Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mecki Sadiki akizungumza na waandishi wa habari.
Ndugu wananchi wa Mkoa wa
Dar es Salaam,
Nachukua fursa hii kuwaarifu kuhusu maadhimisho ya wiki
ya Sheria itakayofanyika Mkoani Dar es Salaam na Kama mnavyofahamu Mahakama
huadhimisha kila Mwaka siku ya Sheria ambayo huashiria mwanzo wa shughuli za
Mahakama katika Mwaka husika. Kwa Mwaka huu wa 2015, utaratibu wa kuadhimisha
siku ya Sheria umebadilika. Badala ya kuadhimishwa siku moja, sasa imeonekana
ni busara maadhimisho hayo yakatanguliwa na maonyesho ya shughuli mbalimbali zinazofanywa
na Mahakama kwa siku tano kabla ya maadhimisho ya kilele cha siku ya Sheria.
Ndugu wananchi,
Lengo
la Maonyesho hayo ni kutoa fursa pana zaidi kwa wananchi kukifahamu chombo chao
cha Mahakama na shughuli zake. Aidha, wananchi watapata fursa ya kuelimishwa
juu ya mambo mbalimbali ya kisheria na
kujibiwa dukuduku zao hususani kwenye masuala ya kisheria na taratibu zinazotakiwa
kufuatwa katika ngazi mbalimbali za kimahakama
Ndugu wananchi,
Mwaka huu wa 2015 Wiki ya Sheria itaadhimishwa kuanzia tarehe 30/01/2015 kwa kufanya
maonyesho katika Viwanja vya Mnazi Mmoja hadi tarehe 03/02/2015 na Kilele cha
siku ya Sheria kitakuwa tarehe 04/02/2015 katika kiwanja cha Mahakama kilichopo
Mtaa wa Chimala karibu na Hospitali ya
Saratani ya Taifa “Ocean Road ”.
Ndugu wananchi,
Wiki
ya Sheria itazinduliwa rasmi na Rais wetu Mstaafu wa Awamu ya pili Mhe. Ally
Hassan Mwinyi baada ya kuongoza matembezi ambayo yataanzia Viwanja vya Mahakama
ya Hakimu Mkazi Kisutu kwenda Mnazi Mmoja kupitia barabara za Serena - Ohio , Gymkhana – Obama ,
Ikulu, Mahakama ya Biashara, Kivukoni, Sokoine, Railway, Nkurumah, Lumumba, Mkunguni
hadi Mnazi Mmoja, siku ya tarehe 01/02/2015 kuanzia saa 12.00 Asubuhi. Natoa
wito kwa wananchi wa fani mbalimbali kujitokeza kwa wingi katika matembezi
hayo.
Ndugu Wananchi,
Wananchi
wa Mkoa wa Dar es Salaam na Mikoa ya Jirani mnaombwa kujitokeza kwa wingi
katika Maonesho yatakayofanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja ili kupata
maelekezo ya kina na yenye ufasaha
kuhusu shughuli za Mahakama ya Tanzania na utoaji wa haki kwa wakati.
Aidha,
Napenda nitoe rai kwa wamiliki wa vyombo vya usafiri kuelekeza magari yao ya
abiria kwenda Uwanja wa Mnazi Mmoja ili
kurahisisha usafiri kwa wananchi, na ninarudia kuwaomba wananchi kujitokeza kwa
wingi katika kushiriki kwenye Maonesho hayo kwani hii ni fursa pekee kwa
wananchi kutambua haki zao za msingi kwa mujibu wa Sheria.
Asanteni kwa kunisikiliza.
Saidi Meck Sadiki
MKUU WA MKOA WA
DAR ES SALAAM
29/1/2015


No comments:
Post a Comment