TANGAZO


Monday, January 16, 2012

Serikali yapewa masaa 72, kuwarejesha madaktari Muhimbili

 
Dk. Mtasiwa asimamishwa uanachama kwa mwaka mmoja
JK atakiwa kuwatafutia kazi nyingine Nyoni, Dk. Mtasiwa.
CHAMA cha Madaktari Tanzania (MAT), kimeipa Serikali masaa 72, iwe imekwisha kuwarejesha Hospitali ya Taifa Muhimbili, Madaktari wanafunzi ililiowafukuza na kuwaondolea udaktari kutokana na kugoma wakati walipokuwa wakidai malipo yao.
Tamko hilo, limetolewa na Rais wa Chama hicho, Dk. Namala Mkopi, wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam leo.
Aidha, Chama hicho kimtaka Rais Jakaya Kikwete, kuwatafutia kazi nyingine, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Blandina Nyoni pamoja na Mganga Mkuu wa Serikali, Dk. Deo Mtasiwa kwa kosa la kumshauri vibaya Waziri wa wizara hiyo, Dk. Hadji Mponda. Alisema Dk. Mponda anasamehewa, kwani hajui alitendalo, ila wanamtaka kuwaomba radhi kwa kuwaita madaktari wenzao kuwa si madaktari bali bado wangali wanafunzi.
Rais huyo, alitangaza pia kuwa kimemfutia uanachama kwa muda wa mwaka mmoja, Mganga Mkuu wa Serikali, Dk. Mtasiwa kwa kosa lake la kuusaliti udaktari kutokana na kukiuka kiapo

cha chake kinachosema kuwa Madaktari wote ni ndugu na nitawatendea haki, kama dada na kaka.
Alisema endapo Dk. Mtasiwa ataendelea na tabia hiyo, ya kudharau taaluma ya udakatari, basi chama hicho, kitaamua kumfukuza kabisa na kumuweka kwenye mtandao wa madaktari duniani, ili iwe fundisho kwa madaktari wengine wenye tabia kama hiyo.
Dk. Mkopi alisema kuwa chama kimesikitishwa sana na kwamba hawaoni ni kwa nini Serikali imeamua kuwaadhibu madaktari wenzao waliokuwa wakidai haki yao ya msingi na kuwaacha kuwaadhibu watu waliosababisha ucheleweshwaji wa makusudi wa kutowalipa malipo yao.
Aliwataka viongozi kuacha tabia ya kutumia siasa kuingilia masuala ya kitaaluma na kwamba wanavyofanya hivyo, wajue kwamba wanaowakomoa si madaktari bali ni wagonjwa ambao ni ndugu na jamaa zetu sote.

Alisema kitendo cha kuwaondoa madakari zaidi ya 200, tayari kimeanza kuleta athari kwa madakatari mabingwa waliokuwa wakisaidia kazi na kwamba kibaya zaidi kusababisha wagonjwa wengi kufariki hospitalini hapo.
"Kitendo cha Serikali kuwaondoa madaktari wenzetu katika Hospitali ya Muhimbili na kuamua kuwapangia Hospitali zingine si kizuri, kwani baadhi ya hospitali walizohamishiwa hakuna nafasi wala mambo wanayotakiwa kujifunza, hivyo mpaka sasa hakuna wanalolifanya," alisema. Chama hicho, kimeitisha mkutano mkubwa wa madakari wote nchini, Jumatano ijayo utakaofanyika, Dar es Salaam, ambao utazungumzia mambo kadhaa, likiwemo la madakatari hao.

Alitaja baadhi ya ajenda watakazozungumzia kwenye mkutano huo, kuwa ni pamoja na hatima ya heshima ya Udaktari, Ulipaji posho kwa Madaktari, Mshahara uendane na elimu, Majukumu na hadhi ya Udaktari, Madaktari kupewa nyumba, posho ya mazingira magumu, posho ya mazingira hatarishi pamoja na uhamishaji ovyo wa madaktari.

No comments:

Post a Comment