TANGAZO


Thursday, July 9, 2015

Wadau wa sekta ya Bima nchini waaswa kushirikiana na TRA kutekeleza sheria mpya ya kodi

Naibu Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Lusekelo Mwaseba akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufungua semina ya wadau wa bima kuhusu sheria mpya ya kodi ya mwaka 2014 ambayo imeanza kutumika Julai Mosi mwaka huu. (Picha na Eleuteri Mangi- MAELEZO)

Na Eleuteri Mangi- MAELEZO
WADAU wa sekta ya Bima nchini wameaswa kushirikiana na Serikali kutekeleza sheria mpya ya kodi ya mwaka 2014 ili waweze kutoa huduma kwa jamii yenye tija kwa wakati na kulipa kodi stahiki.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Lusekelo Mwaseba leo jijini Dar es salaam alipokuwa akifungua semina ya wadau wa bima nchini kuhusu sheria mpya ya kodi ya mwaka 2014 ambayo imeanza kutumika Julai Mosi mwaka huu.

“Tumekutana nanyi katika semina hii tukiwa na lengo la kushirikishana ili kuijua na kuitekeleza kwa sheria hii mpya kwa mnufaa yetu sote kama Serikali na wa wadau wa sekta hii ya Bima” alisema Lusekelo.

Akifafanua juu ya malengo ya semina hiyo, Lusekelo amesema kuwa mojawapo ya malengo ni kuwaelimisha na kuwahamasisha wadau kuingia katika kutekeleza sheria hiyo mpya na kuwasikiliza wadau hao maoni yao ili kutoa au kupunguza na kutafuta kwa pamoja njia ya kutatua changamoto zinazoikabili sekta hiyo nchini. 

Kwa upande wake Afisa Mtendaji wa Kampuni ya Bima ya BUMACO Bw. Ramadhan Mongi amesema kuwa sheria hiyo ni nzuri na inalenga kuimarisha uchumi wa ndani ya nchi ikizingatiwa kuwa ni kwa mara ya kwanza sekta ya bima inaingia kwenye masuala ya shughuli za uchumi nchini.


Aidha, sheria hiyo mpya ya kodi nchini imejumuisha shughuli zinazofanywa na madalali nchini  ambapo katika semina hiyo imeundwa kamati ndogo ya ya wajumbe watatu kutoka jumuiya inayoundwa na wadau wa sekta ya bima itafanya kazi kwa kushirikiana na wataalamu kutoka TRA ili kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayoendana na sheria hiyo ya kodi ya mwaka 2014 katika kuimarisha na kuboresha utoaji huduma na kulipa kodi stahiki kwa maendeleo endelevu nchini.

No comments:

Post a Comment