TANGAZO


Thursday, July 2, 2015

Waziri Magufuli awataka Watendaji wa Wakala wa Ujenzi (TBA) kuwapa kipaumbele watumishi wa Umma



Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli

Na Lorietha Laurence- Maelezo
WAZIRI wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Magufuli  amewataka watendaji wa Wakala wa Ujenzi (TBA) kuwapa kipaumbele zaidi watumishi wa umma katika miradi yao ya nyumba za makazi.


Aliyasema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati wa ziara ya ukaguzi wa miradi inayosimamiwa na TBA iliyopo maeneo ya Bunju B na Ada Estate ambapo  Waziri, Mhe Magufuli alizindua jengo la  EX-NMC lililopo Mbezi beach.


 Aidha aliongeza kuwa serikali imefurahishwa na juhudi za TBA katika kuhakikisha kuwa  watumishi wa umma wanapata  makazi bora na yenye huduma zote za miundo mbinu ikiwemo barabara, maji na umeme.


“Nimefurahishwa na kazi inayofanywa na TBA kwa kweli ni hatua nzuri  itakayowasaidia watumishi kupata makazi bora  hata watakapostaafu  hawatakuwa na  msongo wa mawazo kuhusu mahali pa kuishi” alisema Mhe. Magufuli.


Naye Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ujenzi (TBA) Elius Mwakalinga ameleeza kuwa mpango wao ni kuhakikisha wanajenga nyumba 10,000 nchini ambapo mpaka sasa wamefanikisha kujenga nyumba 1,816.
“Mpaka sasa tumeweza kujenga nyumba 1,816 ikiwemo hizi za Bunju B ambazo ni jumla ya nyumba 851 zilizogharimu shilingi Bilioni 6 mpaka kukamilika kwake” alisema Bw. Mwakalinga.


Pia aliongeza kuwa wamefanikiwa kupata mkopo wa shilingi Milioni 23 kutoka benki ya CRDB ambapo baadhi ya benki kama Benki ya Afrika (BOA) wamehaidi kutoa shilingi milioni 18 wakati Benki ya Uwekezaji (TIB) nayo imeahidi kutoa shilingi Milioni 6 ili kuwezesha ujenzi wa nyumba hizo kukamilika.

 
Aliongeza  kuwa  kwa kuishukuru serikali kwa kuiamini kwa kuwapa usimamizi wa mradi wa kukarabati Ikulu ndogo ya Chamwino pamoja na ujenzi wa nyumba 149 zilizo chini ya Tamisemi.


Wakala wa Ujenzi (TBA ni taasisi ya umma ilianzishwa chini ya  sheria ya ujenzi  na. 30 ya mwaka 1997  jukumu lake kuu ni kusimamia na kuendesha miliki za serikali ikiwemo viwanja,ofisi na nyumba za watumishi wa umma.

No comments:

Post a Comment