Mmoja wa wachunguzi wa maswala ya anga kutoka Urusi amesema kuwa ndege ya Urusi iliyoanguka katika rasi ya Sinai nchini Misri ililivunjika ikiwa hewani.
Mtaalamu huyo Viktor Sorochenko, kutoka Urusi amewambia wandishi wa habari mjini Cairo kuwa hakuna sababu nyengine kwanini miili ya abiria na vitu vyao vingetapakaa kwa eneo hilo lenye mduara wa kilomita 20.
Hata hivyo haikubainika nini kilisababisha kuanguka kwa ndege hiyo iliyokuwa imebeba watalii 224 waliokuwa wakirejea nyumbani kutoka likizoni.
Sorochenko alikuwa amezuru eneo la tukio katika rasi ya Sinai akiwa ameandamana na watalamu wenza kutoka Ufaransa, Ireland na Misri.
Ujumbe huo wa wataalamu wa kuchunguza ajali za ndege walipata fursa ya kutazama vifaa vya kunakili safari za ndege al maaruf Black Box.
Awali wapiganaji wa kundi la Islamic State walisema kuwa waliadungua ndege hiyo ilikulipiza kisasi kufuatia mashambulizi ya Urusi dhidi yao huko Syria.
Madai hayo yalipuziliwa mbali na maafisa wa utawala nchini Misri na Urusi.
Hata hivyo madai haya mapya ya Sorochenko sasa yanaibua hofu kuhusu usalama wa safari za ndege katika maeneo ya vita.
Tayari mashirika ya ndege ya Emirates,Lufthansa na Air France zimesitisha safari zote juu ya rasi hiyo zikihofia usalama wao.
Ndege hiyo ya Kogalymavia Airbus A-321 ilianguka muda mfupi baada ya kupaa kutoka Sharm el-Sheikh.
Ilikuwa inaelekea mji mkuu wa Urusi St Petersburg.
Waziri mkuu wa Misri Sharif Ismail amesema kuwa ilikuwa vigumu kwa waasi hao kudungua ndege ikiwa inapaa kimo cha futi 31,000 kutoka ardhini ambayo ndege hiyo aina ya Airbus 321 ilikuwa inapaa.
Rais Abdul Fattah al-Sisi ametaka jamii ya walioathirika na ile ya kimataifa kuwa na subira uchunguzi ukiendelea.
Urusi imekuwa ikiomboleza vifo vya raia wao.
No comments:
Post a Comment