Na Jonas Kamaleki
MKUU wa Mkoa wa
Arusha, Mrisho Gambo amedhamiria kukomesha vitendo vya uchomaji moto mashule
mkoani humo ili kuondoa hofu kwa wanafunzi na kuwawekea mazingira mazuri ya
kusomea.
Akizungumza baada ya
kuapishwa leo Ikulu jijini Dar es Salaam, Gambo amesema kuwa atafanya kila
liwezekanalo kuwasaka na kuwakamata wanaojihusisha na vitendo hivyo na
kuwafikisha mahakamani ili wachukuliwe hatua za kisheria.
“Tumechoka na hali
hii ya kila kukukicha kusikia matukio ya shule kuungua moto kwa hiyo tutaweka
ulinzi wa uhakika katika shule za bweni na hosteli ili kuzuia vitendo viovu”,
alisema Gambo.
Gambo amesema kuwa akiwa
Mkuu wa Mkoa atahakikisha anasimamia utekelezaji wa vipaumbele vya Taifa kama
Elimu bure, ajira kwa vijana, kujenga uchumi wa viwanda na kuboresha maisha ya
wananchi hasa wa hali ya chini.
Gambo Mrisho
ameapishwa leo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe
Magufuli kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha baada ya aliyekuwa mkuu wa mkoa huo, Felix
Ntibenda Kijiko uteuzi wake kutenguliwa.
Kwa upande wake,
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
(TAMISEMI), Suleiman Jafo amesema kuwa Wizara yake kwa sasa inafanya kazi ya
kuondoa watumishi hewa na kupinga vikali ufanyaji kazi kimazoea.
“Lengo la Serikali ya
Awamu ya Tano ni kufanya kazi kwa maslahi ya wananchi na kuondoa ubinafsi
tuliourithi”, alisema Jafo.
Aidha, Jafo amesema
wapo watu waliokuwa wanahakikisha wanafanya kila liwezekano kutumia ofisi zao
kujinufaisha, na kuongeza kuwa watu hao inabidi wajiondoe haraka au
wataondolewa.
Kuhusu walioongeza
majina ya wanafunzi hewa ili kujipatia vipato, Jafo amesema anawatafuta na
wakibainika hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.










No comments:
Post a Comment