Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt. Abdallah Kigoda akisalimiana na viongozi na wafanyakazi wa Chuo cha Elimu ya Biashara kampasi ya Dar es Salaam alipowasili chuoni hapo kuzindua Bodi mpya ya uongozi ya Chuo hicho leo. (Picha zote na Aron Msigwa- MAELEZO)
Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt. Abdallah Kigoda akizungumza na wajumbe wa Bodi ya Chuo cha CBE na menejimenti ya chuo hicho kabla ya kuzindua rasmi Bodi mpya ya uongozi ya chuo hicho leo.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt. Abdallah Kigoda (kulia) akimkabidhi mwongozo wa utendaji kazi Mwenyekiti wa Bodi iliyoteuliwa ya uongozi wa Chuo cha Elimu ya Biashara, Prof. Mathew Luhanga (kushoto) leo jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt. Abdallah Kigoda (katikati) akizungumza jambo na viongozi na wajumbe wa Bodi mpya ya uongozi ya Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) iliyoteuliwa alipokuwa akitembelea maeneo mbalimbali ya chuo hicho leo jijini Dar es salaam. Kushoto ni Mkuu wa chuo hicho Prof. Emanuel Mjema, Makamu Mwenyekiti wa Bodi Prof. Eleuther Mwageni na kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Uongozi ya CBEP, Prof. Mathew Luhanga.
Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) Prof. Emanuel Mjema (kushoto) akimwonesha Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt. Abdallah Kigoda baadhi ya maeneo ya chuo yaliyokuwa yamevamiwa na watu na kujengwa majengo yakiwa wazi baada ya kubomolewa kufuatia uongozi wa chuo hicho kuendelea na juhudi za kuyarudisha maeneo yote yaliyokaliwa kinyume cha sheria chini ya umiliki wa chuo.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt. Abdallah (katikati)Kigoda akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Bodi ya Uongozi wa Chuo cha CBE na Menejimenti ya CBE leo jijini Dar es Salaam.
Na Aron Msigwa –MAELEZO.
13/1/2015. Dar es Salaam.
WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Dkt. Abdallah Kigoda amezindua rasmi Bodi ya Uongozi ya Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) na kuitaka bodi hiyo kufanya kazi zake kwa kuzingatia sheria na kushirikiana na menejimenti ya chuo hicho kuweka mikakati na mipango ya maendeleo itakayokiwezesha chuo hicho kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.
Akizungumza na viongozi na wajumbe wa bodi hiyo leo jijini Dar es salaam, Dkt. Kigoda amesema serikali inayo imani kubwa na Mwenyekiti na wajumbe wa Bodi hiyo walioteuliwa na kwamba watatimiza majukumu yao kikamilifu na kukiwezesha chuo hicho kufikia malengo na matarajio ya watanzania ya kuendelea kuzalisha wataalam bora wa fani za biashara.
“Ninaamini kuwa Bodi niliyoizindua leo itasimamia shughuli za chuo hiki kwa kufuata misingi ya uadilifu,utawala bora na kuongeza chachu ya kuleta huduma bora kwa wananchuo na umma” Amesisitiza Dkt. Kigoda.
Amesema viongozi na wajumbe wa Bodi walioteuliwa wanalojukumu la kusimamia ustawi wa chuo hicho wakiwa chombo cha juu cha utoaji wa maamuzi na usimamizi wa masuala mbalimbali ya chuo hicho ikiwemo uidhinishaji wa matumizi ya chuo yanayoendana na mapato ya chuo, uteuzi wa Mkuu wa Chuo na watumishi wengine na uidhinishaji wa viwango vya ada.
Akizungumzia mabadiliko ya chuo hicho toka kuanzishwa kwake mwaka 1965 Dkt. Kigoda amesema yamehusisha mabadiliko makubwa ya mitaala ya kufundishia ili kuwafanya wanafunzi na wahitimu waweze kupanua ufahamu wao kwa kuwa na uwezo wa kukabiliana na ushindani wa soko la ajira kwa kuongeza fursa za ajira katika sekta ya umma na binafsi pamoja kuwajengea uwezo wahitimu waweze kujiajiri wenyewe.
Kwa upande wake Mkuu wa Chuo hicho Prof. Emanuel Mjema akizungumza wakati wa kuwakaribisha wajumbe walioteuliwa chuo hapo amesema kuwa wao kama viongozi wa chuo hicho wataendelea kusimamia msingi wa kuanzishwa kwa chuo wa kuendelea kuzalisha wataalam bora katika nyanja za biashara na sekta ya uendeshaji viwanda nchini.
Amesema kuwa wao kama menejimenti ya chuo hicho watashirikiana na uongozi na wajumbe wa bodi iliyoteuliwa kusimamia rasilimali na miundombinu ya chuo hicho ili kiendelee kutoa huduma bora kwa wanafunzi na wananchi wengi Zaidi kwa wakati.
Naye Makamu mwenyekiti wa Bodi ya Uongozi ya Chuo hicho Prof. Eleuther Mwageni akizungumza kwa niaba ya uongozi na wajumbe wa bodi iliyoteuliwa amesema kuwa Bodi iliyoteuliwa itatekeleza majukumu yote yaliyoanishwa kwa mujibu wa sheria.
No comments:
Post a Comment