Ofisa Kazi Mwandamizi wa Wizara ya Kazi na Ajira, Ayubu Musa (kulia), akieleza jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani), kuhusu jinsi ukuaji wa sekta unavyochangia kuanzishwa kwa bodi ya Mshahara kwa sekta husika, wakati wa mkutano uliofanyika ukumbi wa Idara ya Habari, Maelezo, jijini Dar es Salaam leo. Kushoto ni Msemaji Wizara hiyo, Ridhiwan Wema.
Mchumi Mwandamizi wa Wizara ya Kazi na Ajira, Jofrey Mashafi akieleza kuhusu mipango ya Serikali katika kukabiliana na tatizo la upungufu wa Ajira nchini, ikiwa ni pamoja kuanzishwa kwa programu ya miaka 3, inayoratibiwa na wizara hiyo kwa kushirikiana Chuo cha Sokoine na Bank ya CRDB, ya kuwajengea uwezo wahitimu wa Vyuo Vikuu nchini, inayotarajiwa kuzalisha ajira 30,000, wakati wa mkutano, uliofanyika ukumbi wa Idara ya Habari, Maelezo jijini Dar es Salaam leo. Kushoto ni Ofisa Habari wa Idara ya Habari, Maelezo, Georgina Misama. (Picha zote na Frank Mvungi-MAELEZO)
WIZARA ya Kazi na
Ajira imewaasa waajiri katika Sekta binafsi kuzingatia Sera na sheria za kazi
mahali pa kazi ili kuleta tija na nidhamu kazini.
Hayo yamesemwa na
Msemaji wa Wizara hiyo Ridhiwani Wema wakati wa mkutano na waandishi wa habari
leo jijini Dar es Salaam, akieleza kuhusu utaratibu wa uanzishwaji wa Bodi za
mishahara kisekta ili kusaidia kuboresha maslahi ya wafanyakazi.
Wema amevishauri
vyama vya wafanyakazi kuboresha mishahara na maslahi ya wafanyakazi kupitia
majadiliano ya pamoja sehemu za kazi
kwa kuwa sheria na kanuni zinatoa na kuhimiza haki hizo.
Alizitaja bodi za
mishahara zilizoanzishwa kuwa ni kilimo, Afya, Biashara na Viwanda, Mawasiliano,
Madini, Uvuvi na huduma za majini, hoteli na huduma za majumbani, na ulinzi
binafsi.
Wema alifafanua
kuwa katika kipindi cha mwaka 2011 hadi sasa ziliundwa bodi 4 za mishahara
kufanya jumla ya bodi za kisekta kuwa 12 hadi mwaka 2013.
“Moja ya majukumu
ya bodi ni kufanya uchunguzi kuhusu kima cha chini cha mishahara na hali ya
ajira katika sekta husika ambapo
pia humshauri Mhe. Waziri kuhusu kima cha chini cha mishahara pamoja na
masharti ya ajira katika sekta husika”, alisema Wema.
Alibainisha kuwa Bodi
za ajira zimetembelea mikoa ya Dar es Salaam, Mororogoro, Pwani, Dodoma, Arusha, Mwanza,
Tanga, Manyara, Iringa, Mbeya na Kilimanjaro ili kijionea mazingira ya kazi na
kupata maoni ya wadau kuhusu kima cha chini cha mishahara katika Sekta husika.
Msemaji huyo aliongeza
kuwa vyama vya wafanyakazi vina nafasi kubwa kusaidia katika kuboreshwa kwa
maslahi ya wafanyakazi kupitia majadiliano ya pamoja sehemu za kazi kwa kwa
kuwa sheria na kanuni zinatoa na kuhimiza haki hiyo.
Naye Ofisa Kazi
Mwandamizi Idara ya Ajira, Ayubu Musa alisema kuwa wizara hiyo imekuwa mstari
wa mbele katika kuhakikisha kuwa taratibu, sheria na kanuni za kazi
zinazingatiwa ambapo wamekuwa wakifanya ukaguzi mara kwa mara ili kuhakisha
kuwa kuna mazingira bora na maslahi ya wafanyakazi katika sekta binafsi.
Bodi za mishahara
kisekta zinaundwa kwa mujibu wa sheria ya Taasisi za kazi namba 7 ya mwaka 2004
ambapo kila bodi inaundwa na wajumbwe 8 akiwemo mwenyekiti na wajumbe
wanaowakilisha maslahi ya Serikali wajumbe 2,waajiri wajumbe2 na wafanyakazi 2
katika mfumo wa utatu.
No comments:
Post a Comment