TANGAZO


Saturday, October 26, 2013

Kamanda mstaafu wa Usalama Barabarani, James Kombe

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama awaongoza waombolezaji kwenye mazishi


Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, (katikati), Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Robert Boaz (kulia) na Kaimu Kamanda, Mkoa wa Kilimanjaro, Koka Moita wakiwa katika ibada ya maziko ya aliyekuwa Kamanda wa Usalama Barabarani, James Kombe, iliyofanyika leo, nyumbani kwake Msae, Mwika, mkoani Kilimanjaro. (Picha na Amina Mbwambo)

Na Amina Mbwambo, Moshi
MKUU wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, leo amewaongoza maelfu ya waombolezaji katika mazishi ya aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha Usalama Barabarani, Kamishna mstaafu, James Kombe (63), aliyefariki dunia October 21, mwaka huu katika Hospitali ya Ocean Road, jijini Dar es Salaam baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Kombe aliyeitumikia Jeshi la Polisi kwa muda wa miaka 24, katika
nyadhifa mbalimbali, alizikwa jana saa 9:40, alasiri, Nyumbani kwake katika kijiji cha Msae, Kata ya Mwika, Jimbo la Vunjo, Wilaya ya Moshi Vijijini, mkoani Kilimanjaro, baada ya ibada ya maziko iliyofanyika katika Usharika wa Msae-Lyakrima na kuongozwa na Askofu Mkuu wa KKKT, Dayosisi ya Kaskazini, Dk. Martin Shao.

Akitoa Salamu za Rambirambi, Gama alisema serikali imeguswa na msiba huo huku akimuelezea Marehemu Kombe kama mtu muadilifu, mwaminifu na mtu asiyekuwa na ubinafsi na mzalendo aliyeitumikia Taifa lake kwa nguvu zake zote hadi dakika za mwisho za uhai wake.

“Ni kweli mazingira yetu kikazi yanatofautiana, lakini ni wazi kuwa kuna mengi ya kujifunza na kujivunia kutoka kwa Kamishna Kombe enzi za uhai wake, Marehemu ameacha historia iliyotukuka nyuma yake, alikuwa ni mtu mwadilifu sana, mwaminifu, mzalendo na mchapa kazi aliyejitoleakulitumikia Jeshi la Polisi na Taifa kwa ujumla,” alisema Gama.

Kuhusu swala la uwajibikaji na utendaji kazi, Gama alisema wananchi wengi kwa sasa wanashindwa kufanya kazi za maendeleo hasa mkoani Kilimanjaro katika maeneo ya Rombo, Marangu na Mwika kutokana na kukithiri kwa vitendo vya Unywaji pombe holela ambapo aliagiza wakuu wa Wilaya kuhakikisha wanasimamia na kudhibiti hali hiyo.

Awali akiongoza ibada ya Maziko, Askofu Mkuu wa KKKT, Dayosisi ya Kaskazini, Dk. Martin Shao, aliwataka waumini wa dini ya Kikristo, wananchi pamoja na watumishi katika Jeshi la Polisi kufanya yale yaliomema ikiwa kweli wanataka kuenziwa kama ilivyo kwa marehemu Kombe.

Dk. Shao katika ibada hiyo, alimuelezea marehemu Kombe kama mtu anayestahili kuenziwa daima kama anavyoenziwa Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kutoka na utendaji wake kazi uliotukuka, uzalendo na Uadilifu pamoja na uwajibikaji katika kuhakikisha Amani ya Tanzania na usalama wa Wananchi wake.
Kabla ya kifo chake, Kamishna Kombe, alikuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa Kansa ambao ulianza kumsumbua Juni mwaka jana na kutibiwa katika Hospitali ya Rufaa KCMC, mjini Moshi.

James Kombe, aliyezaliwa mwaka 1950, mwika Kilimanjaro ameacha mjane mmoja, Maria Kombe na watoto watano na kwamba alilitumikia Jeshi la polisi kuanzia Machi, mwaka 1970 na kulitumikia mpaka alipostaafu mwaka 2010.

Akisoma historia ya Marehemu, Kamanda wa kikosi cha usalama
Barabarani, Joseph Mwakabonga alisema Kamishna Kombe, alijiunga na Mafunzo ya awali machi 23 mwaka 70 na kumaliza Agosti 28 mwaka huo, huko Mopshi baada ya kuhitimu elimu ya Sekondari mwaka 1969 nchini Uganda.

Alisema alipandishwa vyeo kama Mkaguzi wa polisi (1977), Kamishna msaidizi (1995), Mkaguzi wa Polisi (1986), Mrakibu Mwandamizi (1991) na Kamishna Msaidizi wa Polisi (2002) hadi alipostaafu 2010.

No comments:

Post a Comment