Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Zena Kongoi (wa pili kutoka kulia) akiwa na baadhi ya Wajumbe wanawake wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, muda mfupi kabla ya kushuka chini ya ardhi kwa kutumia Kiberenge maalumu ili kujionea mahala kunakochimbwa madini ya Tanzanite.
Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Zena Kongoi, akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi wa Mgodi wa Tanzanite One kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini hivi karibuni. Kamati hiyo ilifanya ziara Mgodini hapo kujionea namna unavyofanya kazi.
Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Susan Kiwanga, akiuliza swali wakati wa kikao cha majumuisho baada ya ziara ya kamati hiyo katika Migodi mbalimbali inayochimba madini ya Tanzanite Mirerani hivi karibuni.
Na Veronica
Simba - Mirerani
IMEELEZWA kuwa, hatua ya Shirika la Madini la Taifa (Stamico), kuweka wawakilishi
wake katika Mgodi wa Tanzanite uliopo katika eneo la Mirerani Kitalu C,
imeonesha mafanikio makubwa ikiwemo kupungua kwa wizi wa ndani na kuimarika kwa
mifumo ya uendeshaji Mgodi.
Aidha,
imeelezwa kuwa katika kipindi cha ubia wa Shirika hilo na Kampuni ya Madini ya
Tanzanite One (TML), Juni 2013 hadi Februari 2016, jumla ya karati 30,
674, 250 za Tanzanite zimezalishwa na kuuzwa kwa thamani ya Dola za Marekani
milioni 13.64.
Kaimu
Mkurugenzi Mkuu wa STAMICO, Zena Kongoi alisema hayo jijini Arusha hivi
karibuni, wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini
katika Migodi mbalimbali inayochimba madini ya Tanzanite ukiwemo Mgodi wa
Tanzanite One.
Alisema
kuwa Mgodi umeweza kuchangia pato la Taifa kwa kurejesha mrabaha wa asilimia
Tano (5.0) ya mauzo ambayo ni sawa na Dola za Marekani 481, 271.04 kwa
Serikali.
Vilevile,
Kongoi alitaja mafanikio mengine yaliyopatikana katika Mgodi huo kwa mwezi
Februari mwaka huu kuwa ni pamoja na kulipa ushuru wa huduma wa asilimia
0.3 ya mauzo kwa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, kiasi cha Dola za Marekani
32, 769.75.
Akielezea
zaidi kuhusu utaratibu wa Shirika hilo kusimamia kwa karibu maslahi yake na
Serikali kwa ujumla katika kuendesha na kusimamia mradi huo, Mkurugenzi huyo wa
STAMICO alisema kuwa kulingana na maeneo ya usimamizi kuwa mengi mgodini,
kuanzia mwezi Machi mwaka huu, Shirika limeongeza idadi ya watumishi uangalizi
na usimamizi kufikia Sita.
"Awali,
tulipeleka Maafisa watatu kufanya kazi hiyo ya uangalizi na usimamizi. Sasa
tumeongeza idadi hiyo mara mbili ili kuleta ufanisi zaidi," alisema
Kongoi.
Akizungumzia
majukumu ya Maofisa hao, Kongoi alisema kuwa kwa mujibu wa kifungu namba 12 cha
mkataba wa kuendeleza Mgodi huo, timu ya wataalam wenye fani mbalimbali
iliundwa ikijumuisha wahandisi, wajiolojia, wachenjuaji na wahasibu ambao
jukumu lao kubwa ni kufuatilia, kusimamia na kushauri juu ya mwenendo wa
uendeshaji wa shughuli za kila siku za Mgodi pamoja na utekelezaji wa masuala
ya mkataba wa ubia.
STAMICO
iliingia ubia na Kampuni ya Tanzanite One Mining Ltd (TML) mwaka 2013 kwa
uwiano wa 50 kwa 50 ili kumiliki leseni ya uchimbaji madini na kuendeleza Mgodi
wa Tanzanite katika eneo la Mirerani Kitalu C.
No comments:
Post a Comment