TANGAZO


Friday, July 19, 2013

Chama cha Wananchi (CUF), kulishitaki Jeshi la Wananchi (JWTZ) baada ya viongozi wao kukamatwa na kupigwa mkoani Mtwara

Naibu Mkurugenzi wa Oganaizesheni, Uchaguzi na Bunge wa Chama cha Wananchi (CUF), Shaweji Mketo, akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam leo, kuhusu kupigwa na aliodai kuwa ni wanajeshi wa Jeshi la Wananchi (JWTZ), mkoani Mtwara mwishoni mwa mwezi uliopita. Kulia ni Mwenyekiti wa Vijana Mtwara Mjini, Ismail Bakari na Mwenyekiti Mtwara Mjini, Salum Khamis (Picha zote na Kassim Mbarouk-www.bayana.blogspot.com)
Naibu Mkurugenzi wa Oganaizesheni, Uchaguzi na Bunge wa Chama cha Wananchi (CUF), Shaweji Mketo, akiwaonesha waandishi wa habari, alipokuwa akizungumza nao, Dar es Salaam leo, viatu alivyopewa na aliodai wanajeshi wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), mkoani Mtwara baada ya kuvichukua vya kwake, wakati alipokamatwa na kupata kipigo alichodai kutolewa na wanajeshi hao, wakati alipokuwa katika ziara mkoani humo, mwishoni mwa mwezi uliopita. Kushoto ni Mwenyekiti Wilaya ya Mtwara Vijijini, Ismail Khamis.
Naibu Mkurugenzi wa Oganaizesheni, Uchaguzi na Bunge wa Chama cha Wananchi (CUF), Shaweji Mketo (kushoto), akiwa pamoja na baadhi ya viongozi wenzake wa chama hicho, wa Mkoa wa Mtwara, wakiwaonesha waandishi wa habari, Dar es Salaam leo, alama za kupigwa mgongoni walizodai kupigwa na wanajeshi wa Jeshi la Wananchi (JWTZ), mkoani humo mwishoni mwa mwezi uliopita. Kutoka kulia ni Mwenyekiti wa Vijana Mtwara Mjini, Ismail Bakari, Mwenyekiti Mtwara Mjini, Salum Khamis na Katibu wa chama hicho, Mtwara, Said Issa. 
Naibu Mkurugenzi wa Oganaizesheni, Uchaguzi na Bunge wa Chama cha Wananchi (CUF), Shaweji Mketo (kushoto), akiwa pamoja na baadhi ya viongozi wenzake wa chama hicho, wa Mkoa wa Mtwara, wakiwaonesha waandishi wa habari, Dar es Salaam leo, alama za kupigwa mgongoni walizodai kupigwa na wanajeshi wa Jeshi la Wananchi (JWTZ), mkoani humo mwishoni mwa mwezi uliopita. Kutoka kulia ni Mwenyekiti wa Vijana Mtwara Mjini, Ismail Bakari, Mwenyekiti Mtwara Mjini, Salum Khamis na Katibu wa chama hicho, Mtwara, Said Issa. 
Baadhi ya waandishi wa habari na wanachama wa Chama cha Wananchi waliokuwepo kwenye mkutano huo, wakifuatilia habari hizo pamoja na kuwaangalia wanachama hao waliopata kipigo kilichodaiwa nao kutoka kwa wanajeshi wa JWTZ.
 Baadhi ya waandishi wa habari, wakisikiliza habari zilizokuwa zikitolewa na Naibu Mkurugenzi wa Oganaizesheni, Uchaguzi na Bunge wa Chama cha Wananchi (CUF), Shaweji Mketo katika mkutano huo jijini Dar es Salaam leo.
Naibu Mkurugenzi wa Oganaizesheni, Uchaguzi na Bunge wa Chama cha Wananchi (CUF), Shaweji Mketo, akifafanua jambo kwa waandishi wa habari, wakati alipokuwa akizungumza nao, Dar es Salaam leo, kuhusu kupigwa na aliodai kuwa ni wanajeshi wa Jeshi la Wananchi (JWTZ), mkoani Mtwara mwishoni mwa mwezi uliopita. Kulia ni Mwenyekiti Mtwara Mjini, Salum Khamis na kushoto ni Mwenyekiti Wilaya ya Mtwara Vijijini, Ismail Khamis.
Waandishi wa habari, wakiwaangalia kwa huzuni, viongozi waliopigwa na waliodaiwa kuwa wanajeshi wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), mkoani Mtwara.
Wanachama na wananchi waliofika Ofisi za Makao Makuu ya CUF, Buguruni wakiwaangalia, viongozi waliopigwa na waliodaiwa kuwa wanajeshi wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), mkoani Mtwara.
Baadhi ya wanachama na wananchi waliofika Ofisi za Makao Makuu ya CUF, Buguruni wakichukua picha za viongozi waliopigwa na waliodaiwa kuwa wanajeshi wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), mkoani Mtwara.


Na Joyce Ngowi
CHAMA cha Wananchi (CUF) kinakusudia kulishitaki Jeshi wa Wananchi la Tanzania (JWTZ) kutokana baadhi ya askari wa jeshi wa kambi ya Naliendele mkoani Mtwara kuwakamata kuwapiga na kuwatesa viongozi wa ngazi mbalimbali wa chama hicho.

Tukio hilo lililohusishwa na vurugu za kugombea gesi baina ya wananchi wa Mtwara na Serikali lilitokea Juni 27,mwaka huu ambapo viongozi hao walikwenda kwenye kijiji cha Msimbati umbali wa km 40 hadi 45 kutoka Mtwara mjini kwa lengo la kuthibitisha madai ya mmoja wa wanachama wa CUF anayedai kubakwa na mwanajeshi mmoja.

Akizungumza Dar es Salaam leo mchana, Naibu Mkurugenzi wa Uchaguzi na Bunge Shaweji Mketo alisema  tukio la kubakwa kwa mwanamke huyo ni la kweli,kwani baada ya tukio hilo alichukuliwa na mwenyekiti wa kitongoji na kupelekwa polisi ambapo alipatiwa fomu namba tatu kisha alikwenda hospitali kupatiwa matibabu.

Alifafanua kuwa baada ya kujiridhisha huko waliondoka eneo la Msimbati ambapo robo km(1/4) kutoka eneo la hilo njia panda ya Newala walikuta magari mawili aina TATA na gari dogo mali ya JWTZ  yaliyokuwa yamepaki kwa mtindo wa V na kuziba barabara hali iliyosababisha dereva wao Kashinde Kalungwana kusimama kwa lengo la kupisha magari hayo.

Alieleza kuwa baada ya gari lao kusimama walitokeza wanajeshi kama 60 na kuwazunguka ambapo mmoja wao aliyekuwa na cheo cha Kanali alifungua mlango wa gari na kumtoa kisha kuchukua fedha zilizokuwa kwenye mfuko wa shati lake kiasi cha sh.85,000.

"Baadaye msafara wote uliokuwa na watu sita tulipandishwa kwenye gari la jeshi kisha wakanivua viatu vyangu kisha wakanivalisha vya jeshi,walipotufikisha kwenye kambi ya Naliendele walituvua nguo zote kisha tukafungwa kwenye miti iliyopo eneo hilo na kuanza kuchapwa maeneo mbalimbali ya miili yetu isipokuwa kichwani tu,"alisema Mketo.

Alisema kuwa baada ya kujeruhiwa kutokana na kipigo kilichotembea kila baada ya dakika tano waliwekewa maji ya baridi yenye chumvi,ndimu na pilipili kwenye majeraha hayo na baadaye kuendelea na kipigo hadi pale alipopoteza fahamu na kuzinduka saa 11 alfajiri ambapo alijikuta akizungukwa na wanajeshi saba.

"Wanajeshi hao walipokuwa wakitupiga baadhi yao walikuwa wakisema lazima tuwapige kwani heri wachache wafe ila nchi iwe salama,ikiwa wanajeshi wanahamu ya kupigana wapelekwe huko Darfur Sudan au Demokrasia ya Kongo wakapigane na wanajeshi wenzao badala ya wananchi wasio na hatia,"alisema.

Alibainisha kuwa baada ya hapo wanajeshi hao waliwaita askari polisi ambao walifika kwenye kambi hiyo na kuwapeleka kituoni kwa lengo la kutoa maelezo ambapo pia walikataa kuwapa fomu namba tatu kwa ajili ya matibabu kwa madai kuwa haina ulazima wa kupatiwa matibabu.

Mketo alisema baada ya taratibu za polisi kumalizika walifikishwa mahakamani saa 11 jioni ambapo polisi walilazimika kumpigia hakimu simu ili aje kuwasomea mashitaka kutokana na muda wa kazi wa mahakama kumalizika saa tisa na nusu hivyo shughuli hiyo ilifanyika kinyume na sheria za nchi.

Hata hivyo alidai ukiukwaji wa sheria uliendelea kuwepo kwenye mlolongo mzima wa kadhia hiyo kwani watuhumiwa hao walifikishwa gerezani saa 12 jioni ikiwa ni kinyume na matakwa ya sheria.

Aidha alibainisha kuwa watuhumiwa hao walishindwa kupokelewa gereza la Lilungu kutokana na hali mbaya ya kiafya waliyokuwa nayo jambo lililomlazimu Mkuu wa gereza hilo kuwataka askari polisi waliowafikisha gerezani kuhakikisha wanapatiwa matibabu.

"Tunamshukuru Mkuu wa gereza ambaye alikataa kutupokea kutokana na hali zetu,hapo ndiyo polisi wakatupeleka hospitali ya Mkoa Ligula ambapo hatukufanikiwa kupata dawa yoyote zaidi ya dereva wetu kupatiwa kamba ya kutundikia mkono wake kwani ulikuwa umeteguka,"alisema Mketo.

Alibainisha kuwa wananchi wanaumia kwani wanapigwa bila sababu za msingi huku serikali ikichukulia kupigwa kwao kama harakati za kisiasa.

No comments:

Post a Comment