma na Binafsi katika utekelezaji wa Mpango; Uwajibikaji wa Serikali kwa Wananchi; Matumizi ya Teknolojia na Ubunifu; na Mapambano dhidi ya Rushwa.

Alisema miongoni mwa yaliyofanyika ni pamoja na kuongezeka kwa uwazi kuhusu bajeti ya Serikali kwa kuandaa kijitabu cha  “Citizen budget” kilichoandaliwa kwa Kiswahili na  lugha rahisi kwa kuchapishwa kwenye tovuti ya Wizara ya Fedha na Mipango. Pia, taarifa za utekelezaji za sekta za kipaumbele Afya, Elimu na Maji kuchapishwa katika Tovuti za sekta hizo na kukamilika kwa zoezi la upembuzi yakinifu wa Takwimu Huria (Open Data) ili  kuongeza uwazi wa takwimu na taarifa mbalimbali;

Waziri Kairuki alisisitiza kuwa Serikali inaendelea kutekeleza Mpango wa Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi kwa mikakati mbalimbali ikiwamo, kuendelea na utekelezaji wa kuwa na uwazi katika bajeti ya Serikali kwa kuweka taarifa za bajeti kwenye tovuti mbalimbali kwa lugha nyepesi na kwa Kiswahili na kuimarisha mfumo wa Takwimu Huria ambayo utarahisha wadau mbalimbali kupata takwimu zinazohusu masuala mbalimbali hususan Afya, na Elimu.

Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora (OR-MUUUB) ina majukumu ya kuandaa na kusimamia utekelezaji wa Sera za Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma; Taratibu, Miundo na Mifumo ya Utoaji Huduma; Uendelezaji Rasilimaliwatu; Utunzaji wa Kumbukumbu na Nyaraka katika Utumishi wa Umma. Aidha, Ofisi hii inasimamia maadili ya watumishi na viongozi wa umma; mapambano dhidi ya  rushwa; Mfuko wa Maendeleo ya Jamii; Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge; Mfuko wa Rais wa Kujitegemea; na Taasisi ya Uongozi.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma.

No comments:

Post a Comment