TANGAZO


Friday, March 6, 2015

Chanjo ya Ebola kujaribiwa Guinea

Margaret Chan Mkurugenzi mkuu wa WHO
Shirika la afya duniani WHO pamoja na wadau wake, mwishoni mwa wiki hii wanatarajia kuanza majaribio ya ufanisi wa chanjo dhidi ya Ebola nchini Guinea.
Chanjo hiyo aina ya VSV-EBOV imetengenezwa na wakala wa afya ya umma nchini Canada ambapo imeelezwa chanjo nyingine ya pili itaanzishiwa majaribio kadri shehena ya kutosha itakapo patikana.
Mkurugenzi Mkuu wa WHO Dkt.Margaret Chan amesema majaribio yatafanyika kwenye maeneo ya Basse Guinée ambayo ndio yameathirika zaidi na Ebola kwa sasa nchini Guinea na utoaji wake utaanzia kwa wagonjwa wapya na wale wote ambao wamekuwa karibu nao.
Lengo la jaribio la sasa ni kutathmini iwapo chanjo hiyo itawapatia kinga dhidi ya Ebola watu waliokuwa na makaribiano na mgonjwa na pili iwapo utoaji wa chanjo utajenga kinga kwa wale waliopatiwa na hivyo kuzuia maambukizi zaidi.
WHO imesema imejitahidi kwa dhati kuhamasisha nchi zilizoathirika na ugonjwa huo pamoja na wadau ili kuendeleza mbinu za kinga na iwapo chanjo hiyo itafaa itakuwa ni hatua ya kwanza ya kinga dhidi ya Ebola.
Wadau wanaoshirikiana na WHO kwenye majaribio hayo ya chanjo ni pamoja na wizara ya afya ya Guinea, madaktari wasio na mipaka, MSF na taasisi ya afya ya umma, Norway.

No comments:

Post a Comment