TUME ya Kikristo ya Huduma za jamii (CSSC), inatarajia kuadhimisha miaka ishirini na mitano (25), tangu kuanzishwa kwake mwaka 1992, maadhimisho yatakayofanyika kwa siku mbili tarehe 21 na 22 mwezi Februari katika ukumbi wa Diamond Jubelee na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam leo, Mkurugenzi Mtendaji wa tume hiyo, Peter Maduki amesema, maadhimisho hayo yatatumika kutafakari na kuangalia mafanikio na changamoto zinazoikabili sekta ya afya na Elimu nchini pamoja na kuangalia mchango unaotolewa na taasisi za Mkanisa katika maeneo husika.
“Tunaadhimisha miaka 25 ya kuhudumia jamii kwakuwa sisi ni wadau wakubwa katika kushirikiana na serikali kutoa huduma za jamii, ndiyo maana ukiangalia takwimu, utaona kuwa Makanisa yanamiliki asilimia 14 ya taasisi zote zinazotoa huduma ya afya hapa nchini, wakati huohuo makanisa yanamiliki takribani asilimia 42 ya hospitali zote nchini,” alisema Maduki.
Akizitaja changamoto wanazokabiliana nazo kwa kipindi chote hicho, mkurugenzi Maduki alisema kuwa Uelewa, Umaskini na Utashi miongoni mwa watendaji na wananchi vimekuwa ni kiwazo kikubwa ambacho hata hivyo alisema wanaendelea kupambana navyo ili kuhakikisha Kanisa linaendelea kutoa huduma zake kwa jamii kwakuwa huo ni wito wake.
Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii (CSSC) inaundwa na Baraza la Maaskofu katoliki Tanzania (TEC) na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) na ilianzishwa mwaka 1992, kwa dhumuni la kuratibu na kusimamia huduma za kijamii zitolewazo na Taasisi za makanisa hususani za Elimu na Afya Nchini.
No comments:
Post a Comment