Katibu wa Chama cha Mchezo wa Chess
Tanzania (TCA) Bw. Nurdin Hassuji ambaye pia ni Bingwa wa Taifa wa mchezo huo
akiongea na waandishi wa Habari hawapo pichani kuhusu mashindano ya mtu mmoja
mmoja ya ukanda wa Afrika 4.2 yajulikanayo kama (2016 Africa Zone 4.2
Individual Chess Championship), kulia ni Mwenyekiti wa Chama hicho Bw. Geofrey Mwanyika.
Na Ally Daud- BMT
MASHINDANO ya mchezo wa chessi
yanayojulikana kama mashindano ya mtu mmoja mmoja ya ukanda wa Afrika 4.2 (2016
Africa Zone 4.2 Individual Chess Championship) yanatarajiwa kuanza tarehe 23 mwezi huu mpaka tarehe 30 April
mwaka huu hapa jijini Dar es Salaam.
Akizungumza hayo mbele ya waandishi wa
habari Mwenyekiti wa chama cha mchezo huo nchini (TCA) Bw. Geofrey Mwanyika
amesema kuwa michuano hiyo iyafanyika katika Hoteli ya Peacock jijini Dar es
salaam Tanzania ikiwa mwenyeji wa mashindano hayo.
Aidha Bw. Mwanyika ameinisha nchi ambazo
zimeleta washiriki wake ni Uganda, Kenya, Rwanda, Burundi, Djibout,
Eritrea,Somalia,Ethiopia, Sudan Kusini na wenyeji Tanzania.
“Jumla ya washiriki 32 watachuana katika
mashindano hayo ambayo yamegawanyika katika makundi mawili ya Wanaume na
Wanawake na kati ya nchi hizo ambazo zinashiriki Sudan na Seychells
hazijathibitisha kushiriki”. Aliongeza Bw. Mwanyika.
Kwa upande wa Katibu wa TCA Bw. Nurdin Hassuji ambaye pia ni Bingwa wa
Taifa wa mchezo huo amesema kuwa zawadi za washindi ni Dola 4500 za Kimarekani ambazo zitagawanywa kwa
watakaoshinda.
Aidha Bw. Hassuji amewataka wadau wa
Michezo na waandishi wa habari
kujitokeza siku hiyo ili kuipa sapoti timu yao na kuutangaza mchezo ujulikane
na kupendwa zaidi nchini.
Mbali
na hayo Bw. Hassuji amesema kuwa mchezo huo wameupa kipaumbele na kwenda
kuufundisha mashuleni kwa sababu inawasaidia wanafunzi kuweza kufikiri kwa
haraka zaidi na kufanya mwanafunzi awe mwepesi kwenye kupambanua mambo.

No comments:
Post a Comment