TANGAZO


Monday, February 4, 2013

Alichapwa na kuburuzwa akiwa uchi Misri



Kanda ya video iliyoonyesha Hamada akiburuzwa kwenye barabara
Mwanaume mmoja raia wa Misri, aliyeburuzwa au kukokotwa katika barabara za mji mkuu wa Misri Cairo, amesema kuwa maafisa wa usalama walihusika na dhulma hiyo dhidi yake, na kubadili madai yake ya awali kuwa waandamanaji ndio waliohusika.
Hamada Saber alichapwa na polisi waliokuwa wamevalia nguo za kiraia alinaswa kwenye kanda ya video iliyoonyeshwa kwenye televisheni siku ya Ijumaa wakati waandamanaji waliokuwa na hasira walipovamia ikulu ya Rais.
Mwanzo Hamada mwenye umri wa miaka 50 alisema kuwa alivuliwa nguo na kuchapwa na waandamanaji huku polisi wakimwokoa.
Lakini baadaye alisema kuwa polisi ndio wa kulaumiwa kwa masaibu yake.
Alidai kuwa alilazimishwa kutoa ushahidi wa uongo.
Mwanawe aliambia BBC kuwa ikiwa angetuhumu polisi wangemlimbikizia madai ya kuwa na mabomu ya petroli katika maandamano hayo.

Bwana Saber alisema kuwa polisi walikuwa wamemuomba msamaha kwa waliyomtendea.

Rais Mohammed Morsi wa chama cha kiisilamu cha Muslim Brotherhood, amelaani kitendo hicho na hata kuitisha uchunguzi.
Lakini wapinzani wa serikali wanasema kuwa uhalifu dhidi ya binadamu, unapaswa kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

Ghasia na vurugu zilivyotanda Misri mwishoni mwa wiki
Maandamano yaliyofanyika Ijumaa, yalihusisha polisi waliopambana na waandamanaji waliokuwa wanawarushia mawe.
Polisi nao waliwarushia gesi ya kutoa machozi na maji ili kuwatawanya. Ghasia hizi zilitokea baada ya wiki ya ghasia zengine ambapo zaidi ya watu hamsini walifariki.

Mtu mmoja alifariki katika maandamano ya Ijumaa huku wengine hamsini wakijeruhiwa.

Waandamanaji wanamshutumu rais Morsi kwa kuhujumu malengo ya mapinduzi ya kiraia yaliyofanyika mwaka 2011, madai ambayo ameyakana.
Alionya watu kupitia mtandao wa Facebook kuwa maafisa wa usalama wako tayari kuchukua hatua zozote za kiusalama ili kulinda nchi na kwamba makundi yanayosababisha vurugu yatachukuliwa hatua.

No comments:

Post a Comment