Polisi wakiwa katika doria kuzuia maandamano ya Waislamu, ambao wameacha kuandamana baada ya kutakiwa na viongozi wao kutokufanya hivyo. Maandamano hayo yalikuwa yafanyike leo kwa ajili ya kumuondoa madarakani Mufti wa Tanzania, Sheikh Issa bin Shaaban Simba.
DAR ES SALAA, Tanzania
JESHI la Polisi nchini, lilikuwa tayari kwa ajili ya kudhibiti maandamano yaliyokuwa yamepangwa kufanyika jijini hapa leo, kushinikiza kuwaondoa madarakani Mufti wa Tanzania, Sheikh Issa bin Shaaban Simba na Katibu Mkuu wa Baraza la Taifa la Mitihani (Necta), Dk. Joyce Ndalichako.
Polisi iwalikuwa wametanda na kufanya doria leo Adhuhuri, katika maeneo mbalimbali ya Kinondoni kwa ajili ya kuwadhibiti Waislamu kama wakikaidi agizo la kuwataka wasifanye hivyo, agizo lililotolewa na Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova.
Waislam hao ambao walipanga maandamano hayo, kufanyika baada ya Swala ya Ijumaa na kuwatangazia waumini wao, kujitokeza kwa wingi licha ya kupigwa marufuku, na kusambaza vipeperushi mitaani kuwataka kufanya hivyo.
Bayana blogspot, iliweza kushuhudia magari ya Jeshi la Polisi yapatayo manane, yakiwemo ya maji ya kuwasha na mabomu ya machozi, ya Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), Polisi wa Usalama wa Raia na Kikosi cha Mbwa wakizunguka mitaa mbalimbali ya katikati ya jiji kuanzia asubuhi kuelekea barabara ya Morogoro na kutokomea kusikojulikana.
Polisi na makachelo waliovalia mavazi ya kawaida walionwa na Habari Mseto wakiwa wamemwaga kila kona, kuimarisha usalama sehemu mbalimbali ikiwamo Makao Makuu ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata).
Kwa upande wake, Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhadi Musa Salum, aliwataka Waislamu kuungana kwa pamoja na kulaani watu wanaokashifu dini yao kwa maslahi yao binafsi, ikiwamo suala la Raia wa Marekani kumkashifu Mtume Muhammad (SAW) kupitia filamu aliyoitengeneza hivi karibuni.
“Naungana na waislamu wote kulaani kitendo hiki, kwani kinaweza kuleta uvunjifu wa amani duniani, kutokana na kukashifu imani za watu,” alisema Alhadi Mussa, aliyewataka Waislamu kukemea jambo hili kwa nguvu zote kwa amani pasipo kuleta machafuko.
Katika Msikiti wa Mtambani, Kinondoni, Polisi liliweza kujipanga kila kona, huku magari mawili ya FFU yakiwa yamejipanga kukabiliana na hali yoyote ya hatari, kutokana na kudaiwa maandamano yangeanzia hapo baada ya swala ya Ijumaa.
No comments:
Post a Comment