TANGAZO


Sunday, November 29, 2015

Chama cha Washirika -Wauguzi Tanzania kukutana Desemba 12, 2015 jijini Dar es Salaam kujadili maendeleo na changamoto zao

Ofisa Ushirika wa Wilaya ya Kinondoni jijini  Dar es Salaam, Omary Mkamba (kulia), akimkabidhi cheti cha Usajili wa Chama cha Ushirika -Wauguzi Tanzania  (Tanna Saccos Ltd) , Mwenyekiti wa chama hicho, Kapteni Adam Leyna katika mkutano uliofanyika hivi karibuni. Mkamba ni mlezi wa chama hicho.
Mwenyekiti wa chama hicho, Kapteni Adam Leyna (katikati), akizungumza na wanachama wapya waliojiunga na chama hicho mkoani Kagera.
Wanachama wakijadiliana.
Wanachama wakiwa katika picha ya pamoja wakiwa wamevalia fulana rasmi mkoani Kagera
Viongozi wa chama hicho na wanachama wakiwa katika picha ya pamoja.

Na Dotto Mwaibale
CHAMA cha Washirika-Wauguzi  Tanzania (Tanna Saccos Ltd) kinatarajia kujadili mafanikio na changamoto zao mbalimbali katika mkutano wao mkuu , utakaofanyika Desemba 12, mwaka huu jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Tanna Saccos Ltd, Kapteni Adam  Leyna alisema mkutano huo ni muhimu sana kwao kwani unawakutanisha wauguzi washirika nchi nzima na kuweza kujadili mafanikio, changamoto mbalimbali na maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

"Ni mkutano muhimu sana kwetu kwani unatusaidia kubadilishana uzoefu wa ushirika kutoka kwa washirika wenzetu kama Ngome Saccos, Walimu Saccos na Magereza Saccos na kujua changamoto zetu ikiwa ni pamoja na kuzitafutia ufumbuzi' alisema Leyna.

Aliongeza kuwa mkutano huo ambao utafanyika Ukumbi wa Makuti katika Kambi ya Jeshi la Kujenga Taifa Mgulani ni mikutano ambayo hufanyika kila mwaka ili kuzungumzia maendeleo ya chama na uboreshaji wa uchumi wa muuguzi na ustawi wa  jamii kwa ujumla.

Leyna alisema pamoja na mambo mengine katika mkutano huo watajadili taarifa ya maendeleo ya chama na kuweka mpango kazi wa kutekeleza mwaka wa fedha 2016.

Mwenyekiti huyo ametumia fursa hiyo kuwaomba wauguzi washirika wa tanna saccos ltd kujitokeza kwa wingi katika mkutano huo muhimu kwao.

Chama cha Ushirika -Wauguzi Tanzania (Tanna Saccos Ltd)  ni chama cha ushirika kinacho waunganisha wauguzi na wakunga Tanzania ambacho kinasimamia utoaji wa mikopo, elimu ya ujasiriamali na maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wauguzi.
(Imeandaliwa na Dotto Mwaibale)

No comments:

Post a Comment