Waziri Mkuu Mizengo Pinda
Na Magreth Kinabo
WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda kesho (leo Jumatano, Mei 5 2015) anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya siku ya Wakunga Duniani yatakayofanyika kitaifa Mkoani Mara.
Hayo yalisemwa leo Jumatatu (Mei 4, 2015) na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dkt. Seif Rashid wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam, ambapo alisema maadhimisho hayo yataambatana na utoaji wa huduma mbalimbali za mama na mtoto sambamba na kongamano hilo la Wakunga.
Maadhimisho hayo ambayo yatafanyika katika viwanja vya Mkendo katika Manispaa ya Musoma kaulimbiu yake ni “ Wakunga kwa Maendeleo ya Kinaki Kijacho”.
“Kauli mbiu hii inalenga kutambua umuhimu wa wakunga katika kuokoa maisha ya wakinamama na watoto wachanga,”alisema Dkt.Rashid. Aliongeza kwamba kauli mbiu hiyo inakumbusha umuhimu wa wakunga wenye taaluma katika kuleta matumaini kwa wakinamama watoto wachanga na familia.
Kwa mujibu wa Dkt. Rashid kwa upande wa elimu Mkunga anapaswa kuwa na vigezo vinavyotambulika kimataifa vilivyopitishwa na Muungano wa Vyama vya Wakunga Dunia(ICM) uliotoa mwongozo wa mtaala wa kufundishia wakunga na wa ujuzi na stadi za msingi.
Dkt. Rashid aliongeza kwamba wizara yake itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha wakunga wenye ueredi unaokubalika na viwango vya kimataifa ili kuokoa misha ya mama na mtoto.
Aidha Dkt. Rashid kwa mujibu wa tafiti zilizofanywa na nchi 72 zimeonyesha kwamba upatikanaji wa huduma muafaka za ukunga umewezesha kupunguza kiwango cha vifo vya wakina mama vinavyotokana na uzazi kwa wastani wa asilimia tatu kwa mwaka kuanzia mwaka 1990.


No comments:
Post a Comment