TANGAZO


Thursday, August 14, 2014

Naibu Waziri Masele awataka vijana kujikita katika mambo ya Sayansi na Teknolojia



 Naibu Waziri Masele
Na Benedict Liwenga-MAELEZO

14/08/2014.

NAIBU Waziri wa Nishati na Madini Stephen Masele amewataka vijana nchini kupenda kujikita katika masomo ya sayansi na teknolojia kama mihimili yenye kuleta maendeleo kwa haraka ulimwenguni ili waweze kupata ujuzi na mitazamo katika sekta ya gesi ambayo inakuwa kwa kasi kubwa nchini.


Mhe. Masele ameyasema hayo jana wakati alipokuwa akifunga Kongamano la Tatu la Vijana Wanasayansi Duniani lililofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Julius Kambarage Nyerere, kongamano ambalo liliwakutanisha vijana toka nchi zaidi ya 46 ulimwenguni zikiwemo baadhi ya nchi za Afrika ambapo Tanzania ilikuwa mwenyeji wa Kongamano hilo.


Mhe. Masele ameeleza kuwa sayansi na teknolojia ndiyo mihimili mikubwa ya sasa katika kuleta maendeleo ya haraka katika nyanja mbalimbali kwani mambo mengi hivi sasa hutegemea sayansi na teknolojia.

Aidha, Mhe. Masele amezitaja baadhi ya changamoto zinazozikabili baadhi ya nchi za Afrika katika kupata maendeleo ni pamoja na kutowekeza katika sayansi na teknolojia hali inayopelekea baadhi ya nchi nyingi kukosa wataalam wa kutosha katika mambo ya sayansi na teknolojia, hivyo amezitaka nchi za Afrika kuwekeza katika sayansi ili kuweza ili kubadilisha uchumi wa Afrika.

“Sayansi na teknolojia huleta maendeleo makubwa hivyo nawapa moyo vijana muendelee kufanya kazi kwa bidii na kujituma katika mambo ya sayansi na teknolojia ili muweze kuleta uchumui endelevu”. Alisema Masele.


Akizungumzia kwa upande wa Serikali ya Tanzania, Mhe. Masele amesema kuwa serikali ya Tanzania imewekeza nguvu zake kwa sasa katika kuendeleza sayansi ya afya kwa kuanzisha Vyuo mbalimbali na kuwasomesha watanzania nchi mbalimbali za nje ili waweze kwenda kupata ujuzi na kuwa wataalam na wakaguzi katika sekta ya gesi pamoja na mafuta kwa lengo la kuja kuisaidia nchi yao.

“Wajibu wetu kama Serikali tumeamua kwa makusudi kusomesha vijana katika nchi mbalimbali ili wakaweze kupata elimu juu ya sayansi na teknolojia hasa katika masuala ya gesi ili kupata wataalam na wakaguzi wa kutosha nchini ambao watalisaidia taifa kuinua uchumi wake na hivi sasa serikali imeanzisha vyuo mbalimbali nchini, program mbalimbali za mafunzo kwa watanzania, imetoa ufadhili wa masomo kwa watanzania na imedhamini makongamano ya vijana ili wapate fursa ya kujiendeleza.” Alisisitiza Masele.


Mhe. Masele amempongeza Waziri wa Nishati na Madini, Mhe. Prof. Sospeter Muhongo kwa kazi kubwa anayoifanya katika Wizara yake na pia amewapongeza vijana waliohudhuria katika kongamano hilo pamoja kuyapongeza Makampuni wadhamini wa kongamano hilo na kuyataka makampuni hayo kuendelea kuwekeza pamoja na kulipa kodi ili serikali iweze kukusanya mapato na wananchi wapate kunufaika na mapato hayo.


Naye Rais wa Vijana Wanasayansi Duniani (YES) Bw. Meng Wang amemshukuru Makamu wa Rais wa Tanzania, Waziri wa Nishati na Madini pamoja na Naibu Waziri steven Masele kwa kuwaunga mkono vijana waliohudhuria kongamano hilo na kuonesha hali nzuri ya ushirikiano baina ya serikali na vijana na amewaasa vijana kujikita katika sayansi na teknolojia kama mihimili mikuu ya maendeleo duniani.


“Naishukuru sana Tanzania pamoja na ujio wa Mawaziri wake katika kufanikisha kongamano hili la vijana wanasayansi, nawashukuru pia wadhamini wa makampuni mbalimbali wa kongamano hili pamoja na vijana kwa ujumla toka nchi mbalimbali duniani”. Alisema Wang.

No comments:

Post a Comment