Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli, akifunua pazi ili kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa Barabara ya juu makutano ya Tazara jijini Dar es Salaam leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli, akifungua ramani ya mradi wa Barabara ya juu makutano ya Tazara kuashiria ufunguzi rasmi na kuanza kwa ujenzi wa mradi huo Tazara jijini Dar es Salaam leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli, akipokea maelekezo kuhusu mradi wa ujenzi wa Barabara za juu eneo la makutano la Tazara kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wakala wa barabara (TANROADS) Mhandisi Patrick Mfugale katika ufunguzi rasmi wa mradi huo jijini Dar es Salaam leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli, akikata utepe kuashiria ufunguzi rasmi na kuanza kwa ujenzi wa mradi wa Barabara ya juu makutano ya barabara za Nyerere na Mandela, eneo la Tazara jijini Dar es Salaam leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli, akiwa katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbaliwa wa Kitaifa na Kimataifa wakati wa ufunguzi rasmi na kuanza kwa ujenzi wa mradi wa barabara ya juu katika makutano ya Tazara jijini Dar es Salaam leo.
Na Lorietha Laurence-Maelezo
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dk. John Pombe Magufuli ameweka jiwe la msingi ikiwa ni ufunguzi rasmi wa ujenzi wa mradi wa barabara za juu (fly over) katika eneo la tazara utakaosaidia kupunguza msongamano wa foleni katika jiji la Dar es Salaam kwa asilimia 80.
Akizungumza wakati wa hafla hizo Mhe.Dk.magufuli ameeleza kuwa mradi unakadiriwa kugharimu kiasi cha shilingi, Bilioni 100, na unatarajiwa kukamilika mwaka 2018 huku akiwataka wananchi kutunza miundombinu kwa kuhakikisha jiji linakuwa safi na lenye kuvutia.
"Mradi huu ni kwa ajili ya maendeleo ya watanzania hivyo ni jukumu letu sotu kuutunza ili udumu ukizingatia fedha hizi za mradi zimetokana na walipakodi wa Japani wameamua kuleta kwetu hii ishara ya ushirikiano mzuri kwetu,"alisema.
Aidha aliongeza kuwa mradi huu umeshirikisha serikali ya Tanzania na ile ya Japani amabayo imechangia kiasi cha Bilion 93.44 huku Tanzania ikichangia shilingi Bilion 8.36.
Anaongeza na kueleza kuwa lengo la mradi huu ni kuhakikisha kero ya foleni inapungua kama si kwisha kabisa ikiwa ni pamoja na kuokoa muda wa usafirishaji kutoka kutumia dakika 45 mpaka dakika 10 pale mradi utakapokamilika.
Mradi huu wa barabara za juu utatengeneza ajira kwa vijana wa kitanzania kwa kuwataka kuitumia fursa hiyo vyema kwa kuwa waaminifu katika ajira hizo ili kusaidia kumaliza mradi huo kwa wakati.
"Tuna imani kuwa kazi itafanyika kwa haraka maana hakuna sababu kwa kampuni kubwa kutoka japani ambayo inatengeneza barabara kubwa kuchukua muda mrefu kumaliza ujenzi hivyo bora umalizike haraka na watanzania waone matunda yake,"alisema Mhe. Dk.Magufuli.
Dk. Magufuli aliongeza kuwa serikali ina mpango mzuri katika kuleta maendeleo ambapo kuna miradi mingine mingi inafanyika ikiwemo kujenga barabara nyingine za kawaida za njia sita zenye kilomita 128 zitakazoanzia daraja la Kigamboni hadi Chalinze na za juu tano tayari wakandarasi 13 wameshajitokeza kushindania zabuni .
Vilevile ameeleza kuwa katika bajeti ijayo ya mwaka wa fedha wa 2016/2017 kiasi cha Trilioni 1 kitatengwa kwa ajili ya mradi wa kujenga reli ya kati kutoka Dar es Salaam kwenda nchi za jirani ili kurahisisha usafirishaji wa bidhaa mbalimbali zinazopitia Bandarini .
Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa amesema kuwa kwa kiasi kikubwa kumalizika kwa ujenzi wa mradi wa barabara hizo za juu 'Fly Overs' kutasaidia kuokoa kiasi kikubwa cha fedha kilichokuwa kikipotea kutokana na kutumia muda mwingi katika msongamano wa foleni.
Katika hatua nyingine Rais alisema fedha za miradi ya maendeleo zimeongezeka kutoka asilimia 27 hadi kufikia 40 na kuwaomba makatibu wakuu na watumishi wa umma kuwa wavumilivu kwa kuwa fedha za safari, posho na chai zitapelekwa kwenye miradi hiyo kwa ajili ya maendeleo ya taifa.
"Nawaomba makatibu wakuu na watumishi kujifunga mkanda katika kipindi hiki ili tuweze kufikia malengo kwa kuelekeza fedha za chai,safari na posho katika miradi ya maendeleo ikiwemo kufufua shirika la dnege la Tanzania kwa kununua ndege mpya tatu “alisema Mhe. Magufuli.
Watanzania wamechoka kuona uchungu hivyo tuwafanye waone furaha, tubadilike ili fedha ziweze kurudi kwa wananchi wa chini, naamini wote tunalilia maendeleo hivyo tushirikiane na vyama vyote katika kuleta maendeleo,"aliongeza.
Mtendaji Mkuu wa Tanroads, Mhandisi Patriki Mfugale alisema lengo la mradi huo ni kupunguza msongamano wa magari katika barabara ya Mandela na Nyerere kwa kufungua njia nne ili magari yasisimame kwenye foleni katika makutano hayo.
Naye Balozi wa Japani Nchini Tanzania, Balozi Masaharu Yoshida amesema Ushirikiano wa Tanzania na Japani umeanza tangu mwaka 1960 na utaendelea kuwepo ambapo mradi huu ni kiashiria mojawapo cha kudhibitisha hilo.

No comments:
Post a Comment