TANGAZO


Friday, August 29, 2014

Wabunge wa bunge Jumuiya ya Afrika Mashariki watembelea bandari ya Dar es Salaam


Spika wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA), Dkt. Magreth Zziwa (wa pili kulia), akipewa maelezo na Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya TICS, Paul Wallace namna kampuni yake inavyofanya kazi ya kupakua na kupakia mizigo katika bandari ya Dar es Salaam, wakati wa ziara ya Wabunge wa bunge hilo, walipotembelea Ofisi za Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), leo jijini Dar es Salaam. (Picha zote na Eleuteri Mangi-MAELEZO)



Wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki wakitembelea Bandari ya Dar es Salaam, walipofika Ofisi za Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) leo jijini.

Na Eleuteri Mangi-MAELEZO
Jumuiya ya Afrika Mashariki iko makini katika kutekeleza majukumu yake na iko karibu na watu wake kwa kuwahudumia kupitia nchi washirika.
Kauli hiyo imetolewa na Spika wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) Dkt. Magret Zziwa wakati wa ziara yake alipotembelea ofisi za Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) pamoja na wabunge wa bunge hilo leo jijini Dar es salaam.
Spika Dkt. Zziwa alibainisha kuwa lengo la ziara ya wabunge hao ni kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na TPA na Bandari ya Dar es salaam kwa ujumla katika kuhudumia nchi washirka kiuchumi na kujiamii.
“Ni muhimu kuifanya Jumuiya kuwa imara zaidi kiuchumi na kijamii ili kuwahudumia watu wetu kwa umahiri na umakini mkubwa katika mahitaji yao” alisema Spika Dkt. Zziwa.
Wabunge hao walitembelea maeneo mbalimbali bandarini hapo na kujionea shughuli zinazofanywa ikiwa ni pamoja na kupakia na kupakua mizigo inapoingia au kutoka ili kusafirishwa kwenda nchi husika.
Spika Dkt. Zziwa alisisitiza kuwa wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wanahitaji kuona jumuiya yao inavyowajali na kuwahudumia wanapotekeleza majukumu yao ikizingatiwa kuwa kwa sasa hakutakuwa na urasimu wa kusafirisha mizigo kutoka nchi moja kenda nyingine  kwa kukaguliwa mara mbili ambapo kwa sasa utaratibu wa Himaya Moja ya Forodha umeanza kutekelezwa kwa mafanikio makubwa.
Akionesha umuhimu wa uchukuzi na usafirishaji wa mizigo kati ya nchi washirika, Naibu Waziri wa Wizara ya Ushirikiano ya Afrika Mashariki, Dkt. Abdala Juma Abdulla Saadalla amefananisha bandari, reli na barabara katika nchi kuwa ni sawa na “moyo na mishipa ya damu” ambapo amebainisha kuwa Serikali ya Tanzania inaendelea kuboresha reli zilizopo ili ziweze kutoa huduma kwa wakati.
“Tayari Serikali kupitia wataalamu wake wa ndani imeboresha vichwa vya treni nane hadi sasa ambapo vinatarajiwa kuanza kutumika Januari mwakani pamoja na makasha” alisema Naibu Waziri Saadalla.
Kwa upange wake Meneja wa Bandari ya Da es salaam Awadh Massawe alipokuwa akiwaeleza Wabunge wa Jumuiya ya Afrika Mashariki namna TPA inavyofanya kazi, amesema kuwa kwa mwaka 2013/2014 mizigo inayosafirishwa kutoka bandarini hapo imeongezeka kutoka tani milioni 4.05 mwaka 2012/13 hadi tani milioni 4.45 mwaka 2013/2014 ambayo ni sawa na asilimia 9.8.
Massawe amesema kuwa mizigo hiyo ilisafirishwa kutoka bandari ya Dar es salaam kwenda nchi za Zambia, Jamhuri ya Kidemokrasia Kongo, Burundi, Rwanda, Malawi and Uganda kwa kutumia mifumo ya barabara na reli.
Massawe amesema kuwa bandari ya Dar es salaam imekuwa ni kiunganishi cha Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kutumia mitandao iliyopo ya njia ya reli na barabara.
Kwa upande wa reli, Massawe amesema kuwa Bandari ya Dar es salaam inaunganishwa na reli ya kati kwenda Mwanza na Kigoma hali inayorahisisha nchi za Burundi, Rwanda na Kongo DRC kufikika kirahisi na TARZARA ambayo inakwenda hadi Zambia.
Kwa njia ya barabara, Bandari ya Dar es salaam inaunganisha Tanzania na nchi nyingine  kuanzia Dar es salaam  kupitia Dodoma/Isaka/Rusumo /Kabanga, Kigali hadi Bujumbura kwa Rwanda na Burundi, vilevile Dodoma/Mwanza/Mutukula hadi Kampala Uganda.
Aidha, Massawe amesema kuwa kwa mwaka 2013/2014 kumekuwa na jumla ya asilimia 30.4 ya mizigo yote ilihudumiwa na bandari ya Dar es salaam.
Massawe amesema kuwa ongezeko hilo la usafirishaji wa mizigo linatokana na maboresho yaliyofanywa bandarini hapo kuhusu namna ya usafirishaji wa mizingo kufuatia   mfumo wa Himaya Moja ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na kuboreshwa kwa taratibu za kibiashara nchini na nchi inapopelekwa mizigo hiyo.
Naye Kaimu Kamishina wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Lusekelo Mwaseba  alifafanua faida ya mfumo wa Himaya Moja ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kuwa unatarajiwa kupunguza gharama za kufanya biashara na kuondoa urasimu wakati wa usafirishaji mizigo, kupunguza gharama za kiutawala, kuondoa uwezekano wa rushwa na kuimarisha matumizi ya mifumo ya mawasiliano (ICT) taktika kubadilishana taarifa miongoni mwa nchi washirika.
Ziara hiyo ilijumuisha Wabunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki, Makamishina kutoka Burundi, Rwanda, Kenya, Uganda, mwenyeji Tanzania pamoja na Viongozi na watumishi wa TPA.

No comments:

Post a Comment