TANGAZO


Tuesday, August 5, 2014

Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP) watoa tamko kuhusu mwenendo wa mchakato wa Katiba


Mkurugenzi na Katibu Mtendaji  wa Mtandao wa Wanafunzi nchini Tanzania (TSNP), Alphonce Lusako, akizungumza na waandishi wa habari, kuhusu mwenendo wa Mchakato wa Katiba, Dar es Salaam leo. (Picha zote na Kassim Mbarouk-www.bayana.blogspot.com)
Baadhi ya waandishi wa habari, wakiandika maelezo yaliyokuwa yakitolewa na Mkurugenzi na Katibu Mtendaji  wa Mtandao wa Wanafunzi nchini Tanzania (TSNP), Alphonce Lusako (hayupo pichani), wakati alipokuwa akizungumza nao, kuhusu mwenendo wa Mchakato wa Katiba, Dar es Salaam leo. 
Baadhi ya waandishi wa habari, wakiwa kwenye mkutano na Uongozi wa Mtandao wa Wanafunzi nchini Tanzania (TSNP), wakati ulipokuwa ukizungumza nao, kuhusu mwenendo wa Mchakato wa Katiba, Dar es Salaam leo. 

Na Rose Masaka

MTANDAO wa wanafunzi nchini (TSNP) Umetoa tamko dhidi ya mwenendo wa mchakato wa kupata Katiba mpya ya Tanzania.


Mkurugenzi mtendaji wa mtandao wa wanafunzi Bwana Alphonce Lusako ametoa tamko hilo katika mkutano ulioudhuriwa na  waandishi wa habari leo, jijini Dar es Salaam.


Lusako ametoa ombi kwa vyama vyote vya siasa kurudi bungeni na kufanya maridhiano ili tuweze kupata katiba mpya ambayo itasaidia kuokoa mabilioni ya fedha za watanzania ambazo zimekwisha tumika katika mchakato wa kutafuta katiba mpya.


“Tunawaomba CCM, UKAWA, TANZANIA ONE na wajumbe wa Bunge Maaalum la Katiba kujua kuwa kushindwa kwa mchakato huu siyo kushindwa kwa  kwa chama chochote ila ni kushindwa kwa Watanzania,”alisema Lusako.


Viongozi wa mtandao wa wanafunzi nchini, umewaomba UKAWA, CCM na wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba wafikie muafaka na watambue kuwa sheria kuu ya wao ndani ya bunge ni kuboresha Katiba ya wananchi na siyo kupindua maamuzi ya wananchi.

Wajumbe  wa Bunge Maalum la Katiba  wanatakiwa wajue kuwa hawapo kwa ajili ya kutafuta na kutambua mshindi na mshindwa, bali upo kwa ajili ya ushindi wa watanzania ambao pesa zao nyingi zimetumika.

Aidha, ameongeza kwa kusema kuwa, mchakato haupo kwa ajili ya kutambua nani anamsimamo huu na msimamo ule,bali upo kwa ajili ya kutambua msimamo wa watanzania juu ya namna gani taifa lao litaongozwa na katiba iliyotokana na mawazo yao.

Mtandao wa wanafunzi nchini uliitisha kongamano rasmi la wanafunzi wa Vyuo Vikuu na sekondari kwa ajili ya kujadili mchakato mzima wa kupata Katiba mpya ndani ya Taifa letu ambao uliwapa wanafunzi fursa ya kupaza sauti zao juu ya mchakato mzima wa katiba.

1 comment: