TANGAZO


Thursday, September 20, 2012

Tamko la Bakwata kuhusu mgogoro wa Waislamu na Bakwata



Sheikh Mkuu, Mufti Issa Bin Shaaban Simba, akiwa na Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhadi Mussa Salim


TAMKO LA BAKWATA JUU YA HABARI ZINAZOTOLEWA NA VYOMBO VYA HABARI KWA TASWIRA YA “MGOGORO BAINA YA WAISLAMU NA BAKWATA”

   Hivi karibuni nilitoa indhari juu ya njama na hila za kutaka kuvamia ofisi za Bakwata Makao Makuu kwa madai ya kutaka kuung’oa uongozi, zinazoasisiwa na kuratibiwa na kikundi kinachojiita JUMUIYA NA TAASISI ZA KIISLAMU kinachoongozwa na Bw. Ponda Issa Ponda.
  Hii si mara ya kwanza kwa kikundi hiki kutishia kuvamia Makao makuu ya BAKWATA kwa nia ya kuundoa madarakani kwa nguvu uongozi halali uliopo.  Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 1992 wakati wa uongozi wa aliekuwa Mufti wa Tanzania marehemu Sheikh Hemed bin Jumaa bin Hemed kwa madai kama haya haya kwamba uongozi umeshindwa kuwaongoza Waislamu na kuwaletea maendeleo. 
    Ni kwa kufuatia ghasia  hizo ndipo Serikali ilipoamua kuingilia kati na kuidhinisha kuandikishwa hilo linaloitwa BARAZA KUU LA JUMUIA NA TAASISI ZA KIISLAMU ili liweze kufanya maendeleo makubwa zaidi inayodai kuwa BAKWATA imeshindwa kuwaletea Waislamu.  Ni jambo la kustaajabisha hadi sasa ni miaka 20 tangu Baraza hilo lilipoandikishwa na hakuna jambo lolote la kuwaendeleza Waislamu walilolifanya, wameshindwa hata kujenga ofisi ambayo Baraza hilo litaendeshea shughuli zake.
    Hatujawahi kushuhudia toka kwa Baraza Kuu la Jumuia na Taasisi na Tawi lake linalojiita Jumuiya na Taasisi jambo lolote la maendeleo ya Kiislamu zaidi ya ghasia za maandamano, kupora Misikiti na kudandia matukio na kuwachangisha Waislamu fedha mwishoni mwa maandamano kwa kuwatapeli Waislamu fedha zao ambazo huishia mifukoni mwa Ponda na wenzake.
   Habari mbalimbali zinazoendelea kuripotiwa katika kadhia hii zinajaribu kujenga taswira inayoonyesha kwamba mgogoro uliopo ni baina ya “WAISLAMU NA BAKWATA”.  Taswira hii si sahihi ni potofu.
    Napenda kuchukua fursa hii kuufahamisha umma wa kiislamu ukweli na hali halisi ya kadhia hii kama ifuatavyo:
1.             Kikundi hiki kinachojitambulisha kwa jina la JUMUIYA NA TAASISI ZA KIISLAMU si kikundi kinachowakilisha Waislamu wote wa nchi hii bali ni KIGENGE CHA WATU WACHACHE wenye kufuata madhehebu ya MAWAHABI ambao kwa mujibu wa ITIKADI yao wanaamini kwamba Muislamu yeyote asiefuata ITIKADI yao basi huyo sio MUISLAMU na hafai kuwa kiongozi kwa ngazi yoyote ile.
2.             Kikundi hiki ambacho kimejivika vazi la kuendesha wanachokiita Harakati za Kiislamu ni kikundi cha watu wachache ambao hawataki kufuata UTARATIBU uwe wa kidini wala kutii mamlaka ya dola na wanataka matakwa yao yawe ndio utaratibu na wanalazimisha watu wote wayafuate.
3.             Vurugu, chokochoko na ghasia za uvamizi hazikuanzia BAKWATA, wamekuwa wakifanya hivyo sehemu mbalimbali Mikoani  kwa kuvamia na kuteka Miskiti na kuwaondoa viongozi waliochaguliwa kihalali kwa nguvu na udhalilishaji mkubwa sana na hatimae kupora na kuhodhi rasilimali za Misikiti hiyo.
4.             Wamekuwa wakiendesha mafunzo ya KARATE kwenye Misikiti hiyo waliyoiteka na kuikalia kimabavu kwa vijana wao ili waweze kuendeleza dhulma yao ya uporaji wa Misikiti na vituo vingine vya Kiislamu.
5.             Nikiwa kiongozi Mkuu wa Waislamu katika nchi hii nawataka Waislamu wa Tanzania kutambua ya kwamba vitendo vya vurugu na ghasia na vya uvunjaji wa sheria vinavyofanywa na Ponda na kikundi chake kamwe havina uhusiano wowote na dini ya Kiislamu.  Ni vitendo vinavyokiuka maadili ya Uislamu na kuupa sura mbaya Uislamu miongoni mwa jamii na mataifa.  Kwa sababu hiyo nawaonya na kuwatahadharisha Waislamu wa madhehebu zote kujitenga mbali na matendo ya uvunjaji sheria wa kikundi hiki cha watu wachache.
6.             Kwa mujibu wa Katiba ya nchi yetu kila kundi la kidini lina haki ya kuendesha kwa Uhuru shughuli zake za kidini.  Na tunashuhudia katika nchi yetu madhehebu yote ya kidini yakiendesha shughuli zao bila kuingilia madhehebu nyingine mfano Shia Ithaashiria, Bohora, Ibadh, Hannafii na mengineyo.  Madhehebu yote hayo yamekuwa yakiendesha shughuli zao bila kuingiliana na wenzao isipokuwa kikundi hiki cha watu wachache ambao madhehebu yao ni WAHABI na wakati mwingine wanajiita ANSAR SUNNA.
7.             Nawatahadharisha Waislamu wote nchini kwamba Ponda Issa Ponda si mwanachuoni, si Sheikh, hakusoma elimu ya msingi ya kidunia wala ya kidini, hata Qur’an hajui kusoma.  Anajaribu kuwatumia Waislamu kwa manufaa yake binafsi.
8.             Mwisho tunavipongeza vyombo vya dola na Serikali kwa ujumla kwa namna walivyoshughulikia ghasia za kikundi hiki kwa busara, hekima, na subira kubwa waliyotumia pale Wizara ya Mambo ya ndani.  Nakitahadharisha kikundi hiki kinachojishughulisha na harakati za vurugu na ghasia wasiutumie vibaya uvumilivu wa hali ya juu ulioonyeshwa na vyombo vya dola wakati wa maandamano ya kuvamia Wizara ya Mambo ya Ndani tarehe 07/09/2012.  Kitendo kile kilikuwa ni kuvunja sheria za nchi na UISLAMU unatutaka Waislamu kuheshimu mamlaka iliyoko madarakani.
9.             Natoa wito kwa vyombo vya dola kwamba viangalie utaratibu wa kuwashughulikia watu wanaoleta vurugu kwa kujifanya viongozi wa taasisi hewa na kutumia taasisi hizo hewa kutoa matamko ya kutishia kuwaondoa viongozi halali wa taasisi zinazosajiliwa na kuendesha shughuli zake kwa mujibu wa sheria za nchi.
10.         Naviomba vyombo vya dola vielewe kwamba si kila linalofanywa kwa kisingizio cha dini kwamba jambo hilo ni la dini.  Kwa msini huo tunaomba vyombo vya dola visisite kuchukua hatua dhidi ya mtu, kikundi kinachojaribu kutumia anuani ya Uislamu katika kutenda matendo ya uvunjaji wa sheria na hivyo kuhatarisha hali ya amani na utulivu iliyopo hapa nchini.  Uislamu ni AMANI.  Hata jina lenyewe linatafsirika kuwa ni amani.
11.         Nazikumbusha taasisi zote za Kiislamu nchini kila moja kuheshimu na kutekeleza madhumuni ya kuanzishwa kwa taasisi husika kwa mujibu wa malengo yaliyoainishwa katika Katiba zao.  Hakuna taasisi yoyote iliyosajiliwa nchini iliyo na haki ya kuondoa, kuweka au kubadilisha uongozi wa Taasisi nyingine.
12.         Baraza Kuu la Waislamu wa Tanzania halitosimama kutetea kundi lolote litakalojinasibisha na Uilsmau katika vitendo vyovyote vile vinavyokiuka misingi ya dini, sheria za nchi, kusababisha vurugu na kuvunja amani katika nchi.

Wabillah Tawfiq,
 Sheikh Issa bin Shaaban Simba, MUFTI NA SHEIKH MKUU WA TANZANIA

No comments:

Post a Comment